Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Micronesia

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Micronesia

KATHERINE alilelewa nchini Marekani na alipokuwa na umri wa miaka 16 alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Alihubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme katika eneo lake ijapokuwa watu hawakuitikia vizuri. Anasema hivi: “Nilisoma masimulizi kuhusu watu waliomwomba Mungu atume mtu awasaidie kumjua. Nilitamani sana kukutana na mtu kama huyo, lakini haikuwezekana.”

Baada ya kuhubiri katika eneo hilo kwa miaka mingi, Katherine alianza kufikiria kuhamia eneo ambalo watu wangeitikia vizuri zaidi ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, alijiuliza ikiwa atazoea mazingira mapya. Aliwahi kuwa mbali na familia yake kwa majuma mawili tu, na kila siku alitamani sana kurudi nyumbani. Hata hivyo, alichochewa zaidi na tamaa yake ya kupata shangwe inayotokana na kuwasaidia wale wanaomtafuta Yehova. Baada ya kufikiria maeneo kadhaa ambayo angeweza kuhamia, aliandikia ofisi ya tawi ya Guam na akapewa habari alizohitaji. Mnamo Julai 2007, akiwa na umri wa miaka 26, Katherine alihamia Saipan, kisiwa kilicho katika Bahari ya Pasifiki, kilomita 10,000 hivi kutoka nyumbani kwao. Mambo yalikuwaje alipohamia eneo hilo?

SALA MBILI ZAJIBIWA

Muda mfupi baada ya kufika katika kutaniko lake jipya, Katherine alikutana na Doris, mwanamke mwenye umri wa miaka zaidi ya 40 aliyekubali kujifunza Biblia. Baada ya kujifunza naye sura tatu za kwanza za kitabu Biblia Inafundisha, Katherine alianza kuwa na wasiwasi. Anasema hivi: “Doris alikuwa mwanafunzi mzuri na nilitaka aendelee kujifunza. Sikuwahi kamwe kuongoza funzo la Biblia kwa ukawaida na nilihisi kwamba Doris alihitaji kufundishwa na dada mwenye uzoefu zaidi, aliye na umri kama wake.” Katherine alitoa sala ili Yehova amsaidie kupata dada atakayefaa kujifunza na Doris. Kisha akaamua kumweleza Doris kuhusu mpango huo.

Katherine anasema hivi: “Kabla ya kumjulisha jambo hilo, Doris aliniambia kwamba angependa kunieleza tatizo fulani alilokabili. Baada ya kumsikiliza, nilimweleza jinsi Yehova alivyonisaidia kushughulikia hali kama hiyo maishani mwangu. Alinishukuru sana.” Kisha Doris akamwambia Katherine hivi: “Yehova anakutumia unisaidie. Siku ya kwanza ulipofika nyumbani kwangu, nilikuwa nimesoma Biblia kwa saa nyingi. Nilikuwa nikilia na kumwomba Mungu amtume mtu  atakayenisaidia kuielewa Biblia. Kisha ukabisha mlango wangu. Yehova alikuwa amejibu sala yangu!” Katherine alitokwa na machozi aliposimulia pindi hiyo yenye kugusa moyo. Anasema hivi: “Maneno ya Doris yalikuwa jibu la sala yangu. Niliona wazi kwamba Yehova alitaka niendelee kujifunza na Doris.”

Doris alibatizwa mwaka wa 2010, na sasa anaongoza mafunzo mengi ya Biblia. Katherine anasema hivi: “Ninafurahi sana kuona kwamba tamaa yangu ya muda mrefu ya kumsaidia mtu mmoja mnyoofu awe mtumishi wa Yehova ilitimia.” Leo, Katherine anafurahi kutumika akiwa painia wa pekee katika kisiwa cha Pasifiki cha Kosrae.

CHANGAMOTO TATU —NA JINSI YA KUKABILIANA NAZO

Akina ndugu na dada zaidi ya mia moja (wenye umri wa kati ya 19 hadi 79) kutoka nchi nyingine wametumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi katika Micronesia. Wafanyakazi hao wenye bidii wanahisi kama Erica, aliyehamia Guam mwaka wa 2006 akiwa na miaka 19. Anasema hivi: “Inafurahisha sana kufanya upainia katika eneo lenye watu wenye kiu ya kujua kweli. Ninashukuru sana kwamba Yehova amenisaidia kufanya utumishi huu. Hii ndiyo njia bora zaidi ya maisha!” Leo, Erica anatumika kwa shangwe akiwa painia wa pekee huko Ebeye katika Visiwa vya Marshall. Bila shaka, utakabili changamoto unapotumika katika nchi nyingine. Acheni tuchunguze changamoto tatu na jinsi wale waliohamia Micronesia wanavyokabiliana nazo.

Erica

Maisha. Baada ya kufika katika kisiwa cha Palau mwaka wa 2007, Simon aliyekuwa na umri wa miaka 22, alitambua mara moja kwamba mshahara ambao angepata ulikuwa mdogo sana ukilinganishwa na aliokuwa akipata nchini Uingereza. Simon anasema hivi: “Nilijifunza kutonunua kila kitu nilichotaka. Sasa, ninachagua kwa uangalifu chakula ninachonunua na kununua vitu vya bei nafuu. Kitu kinapoharibika, ninatafuta spea na mtu wa kunisaidia kukirekebisha.” Kurahisisha maisha kulimsaidiaje? Anasema hivi: “Kulinisaidia kujua mambo ya maana zaidi maishani na jinsi ninavyoweza kuishi bila vitu vingi. Nimejionea mara nyingi Yehova akinitegemeza maishani mwangu. Kwa miaka saba ambayo nimetumika hapa, sijakosa chakula na mahali pa kulala.” Kwa kweli, Yehova huwategemeza wanaoishi maisha rahisi kwa sababu ya kutafuta kwanza Ufalme.—Mt. 6:32, 33.

Kutamani kurudi nyumbani. Erica anasema hivi: “Nina uhusiano wa karibu sana na familia yangu na nilikuwa na wasiwasi kwamba kuishi mbali nao kungeathiri huduma yangu.” Alifanya nini ili kujitayarisha? Anasema hivi: “Kabla ya kuhama, nilisoma makala za Mnara wa Mlinzi zilizozungumzia tamaa ya kurudi nyumbani. Kufanya hivyo kulinisaidia sana kutayarisha moyo wangu kukabili hali hiyo. Katika makala moja, mama mmoja alimhakikishia binti yake kwamba Yehova angemtunza kwa kumwambia  hivi: ‘Yehova aweza kukutunza vyema zaidi ya vile niwezavyo.’ Uhakikisho huo uliniimarisha sana.” Hannah na mume wake, Patrick, wanatumika katika eneo la Majuro katika Visiwa vya Marshall. Kuwakazia fikira ndugu na dada kutanikoni humsaidia Hannah kutotamani sana kurudi nyumbani. Anasema hivi: “Ninamshukuru Yehova daima kwa undugu wetu wa ulimwenguni pote kwa sababu wao pia ni familia yangu. Bila utegemezo wao wa upendo, singeweza kamwe kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri.”

Simon

Kuzoea eneo. Simon anasema hivi: “Unapofika nchi nyingine, karibu kila kitu ni tofauti. Nyakati nyingine mimi hutamani kuchekesha watu lakini hawanielewi.” Erica anasema hivi: “Mwanzoni, ilikuwa vigumu kuzoea, lakini hilo lilinisaidia kufikiria kusudi langu la kuhama. Nilihama ili nitimize mengi zaidi kwa ajili ya Yehova, si kwa sababu za kibinafsi.” Anaongezea hivi: “Baada ya muda nilipata marafiki wazuri sana ninaowathamini.” Simon alijitahidi kujifunza lugha ya Kipalau inayomsaidia ‘kupanuka’ kuwaelekea ndugu na dada wenyeji. (2 Kor. 6:13) Akina ndugu walimpenda sana kwa sababu ya jitihada zake za kujifunza lugha hiyo. Naam, ndugu kutoka nchi nyingine wanapofanya kazi na ndugu wenyeji, wote hupata thawabu ya kuwa na marafiki wa karibu kutanikoni. Ni thawabu gani nyingine wanazopata wale wanaojitoa kwa hiari kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi?

‘KUVUNA KWA WINGI’

Mtume Paulo alisema hivi: “Yeye anayepanda kwa wingi atavuna pia kwa wingi.” (2 Kor. 9:6) Bila shaka kanuni hiyo inawahusu wale wanaopanua huduma yao. Ni matunda gani ‘wanayovuna kwa wingi’ katika Micronesia?

Patrick na Hannah

Katika Micronesia, bado kuna fursa nyingi za kuanzisha mafunzo ya Biblia na kuona watu wakijifunza, wakitumia kweli ya Neno la Mungu, na kufanya maendeleo ya kiroho. Patrick na Hannah walihubiri pia Angaur, kisiwa kidogo chenye wakaaji 320. Baada ya kuhubiri katika kisiwa hicho kwa miezi miwili, walikutana na mama fulani asiye na mume. Alikubali mara moja kujifunza Biblia, akakubali kweli kwa hamu, na kufanya mabadiliko makubwa maishani mwake. Hannah anasema hivi: “Kila baada ya funzo, tulipokuwa tukiondoka kwake kwa baiskeli zetu, tulisema hivi: ‘Asante Yehova!’” Anaongezea hivi: “Ninajua kwamba Yehova angemvuta mwanamke huyo kwa njia moja au nyingine, hata hivyo kwa sababu tulijitolea katika eneo lenye uhitaji mkubwa zaidi, tulimpata na kumsaidia kondoo huyo kumjua Yehova. Hilo ni mojawapo ya mambo yenye kuthawabisha zaidi maishani mwetu!” Kama Erica anavyosema, “unapomsaidia mtu kumjua Yehova, unapata shangwe isiyo na kifani!”

JE, UNAWEZA KUSHIRIKI?

Nchi nyingi zina uhitaji wa wahubiri zaidi wa Ufalme. Je, unaweza kuwa miongoni mwa wale wanaohamia katika eneo linalohitaji msaada? Mwombe Yehova aimarishe tamaa yako ya kupanua huduma yako. Zungumzia jambo hilo na wazee wa kutaniko, mwangalizi wa mzunguko, au wale ambao wamepata pendeleo la kutumika katika nchi yenye uhitaji. Unapofanya mipango, andikia ofisi ya tawi inayosimamia eneo unalotaka kuhamia na kuomba habari zaidi. * Wewe pia unaweza kujiunga na maelfu ya akina ndugu na dada—wazee na vijana, waliofunga ndoa na waseja—wanaojitoa kwa hiari, ili uonje shangwe ya ‘kuvuna kwa wingi.’

^ fu. 17 Tazama makala yenye kichwa, “Je, Unaweza ‘Kuvuka Uingie Makedonia’?” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Agosti 2011.