Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alikuwa wa Familia ya Kafaya

Alikuwa wa Familia ya Kafaya

Pindi fulani, vitu vya kale huthibitisha moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kuwapo kwa mtu fulani anayetajwa katika Biblia. Kwa mfano, katika mwaka wa 2011, wasomi Waisraeli walichapisha habari kuhusu ugunduzi kama huo. Lilikuwa sanduku la mifupa lililotengenezwa kwa mawe ya chokaa, lililodumu kwa miaka 2,000 ambamo mifupa ya watu waliokufa iliwekwa baada ya wafu hao kuoza.

Sanduku hilo lina maandishi haya: “Miriamu binti ya Yeshua mwana wa Kayafa, kuhani wa Maazia kutoka Bethimri.” Kayafa ndiye kuhani mkuu Myahudi aliyesikiliza kesi ya Yesu na kutoa hukumu. (Yoh. 11:48-50) Mwanahistoria Flavio Yosefo anamtaja kuwa “Yosefo aliyeitwa Kayafa.” Ni wazi kwamba sanduku hilo ni la mtu wake wa ukoo. Kwa kuwa maandishi yaliyo juu ya sanduku lililogunduliwa mapema lililodhaniwa kuwa la kuhani mkuu yanamwita Yehosef bar Caiapha, au Yosefu, mwana wa Kayafa, * Miriamu alikuwa na uhusiano wa kiukoo na Kayafa.

Kulingana na habari iliyotolewa na Shirika la Kuhifadhi Vitu vya Kale nchini Israel (IAA), sanduku la mifupa ya Miriamu lilichukuliwa kutoka mikononi mwa wezi waliopora kutoka katika kaburi la kale. Uchunguzi uliofanywa wa sanduku hilo na maandishi yake unathibitisha kwamba ndilo sanduku lenyewe.

Pia, tunajifunza jambo lingine jipya kutokana na sanduku hilo. Linarejelea “Maazia,” aliyekuwa wa mwisho katika migawanyiko 24 ya makuhani waliotumika kwa zamu katika hekalu la Yerusalemu. (1 Nya. 24:18) Maandishi yaliyo juu ya sanduku hilo yanaonyesha kwamba “familia ya Kayafa ilikuwa na uhusiano na mgawanyiko wa familia ya Maazia,” linasema shirika hilo la IAA.

Maandishi hayo yanamtaja pia Bethimri. Tunaweza kufasiri maandishi hayo kwa njia mbili hivi. Shirika la IAA linasema hivi: “Uwezekano wa kwanza ni kwamba huenda Bethimri ni jina la familia ya kikuhani, yaani, wana wa Imeri (Ezra 2:36-37; Neh. 7:39-42) ambao wazao wake wanatia ndani washiriki wa mgawanyiko wa Maazia. Uwezekano wa pili ni [kwamba Bethimri] ni sehemu aliyozaliwa Miriamu au familia yake yote.” Vyovyote vile, sanduku la mifupa ya Miriamu linathibitisha kwamba Biblia inazungumzia watu halisi kutoka katika familia halisi.

^ fu. 3 Kuhusiana na sanduku la mifupa ya Kayafa, tazama makala yenye kichwa “Kuhani Mkuu Aliyemhukumu Yesu,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 2006, ukurasa wa 10-13.