Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Lefèvre d’Étaples​—Alitaka Watu wa Kawaida Waelewe Neno la Mungu

Lefèvre d’Étaples​—Alitaka Watu wa Kawaida Waelewe Neno la Mungu

ILIKUWA Jumapili asubuhi mwanzoni mwa miaka ya 1520, wakazi wa Meaux, mji mdogo ulio karibu na Paris, hawakuamini mambo waliyosikia kanisani. Walisikia vitabu vya Injili vikisomwa kwa lugha yao ya asili, yaani, Kifaransa badala ya Kilatini!

Mtafsiri wa Biblia aliyeongoza kazi hiyo, Jacques Lefèvre d’Étaples (Kilatini, Jacobus Faber Stapulensis), baadaye alimwaandikia hivi rafiki yake wa karibu: “Inashangaza sana kuona jinsi Mungu anavyowasaidia watu wengi kuelewa Neno lake.”

Wakati huo, Kanisa Katoliki na wanatheolojia wa Paris walipinga kutumia Biblia zilizotafsiriwa kwa lugha zilizozungumza na watu wengi. Kwa hiyo, ni nini kilichomchochea Lefèvre atafsiri Biblia katika Kifaransa? Alifaulu jinsi gani kuwasaidia watu wengi waelewe Neno la Mungu?

ALITAFUTA MAANA SAHIHI YA MAANDIKO

Kabla ya kuwa mtafsiri wa Biblia, Lefèvre alijitahidi kurudisha maana ya awali ya maandishi ya kale ya falsafa na theolojia. Alitambua kwamba kwa karne nyingi maandishi ya kale yalikuwa yamepotoshwa. Alipokuwa akitafuta maana sahihi ya maandishi ya kale, alianza kujifunza kwa makini Biblia iliyokuwa ikitumiwa na Kanisa Katoliki, yaani, Vulgate ya Kilatini.

Kuchunguza kwa bidii Maandiko kulimfanya afikie mkataa kwamba “kujifunza kweli za Neno la Mungu huleta . . . furaha kubwa.” Kwa hiyo, Lefèvre akaacha kujifunza falsafa na kuelekeza nguvu zake zote katika kutafsiri Biblia.

Mwaka wa 1509, Lefèvre alitoa chapisho lililolinganisha tafsiri tano za Zaburi za Kilatini, * kutia ndani marekebisho yake ya Vulgate. Tofauti na wanatheolojia wa wakati huo, Lefèvre alijitahidi kutafuta “maana halisi” ya Maandiko. Mbinu yake ya kutafsiri Maandiko iliwachochea wasomi wengine wa Biblia.—Ona Sanduku “ Jinsi Martin Luther Alivyochochewa na Lefèvre.”

Sanduku lenye majina ya cheo ya Mungu katika Zaburi, kama yanavyopatikana katika kitabu Fivefold Psalter, Toleo la mwaka 1513

Lefèvre alikuwa Mkatoliki, na aliamini kwamba ingewezekana kulifanya upya kanisa ikiwa watu wa kawaida watafundishwa Maandiko ifaavyo. Lakini watu wa kawaida wangenufaikaje na Maandiko, kwa kuwa maandishi hayo matakatifu yaliandikwa kwa Kilatini?

TAFSIRI YA BIBLIA ILIYOPATIKANA KWA WOTE

Utangulizi wa vitabu vya Injili ulifunua wazi tamaa ya Lefèvre ya kutaka watu wote wawe na Biblia katika lugha yao

Kwa kuwa Lefèvre alilipenda sana Neno la Mungu, aliazimia kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo wapate Biblia. Hivyo, Juni 1523, alichapisha tafsiri ya Kifaransa ya vitabu vya Injili katika mabuku mawili madogo. Biblia hiyo iligharimu nusu ya bei ya tafsiri ya kawaida, na hivyo kuwawezesha watu wengi kupata Biblia.

Watu wa kawaida walifurahia sana. Wanaume kwa wanawake walitamani sana kusoma masimulizi ya Yesu katika lugha yao, na nakala 1,200 zilizochapishwa mara ya kwanza zilikwisha baada ya miezi michache tu.

MSIMAMO DHABITI KUELEKEA BIBLIA

Katika utangulizi wa Injili, Lefèvre alieleza kwamba alitafsiri Injili hiyo kwa Kifaransa ili “washiriki wa kawaida” wa kanisa “waelewe mafundisho ya Injili kama wale waliosoma kwa lugha ya Kilatini.” Lakini kwa nini Lefèvre alitamani sana kuwasaidia watu wa kawaida waelewe mambo ambayo Biblia inafundisha?

Lefèvre alijua vizuri kwamba mafundisho na falsafa za wanadamu ziliathiri Kanisa Katoliki. (Marko 7:7; Wakolosai 2:8) Aliamini kwamba muda ulikuwa umefika wa Injili “kutangazwa ulimwenguni kote, ili watu wasidanganywe tena na mafundisho ya uwongo ya wanadamu.”

Lefèvre pia alijitahidi kufunua maoni yenye makosa ya wale waliopinga kutafsiri Biblia katika Kifaransa. Alifichua unafiki wao, kwa kusema hivi: “Watawafundishaje [watu] kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru, ikiwa wanapinga watu wa kawaida kuona na kusoma Injili ya Mungu kwa lugha yao wenyewe?”—Waroma 10:14.

Haishangazi kwamba muda mfupi baadaye, wanatheolojia wa Chuo Kikuu cha Sorbonne, Paris, walijaribu kumnyamazisha Lefèvre. Mnamo Agosti 1523, walipinga tafsiri na habari za Biblia zilizokuwa katika lugha za asili, wakidai kuwa tafsiri hizo ni “hatari kwa kanisa.” Bila msaada wa Mfalme wa Ufaransa, Francis wa I, Lefèvre angehukumiwa kuwa mwasi.

MTAFSIRI AKAMILISHA KAZI YAKE

Lefèvre hakuruhusu upinzani mkali umvunje moyo katika kazi yake ya kutafsiri Biblia. Mwaka wa 1524, baada ya kukamilisha kutafsiri Maandiko ya Kigiriki (ambayo kwa kawaida huitwa Agano Jipya), alitoa tafsiri ya Kifaransa ya Zaburi, ili watu waweze kusali “kwa kujitoa zaidi na kwa hisia nyingi.”

Mara moja, wanatheolojia wa Sorbonne walianza kuchunguza kwa makini tafsiri ya Lefèvre. Kisha, wakaagiza tafsiri yake ya maandiko ya Kigiriki ichomwe moto hadharani, na wakapiga marufuku maandishi mengine wakidai kwamba “yanaunga mkono uasi wa Luther.” Wanatheolojia walipomwita ili atetee maoni yake, Lefèvre aliamua kukaa kimya na kisha akakimbilia Strasbourg. Akiwa huko, aliendelea kutafsiri Biblia. Ingawa wengine waliona jambo alilofanya kuwa ni kukosa ujasiri, yeye aliamini kwamba hiyo ilikuwa njia bora ya kuwajibu wale ambao hawakuthamini “lulu” zenye thamani za kweli ya Biblia.—Mathayo 7:6.

Mwaka mmoja hivi baada ya Lefèvre kukimbilia Strasbourg, Mfalme Francis wa I alimchagua awe mwalimu wa mtoto wake mwenye miaka minne aliyeitwa Charles. Kazi hiyo ilimruhusu kumalizia tafsiri yake ya Biblia. Mwaka wa 1530, Biblia nzima ya Lefèvre ilichapishwa jijini Antwerp, Ubelgiji, kwa kibali cha maliki Charles wa Tano. *

MATARAJIO AMBAYO HAYAKUTIMIA

Katika maisha yake yote, Lefèvre alitumaini kwamba kanisa lingeacha mapokeo ya wanadamu na kurudia ujuzi sahihi wa Maandiko. Aliamini kabisa kwamba “kila Mkristo ana haki na wajibu wa kusoma na kujifunza Biblia kibinafsi.” Hiyo ndiyo sababu alijitahidi sana kuhakikisha kwamba kila mtu anaweza kupata Biblia. Ingawa tamaa yake ya kuona kanisa likibadilika haikutimia, matokeo ya kazi yake yanaonekana. Aliwasaidia watu wa kawaida kujua Neno la Mungu. ▪

^ fu. 8 Kitabu Fivefold Psalter kilikuwa na tafsiri tano za Zaburi kwenye safu tofauti na sanduku lenye majina ya cheo ya Mungu, kutia ndani Tetragramatoni, yaani, herufi nne za Kiebrania zinazowakilisha jina la Mungu.

^ fu. 21 Miaka mitano baadaye, mwaka 1535, mtafsiri Mfaransa Olivétan alitoa tafsiri ya Biblia iliyotegemea lugha za awali. Alitumia sana tafsiri ya Lefèvre kutafsiri Maandiko ya Kigiriki.