Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunajifunza Kumhusu Mungu Kupitia Manabii Wake

Tunajifunza Kumhusu Mungu Kupitia Manabii Wake

Nyakati za kale, Mungu aliwapatia manabii ujumbe muhimu kwa ajili ya wanadamu. Ujumbe huo unatueleza jinsi tunavyoweza kupata baraka za Mungu. Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa manabii watatu waaminifu.

ABRAHAMU

Mungu hana ubaguzi na anataka kuwabariki wanadamu wote.

Mungu alimwahidi nabii Abrahamu hivi: “Familia zote duniani hakika zitabarikiwa kupitia kwako.”​—Mwanzo 12:3.

Tunajifunza nini? Mungu anatupenda sana na anataka kubariki familia za watu wote wanaomtii—​wanaume, wanawake na watoto.

MUSA

Mungu ni mwenye rehema naye huwabariki wote wanaojitahidi kumjua.

Mwenyezi Mungu alimpa nabii Musa nguvu za kufanya miujiza mikubwa. Hata hivyo, Musa alisali hivi, “Nifundishe njia zako ili nikujue na kuendelea kuwa na kibali machoni pako.” (Kutoka 33:13) Mungu alipendezwa na ombi hilo la Musa, naye akambariki kwa kumpa ujuzi mwingi na kumsaidia kuelewa njia na sifa zake. Kwa mfano, Musa alijifunza kwamba, Muumba wetu “ni Mungu mwenye rehema na huruma.”​—Kutoka 34:6, 7.

Tunajifunza nini? Mungu anataka kuwabariki watu wote wanaojitahidi kumjua vizuri—iwe ni wanaume, wanawake au watoto. Ametuonyesha kwenye Maandiko Matakatifu jinsi ya kumwabudu na kwamba tunaweza kupata kibali na baraka zake.

YESU

Yesu alichochewa na huruma kuponya aina zote za magonjwa

Tutafurahia baraka za Mungu tukijifunza kumhusu Yesu, mambo aliyofanya na aliyofundisha.

Neno la Mungu lina habari nyingi kuhusu maisha ya Yesu na mafundisho yake. Mungu alimpa Yesu uwezo wa kufanya miujiza mingi kama vile, kuponya vipofu, viziwi na vilema. Hata aliwafufua watu waliokufa. Kwa kufanya miujiza hiyo, Yesu alionyesha baraka ambazo Mungu atawapatia wanadamu wakati ujao. Na alieleza jinsi kila mmoja wetu anavyoweza kupata baraka hizo aliposema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”​—Yohana 17:3.

Yesu alikuwa mwenye huruma, alijali hisia za wengine na alikuwa mwenye fadhili. Wanaume na wanawake, vijana kwa wazee, walikubali mwaliko huu wa Yesu: “Mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.” (Mathayo 11:29) Tofauti na wanaume wengine katika siku zake, Yesu aliwatendea wanawake kwa fadhili, heshima na staha.

Tunajifunza nini? Yesu alionyesha kwamba aliwapenda watu kikweli, na hata alituwekea mfano bora wa jinsi tunavyopaswa kutendeana.

YESU SI MUNGU

Maandiko Matakatifu yanafundisha kwamba, “kuna Mungu mmoja” ambaye ni Muumba wa ulimwengu na Yesu Kristo alikuwa mjumbe wa Mungu. (1 Wakorintho 8:6) Yesu alisema waziwazi kwamba Mungu ni mkuu kuliko yeye na kwamba Mungu ndiye aliyemtuma duniani.​—Yohana 11:41, 42; 14:28. *

^ fu. 17 Ili kujifunza mengi zaidi kumhusu Yesu Kristo, soma sehemu ya 8 na 9 ya broshua Imani ya Kweli​—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha inayopatikana kwenye tovuti ya www.pr418.com/sw.