Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Kuwa Kiziwi Hakujanizuia Kuwafundisha Wengine

Kuwa Kiziwi Hakujanizuia Kuwafundisha Wengine

Nilibatizwa mwaka 1941 nikiwa na umri wa miaka 12. Lakini mwaka 1946 ndipo nilipoelewa vizuri kweli ya Biblia. Kwa nini? Acheni niwasimulie kuhusu maisha yangu.

KATIKA miaka ya 1910, wazazi wangu walihamia Kanada kutoka Tbilisi, Georgia, na kuishi katika nyumba ndogo iliyo mashambani karibu na Pelly, Saskatchewan, magharibi mwa Kanada. Nilizaliwa mwaka 1928, nikiwa wa mwisho kati ya watoto sita. Baba alikufa miezi sita kabla sijazaliwa, na Mama alikufa nikiwa ningali mchanga. Lucy, dada yangu mkubwa, alikufa muda mfupi baada ya hapo, akiwa na umri wa miaka 17. Kwa hiyo, mjomba wangu Nick, alinitunza mimi na ndugu zangu.

Siku mmoja nilipokuwa bado mdogo, watu wa familia yetu waliniona nikivuta mkia wa farasi wetu wa kiume. Wakiogopa kwamba farasi huyo angenipiga teke, walipiga mayowe ili niache, lakini sikuchukua hatua yoyote. Nilikuwa nimetazama upande mwingine, na sikusikia wakipiga mayowe. Ni vizuri kwamba farasi huyo hakunidhuru, lakini hiyo ndiyo siku familia yetu iligundua kuwa mimi ni kiziwi.

Rafiki fulani wa familia yetu alipendekeza nisome na watoto wengine viziwi, kwa hiyo mjomba wangu Nick alinipeleka kwenye shule ya viziwi huko Saskatoon, Saskatchewan. Nilihamishiwa eneo lililo saa kadhaa mbali na familia yetu, na kwa kuwa nilikuwa na umri wa miaka mitano tu, niliogopa sana. Ningetembelea familia yetu wakati wa likizo tu na wakati wa majira ya joto. Mwishowe, nilijifunza lugha ya ishara (alama) na hivyo nilifurahia kucheza na watoto wengine.

NILIVYOJIFUNZA KWELI YA BIBLIA

Katika 1939, dada yangu mkubwa, Marion, aliolewa na Bill Danylchuck, na wakatuchukua ili kututunza mimi pamoja na dada yangu Frances. Walikuwa ndio watu wa kwanza katika familia yetu kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Wakati wa likizo ya majira ya joto, walinieleza kadiri ya uwezo wao walichokuwa wakijifunza katika Biblia. Kwa kweli, haikuwa rahisi kuzungumza nao, kwa kuwa hawakujua lugha ya ishara. Lakini ni wazi waliona kwamba ninapenda mambo ya kiroho kutoka moyoni. Nilitambua kwamba kulikuwa na uhusiano kati ya walichofanya na kile ambacho Biblia inasema, kwa hiyo niliandamana nao walipoenda kuhubiri. Muda mfupi baadaye, nilitaka kubatizwa, na Septemba 5, 1941, Bill alinibatiza kwenye tangi la chuma lililokuwa na maji yaliyotolewa kwenye kisima. Maji hayo yalikuwa baridi ajabu!

Nikiwa na kikundi cha viziwi katika kusanyiko huko Cleveland, Ohio, mwaka 1946

Mnamo 1946 niliporudi nyumbani wakati wa majira ya joto, tulihudhuria kusanyiko huko Cleveland, Ohio, Marekani. Siku ya kwanza ya kusanyiko hilo, dada zangu walipokezana kuandika mambo makuu ya kusanyiko ili kunisaidia nielewe programu. Lakini siku ya pili, nilifurahi sana kugundua kuwa kulikuwa na kikundi cha viziwi pamoja na mkalimani wa lugha ya ishara. Hatimaye, ningeweza kufurahia programu na lilikuwa jambo lenye kupendeza sana kuelewa vizuri kweli ya Biblia!

NAANZA KUFUNDISHA KWELI

Wakati huo, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimetoka tu kwisha na watu wengi walikuwa na roho ya utaifa. Nilirudi kutoka kusanyikoni nikiwa nimeazimia kuchukua msimamo thabiti kuhusu imani yangu shuleni. Hivyo, nikaacha kusalimu bendera na kuimba wimbo wa taifa. Pia, niliacha kushiriki katika sherehe za sikukuu na kuhudhuria ibada za kanisa zilizokuwa za lazima shuleni. Wenye mamlaka shuleni hawakufurahi na walijaribu kunitisha na kusema mambo ya uwongo ili kunifanya nibadili uamuzi wangu. Mambo hayo yote yaliwashangaza sana wanafunzi wenzangu, lakini yalinipa fursa ya kutoa ushahidi. Mwishowe wanafunzi wenzangu Larry Androsoff, Norman Dittrick, na Emil Schneider walikubali kweli, na wanamtumikia Yehova kwa ushikamanifu hadi leo.

Sikuzote mimi huhakikisha kuwa ninawahubiria viziwi ninapotembelea majiji mengine. Kwa mfano, huko Montreal, nilimhubiria Eddie Tager, kijana aliyekuwa amejiunga na kikundi fulani cha viziwi kilichodharauliwa. Hadi alipokufa mwaka jana, alikuwa akishirikiana na kutaniko la lugha ya ishara la Laval, Quebec. Pia, nilikutana na kijana aliyeitwa Juan Ardanez ambaye, kama Waberoya, alifanya utafiti kwa bidii ili kuhakikisha ukweli wa ujumbe wa Biblia. (Mdo. 17:10, 11) Yeye pia alijifunza kweli na alitumikia kwa uaminifu akiwa mzee wa kutaniko jijini Ottawa, Ontario, hadi alipokufa.

Nikihubiri barabarani mapema katika miaka ya 1950

Mwaka 1950, nilihamia Vancouver. Ingawa napenda kuwahubiria viziwi, sitasahau kamwe pindi fulani nilipomhubiria barabarani mwanamke anayeitwa Chris Spicer, ambaye si kiziwi. Alikubali maandikisho ya gazeti na akataka nikutane na mume wake, Gary. Kwa hiyo, niliwatembelea nyumbani kwao, na tukawa na mazungumzo marefu tukiwasiliana kwa kuandika. Hatukukutana tena hadi miaka michache baadaye, ambapo nilishangaa kwamba walinitambua katikati ya umati kwenye kusanyiko lililofanywa Toronto, Ontario. Gary angebatizwa siku hiyo. Jambo hilo lililoonwa lenye kupendeza lilinikumbusha umuhimu wa kuendelea kuhubiri kwa kuwa hatujui ni wapi au lini kweli itakua.

Baadaye, nilirudi Saskatoon. Nikiwa huko nilikutana na mama fulani aliyeniomba nijifunze Biblia na binti zake viziwi, Jean na Joan Rothenberger, ambao walikuwa wanafunzi katika shule ileile niliyosomea. Baada ya muda mfupi, wasichana hao waliwaeleza wanafunzi wenzao kile walichokuwa wakijifunza. Mwishowe, wanafunzi watano katika darasa lao wakawa Mashahidi wa Yehova. Mmoja wao alikuwa Eunice Colin. Nilikuwa nimekutana na Eunice kwa mara ya kwanza katika shule hiyo ya viziwi nilipokuwa karibu kumaliza shule. Wakati huo, alinipa peremende na kuniomba tuwe marafiki. Baadaye, alikuwa mtu muhimu sana maishani mwangu, yaani, mke wangu!

Mimi na Eunice mwaka 1960 na mwaka 1989

Mama ya Eunice alipogundua kwamba alikuwa akijifunza Biblia, alimwambia mkuu wa shule amkataze. Mkuu huyo hata alichukua machapisho aliyotumia kujifunza. Hata hivyo, Eunice alikuwa ameazimia kumtanguliza Yehova. Alipotaka kubatizwa, wazazi wake walimwambia, “Ukiwa Shahidi wa Yehova, utaondoka nyumbani!” Alipokuwa na umri wa miaka 17, Eunice aliondoka nyumbani, na familia moja ya Mashahidi ikamchukua na kuishi naye. Aliendelea kujifunza na baadaye akabatizwa. Tulipofunga ndoa mwaka 1960, wazazi wake hawakuhudhuria arusi yetu. Lakini kadiri miaka ilivyopita walianza kutuheshimu kwa sababu ya imani yetu na jinsi tulivyowalea watoto wetu.

YEHOVA AMENITUNZA

Mwanangu Nicholas na mke wake, Deborah, wanatumikia katika Betheli ya London

Ingawa sisi ni wazazi viziwi, tuliwalea wavulana saba wenye uwezo wa kusikia. Tulipata changamoto mbalimbali, lakini tulihakikisha kwamba walijifunza lugha ya ishara ili tuweze kuwasiliana nao vizuri na kuwafundisha kweli. Ndugu na dada kutanikoni walitusaidia sana. Kwa mfano, mzazi fulani aliandika kwenye karatasi na kutujulisha kwamba mmoja wa wavulana wetu alikuwa akitumia maneno mabaya kwenye Jumba la Ufalme. Tulishughulikia jambo hilo papo hapo. Wana wangu wanne, James, Jerry, Nicholas, na Steven, wanamtumikia Yehova kwa uaminifu pamoja na wake na familia zao. Wote wanne wanatumikia wakiwa wazee kutanikoni. Kwa kuongezea, Nicholas na mke wake, Deborah, wanasaidia kutafsiri lugha ya ishara kwenye ofisi ya tawi ya Uingereza ilhali Steven na mke wake, Shannan, wanasaidia kutafsiri lugha ya ishara kwenye ofisi ya tawi ya Marekani.

Wanangu James, Jerry, na Steven wakiwa na wake zao wanaunga mkono kazi ya kuhubiri katika lugha ya ishara kwa njia mbalimbali

Mwezi mmoja kabla ya kuadhimisha miaka 40 ya ndoa yetu, Eunice alikufa kwa sababu ya kansa. Alikuwa jasiri sana katika pindi hiyo ngumu. Imani yake katika ufufuo ilimwimarisha. Ninatamani sana siku nitakayomwona tena.

Faye na James; Jerry na Evelyn; Shannan na Steven

Katika Februari 2012, nilianguka na kuvunjika nyonga, na ikawa wazi kwamba ningehitaji msaada. Kwa hiyo, nilianza kuishi na mmoja wa wanangu na mke wake. Sasa tunashirikiana na kutaniko la Lugha ya Ishara la Calgary, ambako ninaendelea kutumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Wazia kwamba hii ndiyo mara ya kwanza nimetumikia katika kutaniko la lugha ya ishara! Niliwezaje kuwa na hali nzuri ya kiroho licha ya kuwa katika kutaniko la Kiingereza tangu mwaka 1946? Yehova ametimiza ahadi yake ya kuwatunza watoto wasio na baba. (Zab. 10:14) Ninashukuru kwa jitihada za wote waliokuwa tayari kuniandikia mambo makuu, kujifunza lugha ya ishara, na kunitafsiria kadiri ya uwezo wao.

Nilipohudhuria shule ya mapainia katika Lugha ya Ishara ya Marekani nikiwa na umri wa miaka 79

Kwa kweli, kuna pindi nilizohisi kuvunjika moyo na kukata tamaa kwa sababu sikuelewa kile kilichokuwa kikisemwa au kwa sababu ilionekana kana kwamba mahitaji ya viziwi hayakueleweka. Hata hivyo, katika pindi hizo nilifikiria maneno haya ambayo Petro alimwambia Yesu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:66-68) Kama ndugu na dada wengi viziwi walioishi wakati wangu, nimejifunza kuwa na subira. Nimejifunza kumsubiri Yehova na tengenezo lake, na nimenufaika sana kwa kufanya hivyo! Sasa nina chakula kingi cha kiroho katika lugha yangu, na ninafurahia ushirika kwenye mikutano na makusanyiko ya Lugha ya Ishara ya Marekani. Kwa hakika, nimekuwa na maisha yenye furaha na yenye kuthawabisha ninapomtumikia Yehova, Mungu wetu mkuu.