Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, ni kweli kwamba zamani mtu angeweza kupanda magugu katika shamba la mtu mwingine?

Nakala hii ya mwaka wa 1468 ya kijitabu (Digest) cha Maliki Justinian ni moja kati ya rekodi nyingi zenye habari kuhusu masuala ya zamani ya kisheria

KATIKA andiko la Mathayo 13:24-26, Yesu ananukuliwa akisema: “Ufalme wa mbinguni umekuwa kama mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. Watu wakiwa wamelala usingizi, adui yake alikuja na kupanda magugu katikati ya ngano, naye akaondoka. Wakati jani lilipoota na kuzaa matunda, magugu yalionekana pia.” Waandishi mbalimbali wanatilia shaka ikiwa mfano huu ni halisi. Hata hivyo, maandishi ya kale ya Roma yaliyohusiana na sheria, yanaonyesha kwamba jambo hilo lingeweza kutukia.

Kamusi moja ya Biblia inasema hivi: “Chini ya sheria ya Roma . . . ilikuwa kosa kupanda magugu kwenye shamba la mtu kwa kusudi la kulipiza kisasi. Kuwekwa kwa sheria hiyo kunaonyesha kwamba jambo hilo lilikuwa la kawaida.” Msomi wa sheria Alastair Kerr anaeleza kwamba katika mwaka wa 533 W.K., Maliki Mroma Justinian aliandika kijitabu kilichokuwa na sheria za Roma kwa ufupi na maelezo machache ya wanasheria walioishi kati ya mwaka wa 100 na 250 W.K. Kulingana na kijitabu hicho (Digest, 9.2.27.14), mwanasheria Ulpian alitaja kesi iliyoshughulikiwa na kiongozi wa Roma aliyeitwa Celsus, aliyetawala katika karne ya pili. Magugu yalikuwa yamepandwa katika shamba la mtu fulani na yakaharibu mimea yake. Kijitabu hicho kilizungumzia hatua za kisheria ambazo mwenye shamba au mtu aliyekodi shamba hilo, angeweza kuchukua ili alipwe kutokana na hasara aliyopata.

Ikiwa njama kama hiyo ingeweza kutukia kwenye Milki ya Roma katika nyakati za kale, basi ni wazi kwamba hali ambayo Yesu alieleza ilikuwa halisi.

Katika karne ya kwanza, serikali ya Roma iliwapa uhuru kadiri gani Wayahudi waliokuwa Yudea?

KATIKA karne ya kwanza, Wayahudi walitawaliwa na Waroma waliowakilishwa na gavana mwenye mamlaka juu ya vikosi kadhaa vya wanajeshi. Jukumu lake kuu lilikuwa kukusanya kodi kwa ajili ya serikali ya Roma na kudumisha amani na utulivu. Waroma walihakikisha kwamba wanazuia shughuli zote zilizofanywa kinyume cha sheria na kumpeleka mahakamani mtu yeyote aliyesababisha vurugu. Ingawa hivyo, Waroma waliwapa viongozi Wayahudi mamlaka ya kusimamia shughuli za kila siku katika mikoa yao.

Kikao cha Sanhedrini ya Kiyahudi kikiendelea

Sanhedrini ilikuwa mahakama kuu ya Wayahudi na ilikuwa baraza lililoongoza mambo ya kisheria. Kulikuwa na mahakama nyingine ndogo katika Yudea. Yaelekea kesi ndogo-ndogo na kesi za uhalifu zilishughulikiwa na mahakama hizo bila kuwahusisha watawala wa Roma. Hata hivyo, waliwekewa kizuizi kimoja kilichohusiana na hukumu ya kifo kwa wahalifu; Waroma pekee ndio waliokuwa na haki ya kutoa hukumu hiyo. Kisa kimoja kinachojulikana sana ambapo sheria hiyo ilikiukwa ni wakati washiriki wa Sanhedrini walimhukumu Stefano na kumpiga mawe.—Mdo. 6:8-15; 7:54-60.

Kwa hiyo, Sanhedrini ilikuwa na mamlaka makubwa. Hata hivyo, msomi Emil Schürer anasema hivi: “Waroma wangechukua hatua wakati wowote bila kuwahusisha Wayahudi, hasa ikiwa wangeshuku kwamba kuna uvunjaji wa sheria katika mambo ya kisiasa.” Mfano mmoja wa kisa kama hicho ni wakati kamanda wa kijeshi Klaudio Lisia, alipomfunga gerezani mtume Paulo, ambaye alikuwa raia wa Roma.—Mdo. 23:26-30.