Hamia kwenye habari

Walijitoa kwa Hiari​—Nchini Bulgaria

Walijitoa kwa Hiari​—Nchini Bulgaria

 Mashahidi wa Yehova nchini Bulgaria wana bidii katika kazi ya kuwafundisha watu kweli kuhusu Mungu na Neno lake, Biblia. Ili kuwasaidia, mamia ya Mashahidi kutoka nchi nyingine wamehamia Bulgaria tangu mwaka wa 2000. Kuhamia nchi nyingine ili kuhubiri kunatokeza changamoto gani? Kwa nini jitihada hizo si za bure? Yafuatayo ni baadhi ya maoni ya waliohamia nchini Bulgaria.

Kujiwekea Mradi

 Darren aliyeishi Uingereza anasema hivi: “Sikuzote tulikuwa na mradi wa kutumikia katika nchi nyingine iliyo na uhitaji mkubwa zaidi. Baada ya kufunga ndoa na Dawn, tulihamia jiji la London ili kuwafundisha Biblia watu wanaozungumza Kirusi. Mara kadhaa tulifanya mipango ya kuhamia nchi nyingine, lakini kwa sababu mbalimbali tulishindwa kuhama. Tulianza kufikiri hatungeweza kutimiza mradi wetu, lakini rafiki yetu alitusaidia kuona kwamba hali zetu zilikuwa zimebadilika na hivyo tungeweza kuutimiza.” Darren na Dawn walianza kutafuta nchi ambayo ina uhitaji mkubwa wa walimu wa Biblia na ambayo wangeweza kuhamia kupatana na hali zao. Walihamia Bulgaria mwaka wa 2011.

Darren na Dawn

 Shangwe ya wale waliohamia nchi nyingine iliwachochea wengine ambao mwanzoni hawakuwa na mradi huo. Giada aliyeiishi Italia na mume wake, Luca, alisema hivi: “Nilikutana na Mashahidi wenye bidii waliokuwa wakitumikia kwa shangwe Amerika Kusini na Afrika. Niliguswa moyo sana na shangwe yao na mambo yaliyoonwa waliyosimulia. Jambo hilo lilinisaidia kurekebisha malengo yangu ya kiroho.”

Luca na Giada

 Tomasz na Veronika waliondoka Jamhuri ya Cheki mwaka wa 2015 na kuhamia Bulgaria, wakiwa na watoto wao wawili Klara na Mathias. Ni nini kilichowachochea kuhama? Tomasz anasema hivi: “Tulifikiria sana mifano ya wengine waliokuwa wamehamia nchi za kigeni, kutia ndani watu wetu wa ukoo, na tukatafakari baadhi ya mambo waliyofurahia. Shangwe yao ilitugusa moyo sana, na tulizungumzia hilo kama familia.” Familia hii yenye furaha sasa wanahubiri katika eneo lao jipya katika jiji la Montana, nchini Bulgaria.

Klara, Tomasz, Veronika, na Mathias

 Linda ni Shahidi mwingine aliyehamia Bulgaria. Anasema hivi: “Miaka mingi iliyopita nilitembelea Ekuado na nikakutana na baadhi ya ndugu na dada waliohamia huko ili kuhubiri. Jambo hilo lilinifanya nione kwamba huenda siku moja ninaweza pia kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa.” Petteri na Nadja, wenzi wa ndoa kutoka Finland, walitafakari pia kuhusu mifano ya watu wengine. Wanasema hivi: “Katika kutaniko letu la nyumbani, tulikuwa na wahubiri wenye uzoefu waliohamia maeneo mengine ili kuwasaidia watu kiroho. Mara zote walizungumza kwa shauku nyingi sana kuhusu miaka waliyotumia katika utumishi huo. Walisema kwamba hiyo ilikuwa miaka bora zaidi maishani mwao.”

Linda

Nadja na Petteri

Kupanga Mambo Mapema

 Ni jambo la muhimu kwa wale wanaotaka kutumikia nchi ya kigeni kupanga mambo mapema. (Luka 14:28-30) Nele kutoka Ubelgiji anasema hivi: “Nilipoanza kufikiria kwa uzito kuhusu kutumikia katika nchi nyingine, nilisali na kuanza kutafuta makala katika machapisho yetu zinazozungumzia jambo hilo. Nilizisoma na kuona ni mambo gani ninayopaswa kufanyia kazi.”

Nele (kulia)

 Kristian na Irmina kutoka Poland, wameishi Bulgaria kwa zaidi ya miaka tisa. Walinufaika sana kushirikiana na kikundi cha Kibulgaria kilichoko Poland kabla ya kuhama. Kikundi hicho kiliwatia moyo na kuwasaidia kujifunza Kibulgaria. Kristian na Irmina wanasema: “Hatimaye tuligundua jinsi inavyopendeza kujitolea na kujionea jinsi Yehova Mungu anavyoweza kukupatia mahitaji yako. Unapomwambia Yehova kwa hiari, ‘Mimi hapa! Nitume mimi!’ unaweza kutimiza mambo ambayo hukufikiria kwamba ungetimiza.”—Isaya 6:8.

Kristian na Irmina

 Ili kujitayarisha na kuweka pesa akiba, Reto na Cornelia, wenzi wa ndoa kutoka Uswisi, waliamua kuishi maisha rahisi. Wanasema hivi: “Mwaka mmoja kabla ya kuhama, tulitembelea Bulgaria kwa juma moja ili kujifunza mengi zaidi kuhusu nchi hiyo. Tukiwa huko tulizungumza na wamishonari wenye uzoefu ambao walitusaidia sana.” Reto na Cornelia walitumia vizuri mapendekezo waliyopewa na sasa wameishi Bulgaria kwa zaidi ya miaka 20.

Cornelia na Reto, pamoja na wana wao Luca na Yannik

Kukabiliana na Changamoto

 Wale wanaohamia nchi ya kigeni wanahitaji kuzoea hali na changamoto mpya. (Matendo 16:9, 10; 1 Wakorintho 9:19-23) Changamoto kubwa zaidi kwa wengi ni kujifunza lugha mpya. Luca aliyetajwa mwanzoni alisema hivi: “Tulifurahia sana kutoa maelezo kutoka moyoni katika mikutano yetu ya Kikristo. Hata hivyo, kwa kipindi fulani haikuwa rahisi kwangu na mke wangu kutayarisha hata jibu moja rahisi katika Kibulgaria! Ni kana kwamba tulikuwa watoto tena. Kwa kweli, watoto katika kutaniko walitoa maelezo bora zaidi ya yetu.”

 Ravil kutoka Ujerumani, anasema hivi: “Kujifunza lugha kulinichosha sana. Hata hivyo nilijiambia, ‘Usijiheshimu kupita kiasi, na cheka unapokosea.’ Niliona changamoto hizo kuwa si matatizo bali sehemu ya utumishi wangu mtakatifu kwa Yehova.”

Ravil na Lilly

 Linda aliyetajwa mwanzoni, alisema hivi: “Si rahisi kwangu kujifunza lugha. Si rahisi kujifunza Kibulgaria, na mara nyingi nilifikiria kuacha kujifunza. Unahisi upweke unaposhindwa kuongea na watu na usipoelewa mambo wanayosema. Ili kuimarisha hali yangu ya kiroho, nilijifunza kila kitu katika Kiswedi. Hatimaye, kwa msaada wa ndugu na dada zangu wapendwa, nilifaulu kujifunza Kibulgaria.”

 Changamoto nyingine ni kutamani kurudi nyumbani. Wale wanaohama huacha watu wao wa ukoo na marafiki nyumbani. Eva aliyehamia Bulgaria pamoja na mume wake, Yannis anasema hivi: “Mwanzoni nilihisi upweke. Ili kukabiliana na hali hiyo, tuliwasiliana kwa ukawaida na marafiki na watu wa familia, na tulipata marafiki wapya hapa.”

Yannis na Eva

 Kuna changamoto nyingine. Robert na Liana, waliohamia kutoka Uswisi wanasema hivi: “Lugha na utamaduni mpya ulikuwa changamoto kubwa sana kwetu, na hatukuwa tumejitayarisha kukabiliana na majira ya baridi kali sana ya hapa. Hata hivyo, kudumisha mtazamo mzuri na furaha kumewasaidia wenzi hao kutumikia kwa uaminifu nchini Bulgaria kwa miaka 14 sasa.

Robert na Liana

Baraka

 Lilly anapendekeza kuhubiri katika eneo lenye uhitaji mkubwa. Alisema hivi: “Nimekuja kumjua Yehova katika njia ambayo huenda nisingeweza ikiwa ningekuwa nchini kwetu. Nimekuwa na mengi ya kufanya katika kuwasaidia wengine, na hilo limenisaidia kukua kiroho na linanipatia shangwe na uradhi.” Mume wake Ravil, anakubaliana naye. Anasema hivi: “Haya ndiyo maisha bora, nafasi ya pekee ya kuwafahamu Wakristo wenye bidii kutoka nchi mbalimbali walio na uzoefu mwingi wa kufundisha kweli za Biblia. Nimejifunza mengi kutoka kwao.”

 Wengi wanaoweza na walio na roho ya kujitolea kuhamia maeneo mengine wamesaidia sana katika kuhubiriwa kwa “habari njema ya Ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Kwa sababu ya roho yao ya kujitolea, wote waliohamia Bulgaria wamejionea jinsi Yehova alivyotimiza tamaa za mioyo yao na kufanikisha mipango yao yote.—Zaburi 20:1-4.