Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Jinsi ya Kupinga Vishawishi

Jinsi ya Kupinga Vishawishi

KIKWAZO

“Wakati mwingine wasichana huniomba namba ya simu na kutaka tuwe wapenzi. Mimi hukataa na kuondoka. Lakini akilini, mimi huendelea kujiuliza, ‘Ingekuwaje kama ningempa namba yangu?’ Kwa kweli, baadhi ya wasichana hao ni warembo sana. Ni rahisi kujiambia, ‘Afadhali ningekubali.’”—Carlos, * 16.

Je, wewe hukabiliana na vishawishi kama Carlos? Ikiwa ndivyo, unaweza kushinda vita hivyo.

UNACHOPASWA KUJUA

Ukikubali kushawishiwa, utaumia

Mtu yeyote anaweza kushawishiwa—hata watu wazima. Kuna vishawishi vya aina mbalimbali. Mtume Paulo hakuwa kijana alipoandika: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu . . . , lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi.” (Waroma 7:22, 23) Licha ya mkazo huo, Paulo hakushawishika, nawe pia unaweza kubaki imara! Usikubali kuwa mtumwa wa tamaa zako. (1 Wakorintho 9:27) Kujifunza kushinda vishawishi unapokuwa kijana kutakusaidia uepuke mahangaiko sasa, na utakapokuwa mtu mzima utahitaji sana ustadi wa kupinga vishawishi.

Vyombo vya habari huchochea vishawishi. Biblia inataja “tamaa zinazotukia ujanani,” ambazo zina nguvu kwelikweli. (2 Timotheo 2:22) Lakini sinema, televisheni, muziki, na vitabu kwa ajili ya vijana mara nyingi huchochea tamaa hizo kwa kuonyesha kwamba ni jambo la kawaida kukubali kushawishiwa. Kwa mfano, watu wawili katika sinema ‘wanapopendana,’ ni kawaida kwao kufanya ngono. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba katika maisha halisi wanaume na wanawake wana uwezo wa kuendelea “kujiepusha na tamaa za kimwili.” (1 Petro 2:11) Hilo linamaanisha kwamba unaweza kupinga vishawishi. Inawezekanaje?

 UNACHOWEZA KUFANYA

Tambua udhaifu wako. Usipoziba ufa, utajenga ukuta. Vivyo hivyo, azimio lako la kutenda mema huenda likavunjwa na udhaifu wako. Ni mambo gani ambayo unahitaji kuzingatia?—Kanuni ya Biblia: Yakobo 1:14.

Wazia vishawishi utakavyokabili. Wazia hali ambazo huenda zikaleta vishawishi. Jitayarishe kiakili jinsi utakavyopinga vishawishi hivyo vitakapotokea.—Kanuni ya Biblia: Methali 22:3.

Uwe na msimamo thabiti. Biblia inasema kwamba Yosefu aliposhawishiwa afanye ngono alisema: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwanzo 39:9) Neno “ninawezaje” linaonyesha kwamba Yosefu alikuwa na msimamo thabiti kuhusu mema na mabaya. Je, wewe una msimamo kama huo?

Tafuta marafiki watakaokusaidia. Unaweza kuepuka vishawishi vingi ikiwa utachagua marafiki ambao wana msimamo kama wako kuhusu maadili. Biblia inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—Methali 13:20.

Epuka hali zinazochochea vishawishi. Kwa mfano:

  • Usijiruhusu kuwa peke yako na mtu wa jinsia tofauti.

  • Epuka kutumia Intaneti wakati au mahali ambapo utashawishiwa kutazama ponografia.

  • Epuka watu ambao tabia na maneno yao yanafanya uovu uonekane kuwa jambo zuri.

Unaweza kujiwekea kanuni gani ili uepuke vishawishi?—Kanuni ya Biblia: 2 Timotheo 2:22.

Mwombe Mungu akusaidie. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Endeleeni . . . kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.” (Mathayo 26:41) Ukweli ni kwamba Yehova Mungu anataka ushinde vishawishi, na anaweza kukusaidia kufanya hivyo. Biblia inasema: “Hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

^ fu. 4 Jina limebadilishwa.