Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Sala

Sala

Je, kweli kuna yeyote anayesikiliza sala zetu?

“Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—Zaburi 65:2.

WATU HUSEMA NINI?

 Kuna watu wanaofikiri kwamba mtu anaposali sala yake haiendi popote. Watu wanaoteseka huenda wakashuku ikiwa kweli sala zao zinasikilizwa.

BIBLIA INASEMA NINI?

 “Macho ya Yehova [Mungu] yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao; bali uso wa Yehova uko dhidi ya wale wanaotenda mambo mabaya,” inasema Biblia. (1 Petro 3:12) Ni wazi kwamba Mungu husikiliza sala. Hata hivyo, yeye huwasikiliza wale wanaomtii. Kuhusu utayari wa Mungu kusikiliza sala zetu, andiko lingine linasema: “Huu ndio uhakika ambao tunao kwake, kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Hivyo, mtu anayesali anapaswa kuomba mambo yanayopatana na mapenzi ya Mungu.

 Tunapaswa kusali jinsi gani?

“Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena.”—Mathayo 6:7.

WATU HUSEMA NINI?

 Wafuasi wa dini mbalimbali kama vile Wabudha, Wakatoliki, Wahindu, na Waislamu wamefundishwa kusali wakitumia rozari, mala, au tasbihi ili kukariri na kuhesabu sala.

BIBLIA INASEMA NINI?

 Mtu anapaswa kusali kutoka moyoni na kwa unyoofu, sala hazipaswi kukaririwa wala kurudiwa-rudiwa. Maandiko yanatuhimiza hivi: “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi. Kwa hiyo, msijifanye kama wao, kwa maana Mungu Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.”—Mathayo 6:7, 8.

KWA NINI JAMBO HILI NI MUHIMU?

 Sala ikitolewa kwa njia ambayo haimpendezi Mungu, mtu anayesali anaweza kupoteza muda wake na hata kumkasirisha Mungu. Biblia inaonya kwamba sala za watu wanaokataa kumtii Mungu ni “chukizo” kwake.—Methali 28:9.

Tunapaswa kusali kwa nani?

“Mtafuteni Yehova [Mungu], wakati anapoweza kupatikana. Mwiteni akiwa bado yupo karibu.” —Isaya 55:6.

WATU HUSEMA NINI?

 Watu fulani husali kwa Maria au viumbe wengine kama vile malaika na watu wanaoonwa kuwa “watakatifu.” Wanatia ndani “Mtakatifu” Antoni wa Padua anayeonwa kuwa mlezi wa “mahitaji ya kiroho na ya kimwili,” na “Mtakatifu” Yuda, anayeonwa kuwa mlezi wa “hali ngumu.” Watu wengi husali kwa “watakatifu” kama hao na kwa malaika wakitazamia kwamba watawaombea kwa Mungu.

BIBLIA INASEMA NINI?

 Waabudu wa kweli wanapaswa kusali kwa “Baba yetu [wa] mbinguni.” (Mathayo 6:9) Biblia inatuhimiza hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”Wafilipi 4:6.