Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | FENG-LING YANG

Mwanabiolojia Anaeleza Kwa Nini Anamwamini Mungu

Mwanabiolojia Anaeleza Kwa Nini Anamwamini Mungu

Feng-Ling Yang ni msaidizi wa utafiti katika chuo fulani cha utafiti huko Taipei, Taiwan. Utafiti wake umechapishwa katika majarida ya kisayansi. Zamani aliamini nadharia ya mageuzi. Hata hivyo, alibadili maoni yake. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji kuhusu taaluma yake na imani yake.

 

Tueleze kuhusu malezi yako.

Wazazi wangu walikuwa maskini sana, na mama yangu hakujua kusoma. Tulifuga nguruwe na kukuza mboga za majani katika eneo ambalo hukumbwa na mafuriko karibu na mji wa Taipei. Wazazi wangu walinifundisha umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii, na pia walinifundisha kuwasaidia watu.

Je, familia yenu ilishirikiana na dini yoyote?

Familia yetu ilifuata dini ya Utao. Tulitoa dhabihu, lakini hatukujua lolote kumhusu Mungu. Mara nyingi nilijiuliza: ‘Kwa nini watu huteseka? Kwa nini watu ni wenye ubinafsi?’ Nilisoma vitabu kuhusu Utao, Ubudha na historia ya nchi za Mashariki na Magharibi. Hata nilienda makanisa kadhaa. Lakini sikupata majibu ya maswali yangu.

Kwa nini ulichagua somo la sayansi?

Nilipenda hesabu na nilivutiwa na jinsi ambavyo sheria za fizikia na kemia huongoza mpangilio wa vitu. Kila kitu, kuanzia ulimwengu wetu mkubwa hadi bakteria ndogo sana zina mpangilio unaoongozwa na sheria. Nilitaka kuelewa sheria hizo.

Kwa nini uliamini nadharia ya mageuzi?

Hivyo ndivyo nilivyofundishwa. Tangu nilipokuwa shule ya sekondari hadi chuo kikuu, nilifundishwa kuhusu mageuzi. Pia, kwa kuwa nilifanya utafiti wa viumbe hai, nilitazamiwa niamini nadharia ya mageuzi.

Kwa kuwa nilifanya utafiti wa viumbe hai, nilitazamiwa niamini nadharia ya mageuzi

Ni nini kilichokufanya uanze kusoma Biblia?

Mwaka wa 1996, nilienda Ujerumani kusomea shahada ya tatu. Mwaka uliofuata, nilikutana na mwanamke anayeitwa Simone. Alikuwa Shahidi wa Yehova, na alijibu maswali yangu kwa kutumia Biblia. Aliponiambia kwamba Biblia inaeleza kusudi la uhai, nilitaka kujua zaidi. Nilianza kuamka saa kumi na nusu kila alfajiri ili kusoma Biblia kwa saa moja. Kisha ningeenda kutembea ili nitafakari niliyosoma. Mwaka uliofuata, niliisoma Biblia nzima. Nilivutiwa sana na usahihi wa unabii wake. Hatua kwa hatua, nilisadikishwa kwamba Biblia imetoka kwa Mungu.

Ulikuwa na maoni gani kuhusu chanzo cha uhai?

Nilipoanza kufikiria jambo hilo kwa uzito mwishoni mwa miaka ya 1990, wanabiolojia wa molekuli walikuwa wameanza kutambua kwamba utendaji unaoendeleza uhai ni tata sana kuliko wanasayansi walivyodhani awali. Bila shaka, tayari walikuwa wanajua kwamba hakuna molekuli zilizo tata kuliko protini zilizo ndani ya chembe hai. Lakini sasa walikuwa wakigundua jinsi ambavyo vikundi vya protini hufanyiza mifumo tata ya molekuli yenye sehemu zinazosonga. Mfumo mmoja wa molekuli unaweza kuwa na protini zaidi ya 50. Hata chembe sahili inahitaji mifumo mbalimbali—kwa mfano, inahitaji mfumo wa kutokeza nishati, kunakili habari, na kudhibiti kinachoingia au kutoka kwenye chembe.

Ulifikia mkataa gani?

Nilijiuliza, ‘Mifumo hiyo ya protini inawezaje kufanya kazi kwa ustadi hivyo?’ Wakati huo, utata wa utendaji wa chembe ulifanya wanasayansi kadhaa wajiulize swali hilohilo. Profesa wa biokemia huko Marekani aliandika kitabu kilichosema kwamba utendaji wa molekuli katika chembe hai ni tata sana hivi kwamba haiwezekani uwe ulijitokeza wenyewe. Nilikubaliana naye. Niliona kwamba lazima uhai uwe uliumbwa.

Nilijiuliza, ‘Mifumo hiyo ya protini inawezaje kufanya kazi kwa ustadi hivyo?’

Kwa nini uliamua kuwa Shahidi wa Yehova?

Nilipendezwa na jinsi ambavyo Simone alijitahidi kusafiri umbali wa kilomita 56 hivi kila juma kuja kunifundisha Biblia ingawa alikuwa na matatizo ya afya. Nilijifunza kwamba wakati wa utawala wa Nazi huko Ujerumani, Mashahidi fulani walifungwa katika kambi za mateso kwa sababu ya kukataa kujihusisha katika siasa. Ujasiri wao ulinigusa sana moyo. Upendo wa Mashahidi kwa Mungu ulinichochea kuwaiga.

Je, kuamini kwamba kuna Mungu kumekufaidi?

Wafanyakazi wenzangu wanasema kwamba sasa nina furaha zaidi. Zamani nilijidharau kwa sababu nililelewa katika familia maskini, kwa hiyo sikumwambia mtu yeyote kuhusu malezi yangu wala kuhusu wazazi wangu. Lakini Biblia imenifundisha kwamba Mungu haangalii kama mtu ni maskini au tajiri. Huenda hata Yesu alilelewa katika familia iliyokuwa maskini kama yetu. Sasa mimi huwatunza wazazi wangu na ninafurahia kuwatambulisha kwa marafiki wangu.