Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAHOJIANO | FAN YU

Mtaalamu wa Programu za Kompyuta Anaeleza Kwa Nini Anamwamini Mungu

Mtaalamu wa Programu za Kompyuta Anaeleza Kwa Nini Anamwamini Mungu

DAKT. Fan Yu alianza kazi akiwa mtafiti wa hesabu katika chuo cha China Institute of Atomic Energy, kilicho karibu na mji wa Beijing. Wakati huo, hakuwa anamwamini Mungu na aliamini nadharia ya mageuzi. Lakini leo, Dakt. Yu anaamini kwamba uhai ulibuniwa na kuumbwa na Mungu. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji kuhusu imani yake.

Tafadhali tueleze kuhusu maisha yako ya awali.

Nilizaliwa mwaka wa 1959 katika Mji wa Fuzhou, Wilaya ya Jiangxi, nchini China. Nikiwa na umri wa miaka nane, nchi ilikuwa inakabili madhara yaliyosababishwa na mapinduzi yanayojulikana kama Mapinduzi ya Kitamaduni. Baba yangu ambaye alikuwa mhandisi wa ujenzi, alitumwa kwenda kujenga reli katika eneo la mbali. Kwa miaka mingi, alitutembelea mara moja tu kwa mwaka. Niliishi na mama yangu ambaye alikuwa mwalimu wa shule ya msingi. Tuliishi katika shule aliyokuwa akifundisha. Mwaka wa 1970, tulihamia Liufang, kijiji kilichokuwa maskini, katika Mkoa wa Linchuan. Kulikuwa na shida ya chakula katika kijiji hicho.

Familia yenu iliamini nini?

Baba yangu hakupendezwa na dini wala siasa. Mama alikuwa Mbudha. Shuleni nilifundishwa kwamba uhai ulijitokeza wenyewe, na niliamini kile ambacho walimu walinifundisha.

Kwa nini ulipenda somo la hesabu?

Nilipenda somo la hesabu kwa sababu linahusisha kufikiri ili kujua usahihi wa mambo. Nilienda chuo kikuu muda mfupi baada ya kifo cha kiongozi wa mapinduzi, Mao Tse-tung, katika mwaka wa 1976. Nilichagua kusomea somo la hesabu. Baada ya kupokea shahada ya pili, niliajiriwa kufanya utafiti wa hesabu ili kuunda vifaa vya kutokeza nishati ya atomu.

Mwanzoni ulikuwa na maoni gani kuhusu Biblia?

Katika mwaka wa 1987, nilihamia nchini Marekani ili nipate shahada ya juu katika Chuo cha Texas A&M. Nilijua kwamba watu wengi nchini Marekani wanaamini Mungu, nao husoma Biblia. Pia, nilisikia kwamba Biblia ina mashauri mengi ya hekima, hivyo niliamua kuisoma.

Mafundisho ya Biblia yalionekana kuwa yenye faida. Hata hivyo, sikuelewa sehemu fulani za Biblia na kwa hiyo nikaacha kuisoma.

Ni nini kilikuchochea uanze tena kujifunza Biblia?

Wazo la kwamba kuna Muumba lilikuwa jipya kwangu, hivyo niliamua kufanya utafiti kuhusu jambo hilo

Mwaka wa 1990, nilitembelewa na Shahidi wa Yehova ambaye alinionyesha ahadi ya Biblia kuhusu hali nzuri ya wanadamu wakati ujao. Alifanya mpango ili wenzi wa ndoa wanitembelee na kunisaidia kuielewa Biblia. Baadaye, mke wangu, Liping, ambaye alikuwa mwalimu wa fizikia katika shule ya sekondari nchini China na hakuamini kwamba kuna Mungu, alianza pia kujifunza Biblia. Tulijifunza yale ambayo Biblia inasema kuhusu chanzo cha uhai. Wazo la kwamba kuna Muumba lilikuwa jipya kwangu, hivyo niliamua kufanya utafiti kuhusu jambo hilo.

Ulifanyaje hivyo?

Nikiwa mtaalamu wa hesabu, nilifundishwa kuchunguza uwezekano wa matukio. Pia nilijifunza kwamba ili uhai ujitokeze wenyewe, ni lazima molekuli za protini ziwepo. Hivyo, nilichunguza uwezekano wa protini kujitokeza bila mwongozo wowote. Protini ni kati ya molekuli tata sana, na chembe hai zina maelfu ya protini mbalimbali zinazochangamana kwa njia ya pekee sana. Kama wataalamu wengine, nilitambua kwamba molekuli za protini haziwezi kujitokeza zenyewe. Sijasoma chapisho lolote la nadharia ya mageuzi linaloeleza kwa njia inayosadikisha jinsi ambavyo molekuli hizi tata zilijitokeza zenyewe, sembuse viumbe hai wanaofanyizwa na molekuli hizo. Mambo hayo hakika yalinithibitisha kwamba kuna Muumba.

Ni nini kilikuthibitishia kwamba Biblia ni kitabu cha Mungu?

Kadiri nilivyoendelea kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilijifunza kwamba Biblia ina unabii mwingi wenye habari hususa ambao umetimizwa. Pia nilianza kujionea faida za kutumia kanuni za Biblia maishani. Nilijiuliza hivi: ‘Inawezekanaje kwamba waandikaji wa Biblia ambao waliishi maelfu ya miaka iliyopita waandike maneno yenye hekima yanayotufaidi hadi leo?’ Hatua kwa hatua, nilielewa kwamba Biblia ni Neno la Mungu.

Kwa nini unaendelea kuamini kwamba kuna Muumba?

Ninapofikiria vitu vingi vya msingi vilivyo duniani, sina shaka kwamba kuna Muumba. Kwa sasa, mimi huunda programu za kompyuta, na inashangaza jinsi ambavyo ubongo wetu unazidi uwezo wa programu za kompyuta. Kwa mfano, inastaajabisha sana kuona jinsi ubongo wetu unavyoweza kutambua kile kinachosemwa na mtu hata kama sentensi hazijakamilika, kuna kicheko, kikohozi, kigugumizi, lafudhi tofauti, kelele, au matatizo ya simu. Huenda hilo lisikushangaze. Lakini wataalamu wa programu za kompyuta wanastaajabishwa sana na jambo hilo. Hata programu bora zaidi inayoweza kutambua maneno haiwezi kulinganishwa na uwezo wa ubongo wa mwanadamu.

Tofauti na kompyuta hata zilizo tata zaidi, ubongo wetu unaweza kutambua hisia, lafudhi, na kutofautisha wasemaji kutokana na sauti zao. Wataalamu wa programu za kompyuta wanafanya utafiti wa jinsi wanavyoweza kuboresha uwezo wa programu hizo ili uwe kama wa ubongo wa mwanadamu. Ninaamini kwamba kwa kufanya hivyo, wanajifunza kuhusu uumbaji wa Mungu.