Barua ya Pili kwa Wakorintho 8:1-24

  • Mchango kwa ajili ya Wakristo wa Yudea (1-15)

  • Tito kutumwa Korintho (16-24)

8  Basi akina ndugu, tunawajulisha kuhusu fadhili zisizostahiliwa za Mungu ambazo makutaniko ya Makedonia+ yamepewa.  Wakati wa majaribu makali chini ya mateso, shangwe yao nyingi na umaskini mkubwa ulifanya utajiri wa ukarimu wao uwe mwingi.*  Kwa maana ilikuwa kulingana na uwezo wao,+ ndiyo, ninashuhudia, hata kupita uwezo wao,+  nao kwa kupenda kwao wenyewe waliendelea kutuomba sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili, ili washiriki katika huduma ya kutoa msaada kwa ajili ya watakatifu.+  Na si kama tulivyotumaini tu, bali kwanza walijitoa wenyewe kwa Bwana na kwetu kupitia mapenzi ya Mungu.  Basi tukamtia moyo Tito+ kwamba kama vile alivyokuwa ameanzisha kazi hii kati yenu, pia akamilishe utoaji huu wenye fadhili kwa upande wenu.  Hata hivyo, kama vile mlivyo na utajiri katika kila jambo, katika imani na neno na ujuzi na bidii yote na katika upendo wetu kwenu, pia mzidi katika utoaji huu wenye fadhili.+  Sisemi hivi ili kuwaamuru, bali kuwajulisha kuhusu bidii ya wengine na kuujaribu uhalisi wa upendo wenu.  Kwa maana mnazijua fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba ingawa alikuwa tajiri, alikuja kuwa maskini kwa ajili yenu,+ ili muwe matajiri kupitia umaskini wake. 10  Kuhusu jambo hili ninatoa maoni yangu:+ Hii ni kwa ajili ya faida yenu, kwa kuwa tayari mwaka mmoja uliopita hamkuchukua tu hatua, bali pia mlionyesha tamaa ya kufanya hivyo. 11  Hivyo basi, malizeni pia kile mlichoanza kufanya, ili utayari wenu wa kutenda ukamilishwe kulingana na uwezo mlio nao. 12  Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho,+ si kulingana na kile ambacho mtu hana. 13  Kwa maana sitaki kufanya iwe rahisi kwa wengine, lakini vigumu kwenu; 14  bali kwamba kupitia usawazisho, ziada yenu kwa sasa ijazie uhitaji wao, ili ziada yao pia ijazie upungufu wenu, ili kuwe na usawazisho. 15  Kama ilivyoandikwa: “Mtu aliyekuwa na vingi hakuwa na vingi mno, na mtu aliyekuwa na vichache hakuwa na vichache mno.”+ 16  Basi shukrani kwa Mungu kwa kumfanya Tito awahangaikie ninyi kwa bidii ileile kutoka moyoni,+ 17  kwa sababu kwa kweli ameitikia tulipomtia moyo, lakini akiwa mwenye bidii sana, anakuja kwenu kwa kupenda kwake mwenyewe. 18  Lakini pamoja naye tunamtuma ndugu ambaye sifa yake kuhusiana na habari njema imeenea katika makutaniko yote. 19  Si hayo tu, bali pia makutaniko yalimweka rasmi asafiri pamoja nasi tunaposhughulikia zawadi hii ya fadhili kwa ajili ya utukufu wa Bwana na kwa uthibitisho wa utayari wetu wa kusaidia. 20  Hivyo, tunaepuka kulaumiwa na mtu yeyote kuhusiana na mchango huu wa ukarimu ambao tunaushughulikia.+ 21  Kwa maana ‘tunashughulikia mambo yote kwa unyoofu, si machoni pa Yehova* tu bali pia machoni pa wanadamu.’+ 22  Zaidi ya hayo, pamoja nao tunamtuma ndugu yetu ambaye mara nyingi tumemjaribu na kuona ana bidii katika mambo mengi, lakini sasa ana bidii nyingi zaidi kwa sababu ya uhakika wake mkubwa kwenu. 23  Ingawa hivyo, kama kuna swali lolote kumhusu Tito, yeye ni mwenzangu* na mfanyakazi mwenzi kwa ajili ya faida yenu; au kama kuna swali kuhusu ndugu zetu, wao ni mitume wa makutaniko na utukufu wa Kristo. 24  Basi thibitisheni upendo wenu kwao,+ na mwonyeshe makutaniko sababu iliyofanya tujisifu kuwahusu ninyi.

Maelezo ya Chini

Au “ufurike.”
Tnn., “mshiriki.”