Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu za Kuitegemea Biblia

5. Unabii Uliotimizwa

5. Unabii Uliotimizwa

Hebu wazia mtabiri wa hali ya hewa ambaye ana rekodi ya muda mrefu ya kuwa sahihi nyakati zote. Ikiwa angetabiri kwamba mvua itanyesha, je, ungebeba mwavuli?

BIBLIA imejaa utabiri, au unabii. * Rekodi yake katika historia ni wazi. Unabii wa Biblia ni sahihi nyakati zote.

Mambo ya pekee.

Mara nyingi unabii wa Biblia hutaja mambo hususa nayo yametimizwa hata katika mambo madogo-madogo. Kwa kawaida, unabii huo huhusisha mambo muhimu na hutabiri mambo tofauti na matarajio ya wale wanaoishi wakati unabii huo unapoandikwa.

Mfano wenye kutokeza.

Jiji la kale la Babiloni lililojengwa likiwa limezungukwa na Mto Efrati, liliitwa “kitovu cha kisiasa, kidini, na utamaduni cha nchi za kale za Mashariki.” Mnamo 732 K.W.K., nabii Isaya aliandika unabii wa maangamizi. Alisema kwamba Babiloni litaanguka. Isaya alitaja mambo hususa: Kiongozi anayeitwa “Koreshi” ndiye angekuwa mshindi, maji ya Mto Efrati ‘yatakaushwa’ na malango ya jiji ‘hayatafungwa.’ (Isaya 44:27–45:3) Miaka 200 hivi baadaye, Oktoba 5, 539 K.W.K. (5/10/539), kila sehemu ya unabii huo ilitimizwa. Mwanahistoria Mgiriki Herodotus (wa karne ya tano K.W.K.) alithibitisha jinsi Babiloni lilivyoanguka. *

Sehemu ya unabii yenye kushangaza.

Isaya alitoa utabiri mwingine wenye kushangaza kuhusu Babiloni: “Hatakaliwa kamwe.” (Isaya 13:19, 20) Lilikuwa jambo la ujasiri kutabiri kwamba jiji lenye utendaji mwingi na lililojengwa mahali panapofaa sana lingefanywa ukiwa kabisa. Kwa kawaida, ingetarajiwa kwamba jiji kama hilo lingejengwa tena ikiwa lingeharibiwa. Ingawa Babiloni liliendelea kwa muda fulani baada ya kushindwa, mwishowe maneno ya Isaya yalithibitika kuwa ya kweli. Gazeti Smithsonian linaripoti kuwa leo eneo la Babiloni la kale “ni tambarare, lenye joto, halina mtu na lina vumbi jingi.”

Inapendeza kufikiria umuhimu wa unabii wa Isaya. Kile alichotabiri kinalingana na mtu kutabiri njia hususa ambayo jiji la kisasa, kama vile New York au London, litaharibiwa miaka 200 kutoka sasa, kisha kusema kwa mkazo kwamba jiji hilo halitakaliwa tena. Bila shaka, jambo lenye kupendeza zaidi ni kwamba unabii wa Isaya ulitimia! *

Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba kiongozi anayeitwa Koreshi angeshinda Babiloni lenye nguvu

Katika makala hizi, tumechunguza uthibitisho mbalimbali ambao umewasadikisha mamilioni ya watu kwamba Biblia inategemeka. Kwa sababu hiyo, wao huiona kuwa mwongozo unaotegemeka wa kuongoza hatua zao. Kwa nini usijifunze mengi kuhusu Biblia ili ujiamulie ikiwa wewe pia unaweza kuitegemea?

^ fu. 4 Utabiri wa hali ya hewa unaonyesha mambo ambayo huenda yakatukia. Unabii wa Biblia umeongozwa na Mungu, ambaye anaweza kubadilisha mambo akiamua kufanya hivyo.

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu kutimizwa kwa unabii wa Isaya, ona ukurasa wa 27-29 wa broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 8 Ili kupata mifano zaidi ya unabii wa Biblia na mambo hakika ya kihistoria yanayothibitisha unabii huo, ona ukurasa wa 117-133 wa kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.