Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu za Kuitegemea Biblia

4. Ni Sahihi Kisayansi

4. Ni Sahihi Kisayansi

Sayansi imepiga hatua kubwa katika nyakati za karibuni. Kwa sababu hiyo, nadharia za kisasa zimechukua mahali pa zile za kale. Kile ambacho wakati mmoja kilionekana kuwa kweli sasa huonekana kuwa hadithi tu. Mara nyingi vitabu vya kufundishia sayansi huhitaji kurekebishwa.

BIBLIA si kitabu cha kufundishia sayansi. Hata hivyo, kuhusiana na mambo ya kisayansi, Biblia haitambuliwi tu kwa mambo inayosema bali pia kwa yale isiyosema.

Haina maoni yasiyo ya kisayansi.

Nadharia nyingi zisizo za kweli zilikubaliwa na watu wengi zamani. Kuna wale waliosema kuwa dunia ni tambarare na wengine wakasema kuwa inashikiliwa na vitu fulani. Muda mrefu kabla ya wanasayansi kugundua jinsi ambavyo magonjwa huambukizwa na jinsi ya kuyazuia, madaktari walitumia mbinu ambazo hazingefanya kazi au hata zilizowaua watu. Lakini katika sura zake zaidi ya 1,100, Biblia haijapendekeza hata mara moja maoni yoyote yasiyo ya kisayansi au mazoea yanayodhuru.

Maneno yanayopatana na sayansi.

Miaka 3,500 iliyopita, Biblia ilisema kwamba dunia inaning’inia “pasipo na kitu.” (Ayubu 26:7) Katika karne ya nane K.W.K., Isaya alisema kwa njia ya wazi kuhusu “mviringo wa [au, duara ya] dunia.” (Isaya 40:22) Je, kusema kwamba dunia ni ya mviringo na inaning’inia pasipo kitu si wazo linalopatana na sayansi ya kisasa?

Sheria ya Musa, iliyoandikwa mnamo 1500 K.W.K. (inayopatikana katika vitabu vitano vya kwanza vya Biblia) ilitoa sheria zinazofaa kuhusu kuwatenga wagonjwa, kushughulika na miili iliyokufa, na kushughulikia uchafu.—Mambo ya Walawi 13:1-5; Hesabu 19:1-13; Kumbukumbu la Torati 23:13, 14.

Kwa sababu ya kutumia darubini zenye nguvu kuangalia mbingu, wanasayansi walisema kwamba ulimwengu ulitokea ghafula. Si wanasayansi wote wanaopenda maelezo hayo. Profesa mmoja alisema: “Ulimwengu uliotokea unaonyesha kuwa lazima uwe ulitokezwa na kitu fulani; ni nani anayeweza kuwazia matokeo yanayoonekana bila mwanzilishi?” Hata hivyo, muda mrefu kabla ya darubini kubuniwa, andiko la kwanza la Biblia lilisema wazi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”—Mwanzo 1:1.

Zamani sana, Biblia ilisema kwa usahihi kwamba dunia ni duara na inaning’inia “pasipo na kitu”

Ingawa Biblia ni kitabu cha zamani kinachozungumzia mambo mengi, hakina kasoro zozote za kisayansi. Je, kitabu kama hicho hakistahili kuchunguzwa? *

^ fu. 9 Ili upate mifano zaidi inayoonyesha kwamba Biblia ni sahihi kisayansi, ona ukurasa wa 18-21 katika broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.