Barua ya Kwanza ya Petro 4:1-19

  • Kuishi kwa ajili ya mapenzi ya Mungu, kama alivyofanya Kristo (1-6)

  • Mwisho wa mambo yote umekaribia (7-11)

  • Kuteseka kwa kuwa Mkristo (12-19)

4  Kwa kuwa Kristo aliteseka katika mwili,+ ninyi pia jiimarisheni kwa mwelekeo uleule wa akili;* kwa sababu mtu ambaye ameteseka katika mwili ameachana na dhambi,+  ili aishi wakati wake uliobaki katika mwili, si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena,+ bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.+  Kwa maana wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa,+ mlipofanya vitendo vya mwenendo mpotovu,* uchu, kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu,* mashindano ya kunywa, na ibada za sanamu zenye kuchukiza.+  Wanashangaa kwa sababu hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo uliooza wa upotovu, basi wanawatukana ninyi.+  Lakini watu hao watatoa hesabu kwa yule aliye tayari kuhukumu walio hai na waliokufa.+  Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu habari njema ilitangazwa kwa wafu pia,+ ili ingawa wanahukumiwa katika mwili kwa maoni ya wanadamu, waishi kwa kupatana na roho kwa maoni ya Mungu.  Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, iweni na utimamu wa akili,+ na kukesha* kuhusiana na sala.+  Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana,+ kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.+  Mkaribishane bila kunung’unika.+ 10  Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni kuhudumiana kama wasimamizi wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.+ 11  Yeyote akisema, na afanye hivyo kana kwamba anasema maneno matakatifu kutoka kwa Mungu; yeyote akihudumu, na afanye hivyo kama anayetegemea nguvu ambazo Mungu hutoa;+ ili katika mambo yote Mungu atukuzwe+ kupitia Yesu Kristo. Utukufu na nguvu ni zake milele na milele. Amina. 12  Wapendwa, msishangazwe na majaribu makali* yanayowapata,+ kana kwamba mnapatwa na jambo geni. 13  Badala yake, endeleeni kushangilia+ kwa kadiri ambayo ninyi ni washiriki katika mateso ya Kristo,+ ili mshangilie na kuwa na shangwe sana pia wakati wa ufunuo wa utukufu wake.+ 14  Ikiwa mnashutumiwa* kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha,+ kwa sababu roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu. 15  Hata hivyo, yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mkosaji au mtu anayejiingiza katika mambo ya watu wengine.+ 16  Lakini yeyote akiteseka kwa sababu ni Mkristo, asione aibu,+ bali na aendelee kumtukuza Mungu huku akilibeba jina hili. 17  Kwa maana ni wakati uliowekwa wa hukumu kuanza na nyumba ya Mungu.+ Sasa ikiwa inaanza na sisi kwanza,+ basi matokeo kwa wale wasiotii habari njema ya Mungu yatakuwaje?+ 18  “Na ikiwa mtu mwadilifu anaokolewa kwa shida, itakuwaje kwa mtu asiyemwogopa Mungu na mtenda dhambi?”+ 19  Hivyo basi, acheni wale wanaoteseka kwa kufanya mapenzi ya Mungu waendelee kujikabidhi wenyewe* kwa Muumba mwaminifu wanapotenda mema.+

Maelezo ya Chini

Au “azimio lilelile; uamuzi uleule.”
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.
Au “karamu za kupindukia.”
Au “muwe chonjo; muwe macho.”
Au “majaribu kama moto.”
Au “mnatukanwa.”
Au “kuzikabidhi nafsi zao.”