Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

2 Wakorintho 12:9—“Neema Yangu Yakutosha”

2 Wakorintho 12:9—“Neema Yangu Yakutosha”

 “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha, kwa kuwa nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.”​—2 Wakorintho 12:9, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu.”​—2 Wakorintho 12:9, Union Version.

Maana ya 2 Wakorintho 12:9

 Katika mstari huu Mungu anamwahidi mtume Paulo kwamba atampa nguvu anazohitaji kukabiliana na majaribu na udhaifu wake.

 “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha.” Jibu la Mungu kwa sala ambazo Paulo alitoa tena na tena linaweza pia kuandikwa “unachohitaji tu ni fadhili zangu.” Kwa maneno mengine, fadhili zisizostahiliwa za Mungu zingetosha kumsaidia Paulo kukabiliana na majaribu yake. Jinsi gani? Neno linalotafsiriwa “fadhili zisizostahiliwa,” au “neema,” linafafanua zawadi ya bure na isiyostahiliwa inayotolewa kwa ukarimu na Mungu. Mambo ambayo Paulo aliandika yanaonyesha kwamba alinufaika kwa njia kubwa kutokana na fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Ingawa hapo awali Paulo alikuwa akiwatesa watu, Mungu alimpa nguvu alizohitaji ili kubadili tabia yake na kuwasaidia wengine kuwa Wakristo. (1 Wakorintho 15:9, 10; 1 Timotheo 1:12-14) Paulo angeweza kumtegemea Mungu akiwa na uhakika kwamba angemsaidia kushinda matatizo au changamoto zozote alizokabili.

 “Kwa kuwa nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.” Bwana Yehova a anamkumbusha Paulo kwamba nguvu Zake zinadhihirika zaidi wakati zinatenda kupitia wanadamu dhaifu na wasio wakamilifu. (2 Wakorintho 4:7; 12:8) Wakristo wanapotambua mipaka yako na kumtegemea Yehova awasaidie, wanaruhusu nguvu za Mungu zitende kikamili ndani yao. (Waefeso 3:16; Wafilipi 4:13) Kwa njia hiyo, nguvu za Mungu zinaonekana katika udhaifu wa mwanadamu.

Muktadha wa 2 Wakorintho 12:9

 Mwaka wa 55 W.K. hivi, Paulo aliandika barua iliyoongozwa na roho kwa Wakristo huko Korintho. Katika sehemu ya mwisho ya barua hiyo, alitetea mamlaka yake ya kuwa mtume. Alihisi kwamba alihitaji kufanya hivyo kwa sababu watu fulani waliojipendekeza kuwa walimu walikuwa wamemchambua, labda wakimhukumu kwa sababu ya mwonekano wake au uwezo wake wa kuzungumza.​—2 Wakorintho 10:7-10; 11:5, 6, 13; 12:11.

 Akijitetea, Paulo alieleza kwamba asingaliweza kukamilisha huduma yake na kuvumilia majaribu yake mengi kwa nguvu zake mwenyewe. (2 Wakorintho 6:4; 11:23-27; 12:12) Katika sura ya 12, anataja kuhusu “mwiba katika mwili,” ambao inaonekana ulikuwa ugonjwa wa kuendelea uliokuwa ukimsababishia maumivu mengi ya kimwili au ya kihisia. (2 Wakorintho 12:7) Ingawa Paulo hakufafanua tatizo hilo lilikuwa lipi, alikuwa ameazimia kulivumilia kwa msaada wa Mungu.

 Leo huenda Wakristo pia wakakabili hali ngumu na mateso. Wanafarijika kujua kwamba nguvu za Mungu zinaweza kuwapa uwezo wa kupambana na changamoto zozote ambazo huenda wakakabili. Kama Paulo, wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.”​—2 Wakorintho 12:10.

 Tazama video hii fupi ili upate habari zaidi kuhusu kitabu cha 2 Wakorintho.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?