Hamia kwenye habari

Yesu Alizaliwa Lini?

Yesu Alizaliwa Lini?

Jibu la Biblia

 Biblia haitaji tarehe hususa ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo, kama vitabu hivi vya marejezo vinavyoonyesha:

  •   “Tarehe halisi ya kuzaliwa kwa Kristo haijulikani.”— New Catholic Encyclopedia.

  •   “Tarehe hususa ambayo Kristo alizaliwa haijulikani.”— Encyclopedia of Early Christianity.

 Ingawa Biblia haijibu moja kwa moja swali hili, ‘Yesu alizaliwa lini?’ inaeleza matukio mawili yanayohusiana na kuzaliwa kwake ambayo yanawafanya watu wengi wafikie mkataa wa kwamba hakuzaliwa Desemba 25.

Hakuzaliwa wakati wa majira ya baridi kali a

  1.   Uandikisho. Muda mfupi kabla ya Yesu kuzaliwa, Kaisari Augusto alitoa amri kwamba “dunia yote inayokaliwa iandikishwe.” Kila mtu alipaswa kujiandikisha katika “jiji lake mwenyewe,” na huenda hilo lilimaanisha wazazi wa Yesu wafunge safari ya juma moja au zaidi. (Luka 2:1-3) Amri hiyo—ambayo huenda ilitolewa kwa ajili ya kutoza ushuru na kuandikisha watu jeshini—haingekubaliwa na wengi wakati wowote ule, lakini yaelekea kwamba Augusto hangewaudhi watu zaidi kwa kuwalazimisha wafunge safari hiyo ndefu wakati wa majira ya baridi kali.

  2.   Kondoo. Wachungaji walikuwa “wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku.” (Luka 2:8) Kitabu Daily Life in the Time of Jesus kinasema kwamba mifugo ilikuwa katika maeneo yaliyo wazi kuanzia “juma la kabla ya Pasaka [mwishoni mwa Machi]” hadi katikati ya Novemba. Kinaongezea hivi: “Katika majira ya baridi kali walikuwa ndani ya nyumba; na hilo peke yake linafanya tarehe ya Krismasi, katika majira ya baridi kali, kuwa si sahihi kwa sababu Injili inasema wachungaji walikuwa mashambani.”

Alizaliwa katika majira ya kupukutika kwa majani b

 Tunaweza kukadiria wakati ambapo Yesu alizaliwa kwa kuhesabu tukirudi nyuma kuanzia wakati wa kifo chake wakati wa Pasaka ya Nisani 14 katika majira ya masika ya mwaka wa 33 W.K. c (Yohana 19:14-16) Yesu alikuwa na umri wa karibu miaka 30 alipoanza huduma yake ya miaka mitatu na nusu, kwa hiyo alizaliwa mwanzoni mwa mwezi wa Oktoba, mwaka wa 2 K.W.K.—Luka 3:23.

Kwa nini Krismasi huadhimishwa Desemba 25?

  Kwa kuwa hakuna uthibitisho kwamba Yesu Kristo alizaliwa Desemba 25, kwa nini Krismasi husherehekewa siku hiyo? Kitabu Encyclopædia Britannica kinasema kwamba inaelekea kwamba viongozi wa kanisa walichagua tarehe hiyo “ili ipatane na sherehe ya kipagani ya Waroma ya ‘kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa,’” wakati wa majira ya baridi kali. Kitabu The Encyclopedia Americana kinasema kwamba wasomi wengi wanaamini kwamba tarehe hiyo ilichaguliwa “ili kufanya Ukristo uwe wa maana zaidi kwa wapagani waliogeuza imani yao.”

a Katika eneo ambalo Yesu alizaliwa, majira ya baridi kali huwa kati ya mwezi wa Desemba na Februari.

b Katika eneo ambalo Yesu alizaliwa, majira ya kupukutika kwa majani huwa kati ya mwezi wa Septemba na Novemba.

c Katika eneo ambalo Yesu alizaliwa, majira ya masika huwa karibu na mwishoni mwa mwezi wa Machi na mwanzoni mwa Aprili.