Hamia kwenye habari

Je, Mungu Hubadili Maoni Yake?

Je, Mungu Hubadili Maoni Yake?

Jibu la Biblia

 Ndiyo. Anafanya hivyo katika maana ya kwamba watu wanapobadili mwenendo wao, yeye hutenda kwa njia tofauti na aliyokusudia. Kwa mfano, Mungu alipowatumia ujumbe wa hukumu watu wa taifa la kale la Israeli, alisema hivi: “Labda watasikiliza na kurudi, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya, nami nitajuta msiba ninaofikiria kuleta juu yao kwa sababu ya ubaya wa matendo yao.”​—Yeremia 26:3.

 Tafsiri nyingi za Biblia hutafsiri mstari huo kwa njia inayoonyesha kwamba Mungu “angetubu” kuhusiana na msiba aliotaka kuleta, lakini hilo linaweza kumaanisha kwamba alikuwa amekosea. Hata hivyo, neno la awali la Kiebrania linaweza kumaanisha “kubadili maoni au nia.” Msomi mmoja aliandika hivi: “Mungu hubadili hukumu mwanadamu anapobadili mwenendo wake.”

 Kwa kweli, kwa kuwa Mungu anaweza kubadili maoni yake haimaanishi kwamba lazima ayabadili. Fikiria hali fulani zinazotajwa katika Biblia zinazoonyesha kwamba Mungu hajabadili maoni yake:

  •   Mungu hakumruhusu Balaki abadili maoni Yake na kulaani taifa la Israeli.​—Hesabu 23:18-​20.

  •   Mfalme Sauli wa Israeli alipoazimia kuendelea kutenda mabaya, Mungu hakubadili maoni yake kuhusu kumkataa asiwe mfalme.​—1 Samweli 15:28, 29.

  •   Mungu atatimiza ahadi yake ya kumfanya Mwana wake kuwa kuhani milele. Mungu hatabadili maoni Yake kuhusu jambo hilo.​—Zaburi 110:4.

Je, Biblia haisemi kwamba Mungu habadiliki kamwe?

 Ndiyo. Biblia inasema kwamba Mungu alisema hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika.” (Malaki 3:6) Vivyo hivyo, Biblia inasema kwamba Mungu “habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yakobo 1:17) Hata hivyo, hilo halipingani na wazo la Biblia kuhusu jinsi Mungu anavyobadili maoni yake. Mungu habadiliki katika maana ya kwamba utu wake na viwango vyake vya upendo na haki havibadiliki kamwe. (Kumbukumbu la Torati 32:4; 1 Yohana 4:8) Hata hivyo, anaweza kuwapa watu maagizo tofauti katika pindi tofauti. Kwa mfano, Mfalme Daudi alipopigana katika vita viwili vilivyofuatana, Mungu alimpa maagizo tofauti kwa ajili ya kila kisa, lakini mbinu zote mbili zilifanikiwa.​—2 Samweli 5:​18-​25.

Je, Mungu anajuta kwamba aliwaumba wanadamu?

 Hapana, ingawa anasikitika kwamba watu wengi wanampuuza au kumkataa. Ikifafanua jinsi hali zilivyokuwa kabla ya Gharika ya siku za Noa, Biblia inasema hivi: “Yehova akajuta kwamba amewafanya wanadamu duniani, naye akaumia moyoni mwake.” (Mwanzo 6:6) Katika mstari huo, neno “akajuta” linatokana na neno ya Kiebrania linaloweza kumaanisha “kubadili maoni.” Mungu alibadili maoni yake kuhusu watu wengi walioishi kabla ya Gharika kwa sababu walikuwa waovu. (Mwanzo 6:​5, 11) Hata ingawa alihuzunika kwa sababu walichagua kutenda kwa njia isiyofaa, hakubadili mtazamo wake kuelekea jamii yote ya wanadamu. Kwa kweli aliwakomboa wanadamu kutokana na Gharika kupitia Noa na familia yake.​—Mwanzo 8:​21; 2 Petro 2:​5, 9.