Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Maoni Yanayofaa Kuhusu Sifa Zinazokukasirisha

Maoni Yanayofaa Kuhusu Sifa Zinazokukasirisha
  •   Unapenda kufanya mambo yanapojitokeza; mwenzi wako anahitaji kila kitu kipangwe.

  •   Wewe ni mnyamavu na hupendi sana kuchangamana na watu; mwenzi wako ni mzungumzaji anayependa kuchangamana na watu.

 Je, kuna sifa ya mwenzi wako inayokukasirisha? Kukazia fikira jambo hilo kunaweza kudhuru ndoa yako. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba “yule anayeendelea kuongea kuhusu jambo huwatenganisha marafiki wa karibu.”—Methali 17:9.

 Badala ya kuruhusu sifa zinazokasirisha ziwafanye mzozane, huenda unaweza kujifunza kuona sifa hiyo kwa njia nzuri zaidi.

Katika makala hii

 Maoni yanayofaa kuhusu mambo yanayokukasirisha

 Sifa ya mwenzi wako inayokukasirisha inaweza kuhusiana na sifa fulani unayopenda. Fikiria mifano mitatu:

 “Mara nyingi mume wangu hufanya mambo polepole au kujitayarisha polepole kwenda mahali fulani. Lakini sifa hiyo humfanya awe mwenye subira—hata anaposhughulika nami. Nyakati nyingine mwendo wake wa polepole hunikasirisha, lakini pia ndiyo sababu moja ninayompenda.”—Chelsea.

 “Mke wangu hupanga mambo kwa makini sana; anahitaji kuhisi kwamba anadhibiti kila kitu, na hilo linaweza kukasirisha. Kwa upande mwingine, umakini wake unamaanisha kwamba hakuna jambo linalotushtukiza.”—Christopher.

 “Mume wangu anaweza kuonekana kuwa hapendezwi na mambo mengi, na hilo linaweza kuudhi. Lakini wakati huohuo utulivu wake ni mojawapo ya mambo ambayo yalinivutia kwake. Ninapenda uwezo wake wa kuwa mtulivu hata kunapokuwa na hali zenye mkazo.”—Danielle.

 Kama Chelsea, Christopher, na Danielle walivyogundua, uwezo na udhaifu wa wenzi wao mara nyingi ni sehemu mbalimbali za sifa ileile. Inapokuwa hivyo, huwezi kuondoa udhaifu bila kuondoa uwezo, kama tu ambavyo huwezi kuondoa upande mmoja wa sarafu.

 Bila shaka, sifa fulani hazina upande unaofaa. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba watu fulani ‘hukasirika upesi.’ (Methali 29:22) Inapokuwa hivyo, mtu anapaswa kufanya yote anayoweza kuepuka “kila aina ya chuki yenye uhasama, hasira, ghadhabu, kufoka, matusi.” aWaefeso 4:31.

 Lakini ikiwa sifa fulani inakuudhi tu, fuata ushauri huu wa Biblia: “Endeleeni kuvumiliana . . . hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika.”—Wakolosai 3:13.

 Mbali na hilo, jaribu kutafuta upande unaopendeza wa sifa hiyo—jambo ambalo huenda hata lilikufanya uvutiwe na mwenzi wako. Mume anayeitwa Joseph anasema hivi, “Kukazia fikira jambo lenye kukasirisha ni kama kuzingatia upande wenye makali wa almasi bila kuthamini uzuri wake.”

 Mwongozo wa mazungumzo

 Kwanza, kila mmoja afikirie maswali yafuatayo akiwa peke yake. Kisha zungumzieni majibu yenu pamoja.

  •   Je, mwenzi wako ana sifa ambayo unahisi inasababisha mizozo katika ndoa yenu? Ikiwa ndivyo, ni sifa gani?

  •   Je, sifa hiyo ni mbaya sana, au ni kwamba inakuudhi tu?

  •   Je, kuna upande unaopendeza wa sifa hiyo? Ikiwa ndivyo, ni upi, na kwa nini unathamini jambo hilo kuhusu utu wa mwenzi wako?