Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kusitawisha Subira

Jinsi ya Kusitawisha Subira

 “Sifa ya subira inajaribiwa kila siku katika ndoa. Huenda subira isionekane kuwa suala kubwa ukiwa mseja, lakini ni muhimu sana ili ndoa ifanikiwe.”—John.

 Kwa nini unahitaji subira?

  •   Ndoa inaweza kufanya utambue vizuri makosa ya mwenzi wako.

     “Unapokuwa katika ndoa kwa muda fulani, ni rahisi kukazia fikira sifa mbaya za mwenzi wako. Mtazamo huo mbaya unapoanza, ni rahisi kutokuwa na subira.”—Jessena.

  •   Kukosa subira kunaweza kukufanya uzungumze bila kufikiri.

     “Ninaeleza hisia zangu haraka sana. Ikiwa ningekuwa na subira kidogo, ningekuwa na mtazamo mzuri na kugundua kwamba sihitaji kusema chochote.”—Carmen.

     Biblia inasema: “Upendo ni wenye subira na fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Ni jambo linalopatana na akili kwa watu wawili wanaopendana kuonyeshana subira. Lakini sivyo ilivyo nyakati zote. John aliyenukuliwa mapema anasema hivi: “Kama sifa yoyote nzuri, ni rahisi zaidi kupunguza subira kuliko kuikuza. Inahitaji jitihada nyingi zaidi kuikuza.”

 Unaweza kuonyeshaje subira?

  •   Subira yako inapojaribiwa na jambo lisilotarajiwa.

     Mfano: Mwenzi wako anapozungumza nawe bila fadhili. Huenda wazo la kwanza litakalokuja akilini ni kumjibu bila fadhili.

     Kanuni ya Biblia: “Usikasirike haraka, kwa maana hasira ni dalili ya mjinga.”—Mhubiri 7:9, maelezo ya chini.

     Jinsi ya kuonyesha subira: Tua kidogo. Kabla ya kujibu, jikumbushe kwamba mwenzi wako hakukusudia kukuumiza au kukuaibisha kwa jambo alilosema. Kitabu Fighting for Your Marriage kinasema hivi: “Wengi wetu hutenda kulingana na kile tunachohisi mwenzi wetu anafikiria, bali si kile anachomaanisha kihalisi.

     Hata ikiwa mwenzi wako alikusudia kukukasirisha, kuonyesha subira kwa kujizuia kunaweza kupunguza mkazo badala ya kuuongeza. Biblia inasema, “pasipo na kuni moto huzimika.”—Methali 26:20.

     “Ukianza kumwona mke wako kuwa mpinzani, tua na ufikirie kwa nini unampenda na papo hapo umfanyie jambo zuri.”—Ethan.

     Jambo la kufikiria:

    •  Unatendaje mwenzi wako anaposema au kufanya jambo lisilo la fadhili?

    •  Unawezaje kutenda kwa subira zaidi jambo hilo likitokea wakati ujao?

  •   Jambo linalojirudia linapojaribu subira yako.

     Mfano: Mwenzi wako anachelewa kila wakati, anafanya umsubiri—ukiwa umekasirika.

     Kanuni ya Biblia: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—Wakolosai 3:13.

     Jinsi ya kuonyesha subira: Jitahidi kutanguliza ndoa yenu badala ya mahitaji yako ya kibinafsi. Jiulize, ‘Je, tukigombana au kukasirikiana kwa sababu ya jambo hili tutaimarisha ndoa yetu au tutaivuruga?’ Pia, kumbuka kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Hilo linamaanisha kwamba kuna mambo unayopaswa kufanyia kazi.

     “Wakati mwingine ninawaonyesha subira rafiki zangu kuliko ninavyomwonyesha mume wangu. Nafikiri ni kwa sababu ninatumia muda mwingi na mume wangu na ninajua udhaifu wake. Lakini subira ni sehemu ya upendo—ni ishara ya heshima—basi ni muhimu sana katika ndoa yangu.”—Nia

     Jambo la kufikiria:

    •  Je, una subira kuelekea udhaifu wa mwenzi wako?

    •  Unawezaje kuonyesha subira zaidi wakati ujao?