Hamia kwenye habari

Juu kushoto: Ndugu na dada wakiimba kwa shangwe wimbo wa Ufalme katika Lugha ya Ishara ya Filipino. Chini kushoto: Baadhi ya wahudhuriaji wenye shauku wakifanya ishara za baadhi ya mistari kutoka kwenye kitabu cha Mathayo katika Lugha ya Ishara ya Filipino. Kulia: Ndugu Dean Jacek akitangaza kutolewa kwa Kitabu cha Biblia cha Mathayo

APRILI 29, 2024
FILIPINO

Kitabu cha Biblia cha Mathayo Chatolewa Katika Lugha ya Ishara ya Filipino

Kitabu cha Biblia cha Mathayo Chatolewa Katika Lugha ya Ishara ya Filipino

Wale waliohudhuria wakipiga makofi kwa sababu ya kutolewa kwa kitabu cha Mathayo katika Lugha ya Ishara ya Filipino

Aprili 21, 2024, Ndugu Dean Jacek, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Filipino, alitangaza kutolewa kwa kitabu cha Biblia cha Mathayo katika Lugha ya Ishara ya Filipino wakati wa programu ya pekee iliyofanyika kwenye ofisi ya tawi ya Filipino Jijini Quezon. Jumla ya ndugu na dada 413 walihudhuria programu hiyo uso kwa uso. Ndugu na dada wengine 3,998 kutoka maeneo mbalimbali ya nchi ya Filipino waliunganishwa kupitia video mtandaoni. Kitabu hicho kilikuwa tayari kupakuliwa kwenye jw.org na kwenye programu ya JW Library Lugha ya Ishara.

Inakadiriwa kwamba watu 500,000 wanatumia Lugha ya Ishara ya Filipino. Kutaniko la kwanza la Lugha ya Ishara lilianzishwa katika Jiji la Quezon mwaka wa 1999, na machapisho yanayotegemea Biblia yalitafsiriwa kwa mara ya kwanza katika lugha hiyo mwaka wa 2011. Leo, zaidi ya ndugu na dada 3,000 wanatumikia katika makutaniko na vikundi 72 vya Lugha ya Ishara kote nchini Filipino.

Hiki ni kitabu cha kwanza cha Biblia kilichokamilika kutafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Filipino. Ndugu mmoja ambaye ni kiziwi alisema hivi: “Kabla ya toleo hili, tulikuwa tu na baadhi ya mistari kutoka kwenye kitabu cha Mathayo iliyopatikana katika lugha yetu. Ni kana kwamba tulikuwa tu na baadhi ya vipande vya picha kubwa. Lakini sasa tunaweza kuona picha yote!” Mzee anayetumikia katika kutaniko la Lugha ya Ishara nchini Filipino aliongezea hivi: “Kuna kanuni nyingi katika kitabu cha Mathayo zinazoweza kutusaidia tunapofanya ziara za uchungaji au kuwaimarisha ndugu na dada kutanikoni. Kwa mfano, Mathayo 5:23, 24 inatuchochea kufanya amani na ndugu zetu, kutoelewana kunapotukia. Ninamshukuru Yehova kwa kufanya masomo haya yapatikane katika lugha yetu wenyewe.”

Tunashangilia kutolewa kwa kitabu cha Mathayo katika Lugha ya Ishara ya Filipino, ambayo itawasaidia watu wengi wenye mioyo minyoofu kunufaika kutokana na Neno la Mungu.​—Mathayo 7:24, 25.