SOMO LA 3

Je, Unaweza Kuiamini Biblia?

Je, Unaweza Kuiamini Biblia?

Biblia ina ahadi nyingi na pia inatoa ushauri mwingi. Labda ungependa kujua mambo inayofundisha, lakini huenda una shaka. Je, unaweza kuamini ahadi na ushauri wa kitabu kilichoandikwa zamani sana? Je, kweli unaweza kuamini mambo ambayo Biblia inasema kuhusu kufurahia maisha sasa na wakati ujao? Watu wengi wanaiamini. Wewe pia unaweza kuiamini.

1. Je, mambo yaliyoandikwa katika Biblia ni ya kweli?

Biblia inasema kwamba ina “maneno sahihi ya kweli.” (Mhubiri 12:10) Inasimulia matukio halisi yanayohusu watu halisi. (Soma Luka 1:3; 3:1, 2.) Wanahistoria wengi na wataalamu wa vitu vya kale wamethibitisha usahihi wa tarehe, watu, mahali, na matukio muhimu yanayotajwa katika Biblia.

2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Biblia haijapitwa na wakati?

Biblia inataja mambo mbalimbali ambayo hayakujulikana ilipoandikwa. Kwa mfano, inazungumzia mambo ya kisayansi. Watu wengi hawakuamini mambo iliyotaja kuhusu habari hizo. Hata hivyo, sayansi imethibitisha kwamba habari zilizo katika Biblia ni sahihi. Biblia ‘inategemeka sikuzote, sasa na milele.’​—Zaburi 111:8.

3. Kwa nini tunapaswa kuamini mambo ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao?

Biblia ina unabii * unaotabiri “mambo ambayo bado hayajafanywa.” (Isaya 46:10) Ilitabiri kwa usahihi matukio ya kihistoria muda mrefu kabla hayajatokea. Pia, inataja kihususa hali zilizopo ulimwenguni leo. Katika somo hili, tutachunguza baadhi ya unabii ulio katika Biblia. Unabii huo ulitimia kwa usahihi kabisa!

CHIMBA ZAIDI

Fikiria jinsi Biblia inavyopatana na sayansi, na uchunguze unabii fulani wenye kuvutia ulio katika Biblia.

4. Sayansi inapatana na Biblia

Nyakati za kale, watu wengi waliamini kwamba dunia imeshikiliwa na kitu fulani. Onyesha VIDEO.

Ona jambo ambalo liliandikwa katika kitabu cha Ayubu miaka 3,500 hivi iliyopita. Soma Ayubu 26:7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini inashangaza kwamba maneno dunia inaning’inia “pasipo na kitu” yaliandikwa miaka 3,500 iliyopita?

Mzunguko wa maji duniani ulieleweka vizuri miaka 200 hivi iliyopita. Hata hivyo, ona jambo ambalo Biblia ilisema miaka 3,500 hivi iliyopita. Soma Ayubu 36:27, 28, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Ni nini kinachokupendeza kuhusu ufafanuzi huu rahisi wa mzunguko wa maji?

  • Je, maandiko uliyosoma yamekusaidia kuiamini zaidi Biblia?

5. Biblia ilitabiri matukio muhimu

Soma Isaya 44:27–45:2, kisha mzungumzie swali hili:

  • Biblia ilitaja kihususa habari gani miaka 200 kabla ya kuanguka kwa jiji la Babiloni?

Historia inathibitisha kwamba Mfalme Koreshi wa Uajemi na jeshi lake walilishinda jiji la Babiloni mwaka wa 539 K.W.K. * Waligeuza mkondo wa mto uliolinda jiji hilo. Wakaingia katika jiji kupitia malango yaliyokuwa yameachwa wazi na kuliteka bila kupigana. Leo, zaidi ya miaka 2,500 imepita na bado jiji la Babiloni ni magofu. Ona jambo ambalo Biblia ilitabiri.

Soma Isaya 13:19, 20, kisha mzungumzie swali hili:

  • Unabii kuhusu Babiloni ulitimizwaje?

Magofu ya Babiloni nchini Iraq

6. Biblia ilitabiri hali tunazoona leo

Biblia inasema kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Ona mambo ambayo Biblia ilitabiri kuhusu siku za mwisho.

Soma Mathayo 24:6, 7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Biblia ilitabiri nini kuhusu siku za mwisho?

Soma 2 Timotheo 3:1-5, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Biblia ilitabiri watu wa siku za mwisho wangekuwa na tabia gani?

  • Umejionea mambo gani kati ya hayo yakitimia leo?

WATU FULANI HUSEMA: “Biblia ni kitabu cha hadithi na hekaya.”

  • Ni jambo gani linalokupa uhakika kwamba tunaweza kuiamini Biblia?

MUHTASARI

Matukio ya kihistoria, uthibitisho wa kisayansi, na unabii unatusaidia kuiamini Biblia.

Ungejibuje?

  • Je, mambo yaliyoandikwa katika Biblia ni ya kweli?

  • Ni mambo gani ya kisayansi yanayopatana na Biblia?

  • Je, unaamini kwamba Biblia inatabiri kuhusu wakati ujao? Kwa nini?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Je, Biblia ina habari zisizo sahihi kisayansi?

“Je, Sayansi Inapatana na Biblia?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Jifunze jinsi unabii wa Biblia kuhusu Milki ya Ugiriki ulivyotimizwa.

Kuimarishwa na “Neno la Kinabii” (5:22)

Ona jinsi unabii wa Biblia ulivyobadili maoni ya mwanamume huyu.

“Niliamini Hakuna Mungu” (Mnara wa Mlinzi Na. 5 2017)

^ Unabii unatia ndani ujumbe kutoka kwa Mungu kuhusu wakati ujao.

^ K.W.K. inamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida,” na W.K. inamaanisha “Wakati wa Kawaida.”