Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA

Vijana Wanashuka Moyo—Sababu Gani? Ni Nini Inaweza Kuwasaidia?

Vijana Wanashuka Moyo—Sababu Gani? Ni Nini Inaweza Kuwasaidia?

ANNA * anasema hivi: “Wakati nashuka moyo, nakosa hamu ya kufanya jambo lolote, hata mambo yenye nafurahia kufanya. Napenda tu kulala. Mara nyingi, najisikia kama hakuna mutu mwenye ananipenda, najisikia kuwa mutu wa bure, na muzigo kwa watu wengine.”

Julia anakumbuka mambo yenye yalimufikia. Anasema hivi: “Nilikuwa na mawazo ya kujiua. Kusema kweli, sikupenda kufa. Nilipenda tu nisiendelee kujisikia hivyo. Kwa kawaida, mimi ni mutu mwenye kuhangaikia wengine, lakini wakati nashuka moyo, sihangaikie sana mutu yeyote ao jambo lolote.”

Anna na Julia walikuwa katika mwanzo wa miaka yao ya ujana wakati walishuka moyo kwa mara ya kwanza. Hata kama vijana wengine wanaweza kushuka moyo kwa muda kidogo tu, wakati fulani Anna na Julia walikuwa wanashuka moyo kwa muda wa majuma ao miezi fulani. Anna anasema hivi: “Ni kama kufungwa katika shimo la murefu, lenye kuwa na giza na lenye halina njia ya kutokea. Unajisikia kuwa umevurugika akili, na unajisikia kama hauko vile unakuwaka.”

Wengi wanajikuta katika hali ya Anna na Julia. Hesabu ya vijana wenye kuwa na tatizo la kushuka moyo inaendelea kuongezeka sana. Na kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni (OMS), kushuka moyo ni “sababu kubwa ya magonjwa na ulemavu kwa vijana wanaume na wanawake wa miaka 10 mupaka 19.”

Alama za kushuka moyo zinaweza kutokea wakati wa ujana, na kati ya alama hizo kunaweza kuwa matatizo ya usingizi, kukosa hamu ya kula, na kubadilika kwa kilo ya mwili. Mutu anaweza pia kukata tamaa, kupoteza tumaini, kuwa na huzuni, na kujiona kuwa wa bure. Alama zingine zinaweza kuwa kujitenga na wengine, kuwa na magumu ya kukumbuka ao ya kukaza akili juu ya jambo fulani, matendo ao mawazo ya kutaka kujiua, na alama fulani za magonjwa zenye hazieleweke. Wakati wataalamu wa afya ya akili wanawaza kama mutu anashuka moyo, mara nyingi wanatafuta alama zenye zinaendelea kuonekana kwa majuma fulani na alama zenye kuvuruga maisha ya kawaida ya mutu.

SABABU ZENYE ZINAWEZA KUFANYA VIJANA WASHUKE MOYO

Kulingana na OMS, “kushuka moyo kunaletwa na muchanganyiko wa mambo yenye kutokana na uhusiano wetu na wengine, akili, na mwili.” Kati ya mambo hayo, kunaweza kuwa mambo yenye kufuata:

Mambo yenye kutokana na mwili wa mutu. Kama vile ilikuwa katika hali ya Julia, mara nyingi kushuka moyo kunaletwa na chembe za uriti, pengine chembe hizo zinavuruga namna kemikali inafanya kazi katika ubongo. Mambo mengine yenye kutokana na mwili yanaweza kuwa ugonjwa wa moyo, kuongezeka ao kupunguka kwa homoni, na kutumia dawa za kulewesha. Kuendelea kutumia dawa za kulewesha kunaweza kuongeza mushuko wa moyo, ao kutokeza hali hiyo. *

Mukazo wa akili. Hata kama mukazo kidogo wa akili unaweza kuwa na matokeo mazuri juu ya afya, mukazo wa akili wenye kupita kipimo ao wenye kuendelea unaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya mwili na akili ya mutu, mupaka wakati fulani kufanya kijana mwenye kuwa zaifu kimwili ashuke moyo. Hata hivyo, sababu zenye kufanya mutu ashuke moyo hazijulikane muzuri mupaka sasa, na kama vile tumekwisha kuona, muchanganyiko wa mambo mengi unaweza kuleta tatizo hilo.

Kati ya mambo yenye kutokeza mukazo wa akili yenye yanaweza kumufanya mutu ashuke moyo kunaweza kuwa wazazi kutengana ao kuvunja ndoa yao, kifo cha mupendwa, kutendewa mubaya kimwili ao kingono, aksidenti kubwa, magonjwa, ao tatizo la kujifunza mambo, zaidi sana kama hilo linafanya mutoto ajisikie kwamba hakuna mutu mwenye anamuhangaikia. Jambo lingine linaweza kuwa muzazi kutazamia mutoto atimize mengi zaidi, pengine kwa kuomba mutoto afikie kusudi fulani kwenye masomo. Sababu zingine zinaweza kuwa kuchokozwa, kutokuwa na tumaini kuhusu wakati wenye kuja, kuwa na muzazi mwenye kushuka moyo ambaye hahangaikie namna mutoto wake anajisikia, na kuwa na wazazi wenye hawana musimamo. Kama kijana anashuka moyo, ni nini inaweza kumusaidia?

UHANGAIKIE AKILI NA MWILI WAKO

Tatizo lolote la kushuka moyo linaweza kushugulikiwa kwa kutumia dawa na kwa kufuata mashauri ya munganga wa afya ya akili. * Yesu Kristo alisema hivi: ‘Wale walio na nguvu hawahitaji tabibu [ao, munganga], bali wale walio wagonjwa wanamuhitaji.’ (Marko 2:17) Na ugonjwa unaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya sehemu yoyote ya mwili wetu, kutia ndani ubongo wetu! Inaweza pia kuwa muzuri kubadilisha namna ya kuishi kwa sababu kuna uhusiano mukubwa kati ya akili na mwili wetu.

Kama uko na tatizo la kushuka moyo, ukamate mipango yenye kufaa ili kuhangaikia afya yako ya kimwili na ya kiakili. Kwa mufano, ukule chakula chenye kufaa, ulale vya kutosha, na ufanye mazoezi ya mwili kwa ukawaida. Mazoezi ya mwili yanaweza kusaidia mwili utokeze kemikali zenye zinaweza kukusaidia ujisikie muzuri, kuongeza nguvu zako, na kufanya ulale muzuri zaidi. Kama inawezekana, ujikaze kutambua mambo yenye kutokeza mushuko wa moyo ao alama zenye kuonyesha kwamba uko karibu kushuka moyo na ukamate mipango yenye kufaa ili kupiganisha hali hiyo. Uambie mutu mwenye unatumainia magumu yako. Watu wa familia na marafiki wa sana wanaweza kukusaidia kupiganisha muzuri zaidi mushuko wa moyo, na pengine kupunguza alama fulani. Uandike mawazo na namna unajisikia katika buku fulani; kufanya hivyo kulimusaidia Julia mwenye tumekwisha kutaja. Zaidi ya yote, uhakikishe kwamba unahangaikia afya yako ya kiroho. Hilo linaweza kukusaidia ukuwe na mawazo yenye kufaa juu ya maisha. Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Ukule muzuri, ufanye mazoezi, na ulale vya kutosha

Unaweza kupata kitulizo kwa kutimiza mahitaji yako ya kiroho

Anna na Julia wanakubaliana na maneno ya Yesu. Anna anasema hivi: “Mambo ya kiroho yananisaidia kukaza akili yangu juu ya watu wengine, kuliko tu kukaza akili juu ya magumu yangu. Kufanya hivyo haiko mwepesi sikuzote, lakini hilo linaniletea furaha sana.” Julia anapata kitulizo kupitia sala na usomaji wa Biblia. Anasema hivi: “Kufungulia Mungu moyo wangu katika sala kunanituliza. Na Biblia inanisaidia kuona kwamba Yehova ananiona kuwa mutu wa maana na kwamba ananihangaikia kabisa. Kusoma Biblia kunanisaidia pia kuwa na mawazo mazuri kuhusu wakati wenye kuja.”

Kwa kuwa Yehova Mungu ni Muumbaji wetu, anaelewa muzuri kwamba namna wazazi wetu walitukomalisha, mambo yenye yanatupata katika maisha, na mambo yenye tumeriti kwa wazazi wetu yanaweza kuwa na matokeo juu ya mawazo yetu na namna tunajisikia. Kwa hiyo, iko tayari kututolea kitulizo na musaada wenye tuko nao lazima, pengine kupitia Wakristo wenzetu wenye huruma na wenye kutuelewa. Zaidi ya yote, saa inakuja wakati Mungu atatuponyesha kutokana na magonjwa yote, ya kimwili na ya kiakili. Andiko la Isaya 33:24 linasema hivi: ‘Hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa.’

Ndiyo, Biblia inaahidi kwamba Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [yetu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Hili ni jambo lenye kutia moyo na lenye kutuliza kabisa. Kama unapenda kupata habari zaidi juu ya kusudi la Mungu kuhusu wanadamu na kuhusu dunia, tafazali fungua adresi yetu ya Internete jw.org. Kwenye adresi hiyo, utapata tafsiri ya muzuri ya Biblia, na pia habari zenye kuzungumuzia mambo mbalimbali, kutia ndani kushuka moyo.

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 10 Mamia ya magonjwa, dawa, na dawa za kulewesha vinaweza kubadilisha namna mutu anajisikia moyoni, na kufanya ikuwe lazima kuenda kupimwa kwenye hospitali.

^ fu. 14 Amuka! haipendekezi matunzo ao dawa yoyote ya pekee.