Hamia kwenye habari

Ubora wa Biblia Mpya Watambuliwa Nchini Estonia

Ubora wa Biblia Mpya Watambuliwa Nchini Estonia

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kiestonia ilikuwa miongoni mwa kazi 18 zilizoteuliwa kugombea tuzo ya Language Deed of the Year Award nchini Estonia kwa mwaka wa 2014. Baada ya kura za mwisho kupigwa, tafsiri hiyo ilishinda nafasi ya tatu.

Tafsiri hii mpya ya Biblia iliyotolewa Agosti 8, 2014, ilichaguliwa kugombea tuzo hiyo na mtaalamu wa lugha katika Taasisi ya Lugha ya Kiestonia, Kristiina Ross. Alieleza kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni “rahisi kusoma na inafurahisha,” na akaongezea hivi: “Kazi iliyohusika katika kuitafsiri imeboresha kwa kiasi kikubwa Utafsiri wa Kiestonia.” Rein Veidemann, ambaye ni profesa wa fasihi na utamaduni wa Kiestonia, alisema kuwa tafsiri hiyo ni “utimizo mkubwa.”

Biblia ya kwanza ya Kiestonia ilichapishwa ikiwa nzima katika mwaka wa 1739, na tangu wakati huo tafsiri nyingine zaidi zimetayarishwa. Kwa nini basi isemwe kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni ‘imetimiza jambo kubwa’?

Usahihi. Biblia maarufu ya Kiestonia iliyochapishwa mwaka wa 1988, inatafsiri jina la Mungu kuwa “Jehoova” (Yehova) zaidi ya mara 6,800 katika Maandiko ya Kiebrania (Agano la Kale). * Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiestonia imefanya hata zaidi. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetumia pia jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (Agano Jipya) mahali ambapo kuna msingi wa wazi wa kufanya hivyo.

Inaeleweka kwa urahisi. Je, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni sahihi na inaeleweka kwa urahisi? Toomas Paul, mtafsiri wa Biblia anayeheshimiwa, aliandika katika gazeti Eesti Kirik (Kanisa la Estonia) kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya “imefanikiwa kufikia ubora wa kuwa tafsiri fasaha ya Kiestonia.” Aliongeza hivi: “Nina hakika kwamba hii ndiyo mara ya kwanza kwa ufasaha wa aina hii kufikiwa.”

Wahudhuriaji wa kusanyiko wakitumia tafsiri mpya ya Kiestonia

Toleo hilo la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya lilipokewa vizuri sana na Waestonia. Kituo kimoja cha redio ya taifa kilikuwa na kipindi cha dakika 40 kuhusu Biblia hiyo mpya. Pia, makasisi fulani na waumini wao wamewasiliana na Mashahidi wa Yehova kupata nakala za Biblia hiyo. Shule moja maarufu jijini Tallinn iliagiza nakala 20 za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ili zitumiwe katika darasa moja. Waestonia wanapenda kusoma vitabu, na Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuwaandalia tafsiri sahihi na rahisi kueleweka ya kitabu bora zaidi kuwahi kuandikwa.

^ fu. 5 Baada ya kueleza msingi wa kutamka jina la Mungu kuwa “Jehoova” katika Kiestonia, Ain Riistan, mwenyekiti wa New Testament Studies katika Chuo Kikuu cha Tartu alisema hivi: “Ninaona kwamba katika siku zetu jina Jehoova linafaa kabisa. Licha ya chimbuko lake, limekuwa na . . . maana muhimu na yenye kina kwa vizazi vingi​—Jehoova ni jina la Mungu aliyemtuma Mwana wake kuwakomboa wanadamu.”