Hamia kwenye habari

Kuwafikia Wasinti na Waromani Nchini Ujerumani

Kuwafikia Wasinti na Waromani Nchini Ujerumani

Maelfu ya Wasinti na Waromani wanaishi nchini Ujerumani. * Hivi karibuni, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakichapisha trakti za Biblia, broshua, na video katika lugha yao ya Kiromani. *

Wakati wa kampeni ya pekee iliyofanywa Septemba na Oktoba 2016, Mashahidi wa Yehova walijitahidi kuwahubiria Wasinti na Waromani habari hiyo katika lugha ya Kiromani kwenye majiji mbalimbali ya Ujerumani kutia ndani Berlin, Bremerhaven, Freiburg, Hamburg, na Heidelberg. Pia, walianzisha mikutano ya Kiromani katika majumba yao ya Ufalme.

Itikio la Kupendeza

Wasinti na Waromani wengi walishangazwa na kupendezwa na kampeni hiyo ya Mashahidi wa Yehova. “Watu walifurahi sana kwa sababu tulifanya jitihada za pekee kuwafikia,” walisema Andre na Esther, wenzi walioshiriki kampeni hii. Wengi waliguswa waliposikia na kusoma ujumbe wa Biblia katika lugha yao. Mwanamke mmoja kijana alitazama video ya Kiromani Kwa Nini Ujifunze Biblia? Tena na tena alisema hivi kwa mshangao, “Hii ni lugha yangu!”

Shahidi anayeitwa Matthias, ambaye aliunga mkono kampeni hiyo katika eneo la Hamburg, alisema hivi: “Mimi na mke wangu tulikuwa katika kikundi cha Mashahidi wanane waliotembelea eneo lenye Wasinti na Waromani 400 hivi. Kila mtu tuliyezungumza naye alitaka machapisho.” Bettina, ambaye pia alijitolea katika eneo la Hamburg, alisema hivi: “Baadhi ya watu walilia walipoona kwamba Mashahidi wa Yehova wamechapisha machapisho katika Kiromani.” Wengi wao walianza kusoma kwa sauti machapisho hayo mara moja, na wengine waliomba nakala za ziada kwa ajili ya rafiki zao.

Wasinti na Waromani kadhaa walikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano wa watu wote. Wengi kati ya watu 94 waliohudhuria mikutano huko Hamburg hawakuwa wamewahi kuingia kwenye Jumba la Ufalme. Huko Reilingen, karibu na Heidelberg, watu 123 walihudhuria mkutano. Baadaye, Waromani watano waliomba kujifunza Biblia.

Wakati wa kampeni hiyo, Mashahidi wa Yehova walisambaza trakti na broshua 3,000 hivi. Mashahidi walizungumza na Wasinti na Waromani zaidi ya 360, na 19 kati yao walianza kujifunza Biblia. Baadhi yao walisema, “Tunafurahi sana kwamba Mungu anatukumbuka.”

^ fu. 2 Wasinti ni jamii ndogo ya watu wanaoishi Ulaya Magharibi na Kati, na Waromani ni jamii ndogo ya watu waliotoka Ulaya Mashariki na Kusini-mashariki.

^ fu. 2 Kitabu kimoja cha marejeo (Encyclopædia Britannica Online) kilisema kwamba lugha ya Kiromani ina lahaja “60 au zaidi zenye tofauti mbalimbali.” Ili kurahisisha mambo, makala hii inatumia neno “Kiromani” kurejelea lugha inayozungumzwa na Wasinti na Waromani wa Ujerumani.