Hamia kwenye habari

Jiji Lenye Hazina Laonyesha “Zawadi ya Mungu kwa Wanadamu”

Jiji Lenye Hazina Laonyesha “Zawadi ya Mungu kwa Wanadamu”

Cluj-Napoca, ni mojawapo ya majiji makubwa zaidi ya Romania. Linajulikana kama Jiji Lenye Hazina. Katika maonyesho ya vitabu ya Gaudeamus, yaliyofanywa jijini humo kuanzia Aprili 20 hadi 24, 2016, Mashahidi wa Yehova walizungumzia viwango vya maadili na vya kiroho vinavyopatikana katika Biblia. Walisimamisha kibanda kwenye maonyesho hayo na kuzungumza na maelfu ya wahudhuriaji ambao walitaka kujua kuhusu video, machapisho ya Biblia, na Biblia walizokuwa nazo.

Shule kadhaa zilitembelea maonyesho hayo, na walimu waliwaleta wanafunzi kwenye kibanda cha Mashahidi. Wanafunzi walifurahia hasa kutazama video kwenye mfululizo wenye kichwa Uwe Rafiki ya Yehova, na wengi wao walitaka nakala ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na broshua Wafundishe Watoto Wako. Mfanyakazi mmoja anayeshughulika na watoto alimwambia mwenzake, “Tunahitaji kuandika anwani ya tovuti hii [www.pr418.com] ili tuwaonyeshe watoto vibonzo hivyo vyote.”

Wanafunzi matineja walivutiwa na vibonzo kwenye ubao. Video zilizoonyeshwa zilitia ndani Je, Huu Ni Upendo wa Kweli?, Tumia Mitandao ya Kijamii kwa Hekima, na Mshinde Mnyanyasaji Bila Kutumia Ngumi.

Kasisi wa Kanisa Othodoksi na mke wake walitembelea kibanda hicho mara kadhaa, wakachukua Biblia Takatifu–Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na broshua kadhaa. Kasisi huyo alisema kwamba amevutiwa na sehemu ya “Fahirisi ya Maneno ya Biblia” katika tafsiri hiyo na vyanzo vyenye kutegemeka ambavyo watafsiri walitumia. Aliwapa Mashahidi namba ya simu na kuwaomba wawasiliane naye ili wazungumzie Biblia pamoja.

Mke wa kasisi huyo aliuliza angepata wapi kwenye tovuti ya jw.org habari kwa ajili ya watoto na akaelekezwa kwenye sehemu ya “Watoto” ya tovuti hiyo. Kisha akatazama video Sema Kweli, ambayo alifurahia sana. Baada ya kuchunguza sehemu hiyo, mume wake aliiita “Zawadi ya Mungu kwa wanadamu.”