Hamia kwenye habari

Sala Kwenye Mti wa Mwaloni

Sala Kwenye Mti wa Mwaloni

 Rachel, ambaye sasa anaishi katika Jamhuri ya Dominika anasema hivi: “Nilizaliwa katika familia iliyomtumikia Yehova. Kwa kusikitisha, nilipokuwa na umri wa miaka saba, baba yangu aliacha kushirikiana na watu wa Yehova naye akawa mpinzani mkali dhidi ya kweli. Alifanya iwe vigumu sana kwangu kumtumikia Yehova. Kwa mfano, nyakati nyingine aliniahidi kwamba angenipa vitu kama vile simu, safari ya kwenda Disneyland, au hata kadi ya benki, ikiwa tu ningeacha kumtumikia Yehova! Nyakati nyingine alinipiga ngumi akisema ‘angempiga Yehova atoke ndani yangu.’ Alisema kwamba ikiwa nisingeweza kuzungumza au kutembea, basi nisingeweza kwenda kwenye mikutano. Lakini yote hayo hayakufanikiwa. Sikuzote niliazimia kuhudhuria mikutano.

 “Baba alihakikisha kwamba hanipigi wakati ambapo Mama yupo. Aliniambia kwamba angemuumiza Mama ikiwa ningemjulisha kuwa alikuwa akinipiga. Sikuzote alitoa udhuru kuhusu majeraha niliyopata akisema yalitokana na mazoezi ya kupigana karate ambayo alisisitiza ninapaswa kupata.

 “Nilikuwa mdogo na niliogopa sana kumwambia Mama kilichokuwa kikiendelea. Kwa hiyo, nilimweleza Yehova. Nilitumia muda mwingi katika vichaka vilivyokuwa nyuma ya nyumba yetu kule Maryland, Marekani. Katika vichaka hivyo, kulikuwa na mti mzuri wa mwaloni ambao nilipenda kuupanda, kisha ningeketi kwenye tawi lenye kustarehesha na kuzungumza na Yehova. Nilisali kuhusu hisia zangu na kuhusu mambo ambayo nilimwahidi ningemfanyia baada ya kuwa mkubwa—ikiwa tu angenisaidia niokoke na kufikia umri huo. Pia nilizungumza kuhusu kile ambacho ningefanya katika ulimwengu mpya, familia ambayo ningekuwa nayo, na amani na shangwe ambayo ningepata bila kuwa na maumivu wala woga.

 “Baba yangu alipojaribu kunifanya nimwache Mungu kwa kunihonga au kunipiga, sikuzote nilihisi mkono wa Yehova ukinifariji na kuniimarisha. Mungu alinisaidia niendelee kuwa mshikamanifu na mwenye nguvu.

 “Nilibatizwa nilipokuwa na umri wa miaka kumi, na miaka miwili baadaye nikaanza kufanya upainia. Mwanzoni, baba yangu hakujua chochote kuhusu mambo hayo. Alipogundua, alinipiga ngumi na kunivunja utaya.

 “Watu fulani walinishauri nisianze upainia kwa sababu nilikuwa mdogo sana, na walihofia ikiwa nilielewa uzito wa uamuzi wangu. Lakini kadiri muda ulivyopita, niliona vijana wengi Mashahidi katika eneo letu wakiishi tu bila kukazia fikira mambo ya kiroho. Walikuwa wakijishughulisha na karamu na kufurahia maisha tu. Na mambo waliyofanya yalionekana kuwa yenye kuvutia! Nilishawishika kufanya mambo waliyokuwa wakifanya. Nilijiuliza hivi, ‘Kwa nini nisiache kuhubiri na kufurahia maisha kama vijana wengine wa umri wangu?’ Lakini kila wakati nilipohisi hivyo, nilizungumza na Yehova kuhusu jambo hilo.

 “Nilipokuwa na umri wa miaka 15 hivi, shirika moja la mitindo ya nguo liliwasiliana nami ili kuniajiri. Waliahidi wangenilipa pesa nyingi ikiwa ningefanya kazi nao katika ofisi zao huko Milan, Italia. Nilijihisi vizuri kuambiwa kwamba ningeweza kuwa mwanamitindo, picha zangu zingewekwa kwenye magazeti, na kwamba ningetembea mbele ya watu kwenye matamasha ya mitindo nikiwa nimevalia mavazi ya bei kubwa. Kwa kuwa nilikuwa nimefanya upainia wa kawaida kwa karibu miaka mitatu, niliajiambia, ‘Kazi hii inaweza kunitegemeza kifedha na kuniwezesha kuendelea kufanya upainia kwa muda mrefu sana!’ Baba alikuwa ameatuacha, kwa hiyo niliwaza jinsi ambavyo pesa hizo zingeweza kumsaidia Mama kushughulikia gharama zetu.

 “Nilisali kuhusu jambo hilo. Nikazungumza na mama yangu, ambaye alikuwa painia kwa miaka mingi, na nikazungumza na mzee wa kutaniko ambaye nilimpenda na kumheshimu. Kama kawaida, nilienda pia kwenye mti wangu na kusali tena na tena. Yehova alijibu sala zangu kupitia mzee huyo ambaye alinionyesha maneno ya mstari mmoja katika Biblia. Alinionyesha Mhubiri 5:4, inayosema: ‘Wakati wowote unapoweka nadhiri kwa Mungu, itimize. Unapoweka nadhiri, itimize.’ Nilikuwa nimeweka nadhiri nitamtumikia Yehova kikamili, na niliogopa kwamba kazi hii ingenidhuru kiroho. Kwa hiyo niliamua kukataa kazi hiyo.

 “Licha ya yaliyonipata utotoni, nilifaulu kuwa mtu mzima! Sasa ninaishi kwa furaha pamoja na mume wangu, Jaser, na mwana wetu, Connor, ambaye ana umri wa miaka tisa. Jaser ni mzee, na Connor ni mhubiri ambaye hajabatizwa. Nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa karibu miaka 27.

 “Mara nyingi mimi hufikiria yale mazungumzo marefu niliyokuwa nayo na Yehova juu ya mwaloni katika vichaka nyuma ya nyumba yetu. Nilimsihi Yehova anisaidie, naye amefanya hivyo kwa njia ya pekee. Ameniimarisha, akanifariji, na kuniongoza. Katika maisha yangu yote, Yehova amenionyesha tena na tena kwamba yeye ni baba wa pekee sana. Ninafurahi kwamba nilichagua kumtumikia kwa moyo wangu wote. Huo ndio uamuzi wenye hekima zaidi ambao nimewahi kufanya.”