Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nina Amani na Mungu Pamoja na Mama Yangu

Nina Amani na Mungu Pamoja na Mama Yangu

MAMA aliniuliza, “Kwa nini huabudu mababu zako? Je, hujui kwamba uko hai leo kwa sababu yao? Hutaki hata kuwashukuru? Unawezaje kuacha desturi ambazo zimekuwepo kwa vizazi vingi? Kukataa kuabudu mababu ni sawa na kusema kwamba ibada yetu ni upumbavu.” Kisha akaanza kulia.

Mama hakuwa na kawaida ya kuzungumza hivyo. Isitoshe, yeye ndiye aliyepanga nijifunze Biblia, ingawa alifanya hivyo ili kuepuka kujifunza na Mashahidi. Sikuzote nilimtii mama yangu, hivyo ilikuwa vigumu kwangu kukataa kufuata mwongozo wake. Hata hivyo, katika kisa hiki sikuwa na budi kufanya hivyo ili nimfurahishe Yehova. Haikuwa rahisi, lakini Yehova alinipa nguvu.

KUJIFUNZA KUMHUSU YEHOVA

Kama Wajapani wengi, sisi pia tulikuwa Wabudha. Baada ya kujifunza na Mashahidi wa Yehova kwa miezi miwili tu, nilisadiki kwamba Biblia ina ujumbe wa kweli. Kutambua kwamba nilikuwa na Baba wa mbinguni, kulinichochea nitake kumjua. Mimi na Mama tulizungumzia kwa shangwe mambo niliyojifunza. Nilianza kuhudhuria mikutano ya Jumapili kwenye Jumba la Ufalme. Ujuzi wangu wa kweli ulipoongezeka, nilimweleza Mama kwamba sitaendelea kushiriki katika desturi za Wabudha. Ghafla Mama akabadilika. Alisema hivi: “Ni aibu kubwa kuwa na mshiriki wa familia ambaye hawaheshimu mababu zetu.” Alitaka niache kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano. Sikuwahi kutarajia kama mama angesema hivyo! Alikuwa amebadilika kabisa.

Kitabu cha Waefeso sura ya 6 kilinifundisha kwamba Yehova anataka niwatii wazazi wangu. Baba alimuunga mkono Mama. Mwanzoni nilifikiri kwamba nikiwasikiliza, wao pia watanisikiliza, na hivyo kurudisha amani katika familia yetu. Wakati huohuo, nilihitaji kujitayarisha kwa ajili ya mitihani ya kuingia shule ya sekondari. Hivyo nilikubali kufanya kama walivyotaka kwa miezi mitatu, lakini nilimwahidi Yehova kwamba ningeanza kuhudhuria mikutano tena muda huo utakapokwisha.

Uamuzi wangu haukuwa mzuri kwa sababu mbili. Kwanza, nilifikiri kwamba katika kipindi hicho, hisia zangu hazingebadilika. Lakini nilianza kupata njaa ya kiroho, na uhusiano wangu na Yehova uliathirika sana. Pili, badala ya Mama na Baba kulegeza msimamo wao, waliendelea kunishinikiza niache kila kitu kilichohusiana na ibada ya kweli.

MSAADA NA UPINZANI

Katika Jumba la Ufalme, nilikutana na wengi ambao walikabili upinzani kwenye familia zao. Walinihakikishia kwamba Yehova angeniimarisha. (Mt. 10:34-37) Walinieleza kwamba nilikuwa na fursa nzuri ya kuisaidia familia yangu ipate wokovu. Hivyo nilianza kusali kwa bidii na kujifunza jinsi ya kumtegemea Yehova.

Familia yangu ilinipinga kwa njia tofauti tofauti. Mama alijaribu kunisihi na kunipa sababu za kuacha kujifunza. Kwa kawaida, sikumjibu chochote, kwa kuwa nilipozungumza, mara nyingi tulishindwa kudhibiti hisia, kwa sababu kila mmoja alitaka kutetea hoja zake. Huenda hali ingetulia kama ningejali zaidi hisia na imani ya mama. Wazazi wangu waliniongezea kazi za kufanya ili nisipate nafasi ya kwenda popote. Wakati mwingine walininyima chakula au walifunga mlango ili nisiingie ndani.

Mama aliomba msaada kwa watu wengine. Alizungumza na mwalimu wangu, ambaye hakuunga mkono upande wowote. Alinipeleka kwa meneja wake kazini ili ajaribu kunisadikisha kwamba dini zote hazina thamani. Nyumbani, mama aliwapigia simu watu wa familia na kuwaomba msaada huku akilia. Jambo hilo lilinikasirisha, lakini nilipohudhuria mikutano wazee walinisaidia kufikiria watu ambao Mama alikuwa akiwatolea ushahidi bila yeye kujua.

Isitoshe, nilihitaji kuamua ikiwa nitaenda chuo kikuu au la. Wazazi wangu walitaka niende chuo kwa sababu walifikiri huo ndio msingi wa maisha bora. Walitumaini kwamba ningepata kazi nzuri. Kwa kuwa hatukuweza kuzungumzia jambo hilo kwa utulivu, niliwaandikia Mama na Baba barua kadhaa ili kuwaeleza malengo yangu. Baba alinitishia hivi kwa hasira: “Ikiwa unafikiri unaweza kupata kazi, basi uwe umeipata kufikia kesho, la sivyo uondoke nyumbani kwangu.” Nilisali kwa Yehova. Nilipokuwa utumishi siku iliyofuata, dada wawili walinipa kazi ya kuwafundisha watoto wao. Baba hakufurahishwa na jambo hilo naye akaacha kabisa kuzungumza nami; alianza kunipuuza. Mama alisema kwamba afadhali ningekuwa mhalifu kuliko kuwa Shahidi wa Yehova.

Yehova alinisaidia kurekebisha njia yangu ya kufikiri na kujua jambo la kufanya

Wakati mwingine nilijiuliza ikiwa Yehova alitaka nipinge maoni ya wazazi wangu kwa kadiri hiyo. Lakini kusali na kutafakari mara nyingi Maandiko yanayozungumzia upendo wa Yehova, kulinisaidia kuwa na mtazamo unaofaa na kuelewa kwamba wazazi wangu walinipinga kwa sababu walikuwa na wasiwasi. Yehova alinisaidia kurekebisha njia yangu ya kufikiri na kujua jambo la kufanya. Pia, kadiri nilivyozidi kushiriki katika huduma, ndivyo nilivyozidi kuifurahia. Naam, niliweka lengo la kuwa painia.

KUTUMIKIA NIKIWA PAINIA

Dada fulani walipojua kwamba nilitaka kuwa painia, walinishauri nisubiri hadi wazazi wangu watakapotulia. Nilisali ili nipate hekima, nilifanya utafiti, nilichunguza nia yangu na kuzungumza na ndugu na dada wakomavu. Nilikata shauri kwamba ninataka kumfurahisha Yehova. Zaidi ya hilo, kuahirisha kuanza upainia hakungemaanisha kwamba wazazi wangu wangebadili mtazamo wao.

Nilianza upainia nilipokaribia kumaliza elimu ya sekondari. Baada ya kufanya upainia kwa muda fulani, niliweka lengo la kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Lakini Mama na Baba hawakutaka niondoke nyumbani. Kwa hiyo nilisubiri hadi nilipofikisha umri wa miaka 20. Kisha, ili kumwondolea Mama wasiwasi, niliiomba ofisi ya tawi inipe mgawo kusini mwa Japani, ambako tulikuwa na watu wa ukoo.

Katika mgawo huo, nilifurahi kuona watu kadhaa ambao nilijifunza nao wakibatizwa. Wakati huohuo nilijifunza Kiingereza nikiwa na lengo la kuongeza utumishi wangu. Kulikuwa na ndugu wawili ambao walikuwa mapainia wa pekee katika kutaniko letu. Niliona bidii yao na jinsi walivyowasaidia wengine. Hivyo, niliweka lengo la kuwa painia wa pekee. Katika kipindi hicho, Mama alipatwa na matatizo makubwa ya kiafya. Kila alipougua, nilirudi nyumbani ili kumtunza. Hilo lilimshangaza, naye akabadili kidogo mtazamo wake.

BARAKA TELE

Baada ya miaka saba, nilipokea barua kutoka kwa Atsushi, mmoja wa mapainia wa pekee waliotajwa awali. Alisema kwamba alikuwa akifikiria kufunga ndoa na alitaka kujua hali na hisia zangu kuhusu jambo hilo. Sikuwahi kuvutiwa kimahaba na Atsushi, na sikufikiri kwamba alivutiwa nami. Mwezi mmoja baadaye, nilimjibu kwamba nilikuwa tayari tujuane vizuri. Tulitambua kwamba tulikuwa na malengo yaliyofanana; sote tulitaka kuwa watumishi wa wakati wote na tulikuwa tayari kutumikia katika mgawo wowote. Baada ya muda, tulioana. Nilifurahi sana Mama, Baba, na watu kadhaa wa familia walipohudhuria harusi yetu!

Nepal

Muda mfupi baadaye, tulipokuwa tungali mapainia wa kawaida, Atsushi aliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Punde si punde, tulipokea baraka nyingine. Tulipewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee, na kisha Atsushi akawekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko. Baada ya kuzungukia makutaniko yote mara moja, tulipokea simu kutoka ofisi ya tawi. Tuliulizwa, ‘Je, mtakubali mgawo wa kuzungukia makutaniko nchini Nepal?’

Kutumikia katika nchi mbalimbali kumenifundisha mambo mengi kumhusu Yehova

Sikujua wazazi wangu wangehisije kuhusu suala la mimi kuhamia nchi nyingine. Kwa hiyo niliwapigia simu, na Baba ndiye aliyeipokea. Alisema hivi: “Unaenda eneo zuri sana.” Juma moja tu mapema, rafiki yake alimpa kitabu kinachozungumzia nchi ya Nepal, naye alikuwa ameanza kufikiria kutembelea huko.

Tulipokuwa tukifurahia mgawo wetu pamoja na watu wachangamfu nchini Nepal, tulipokea baraka nyingine. Nchi ya Bangladesh iliongezwa kwenye mzunguko wetu. Nchi hiyo iko karibu sana na Nepal lakini inatofautiana katika mambo mengi. Huduma ya shambani ilifanywa kwa njia tofauti tofauti. Baada ya miaka mitano, tulipewa mgawo wa kurudi Japani, ambako sasa tunafurahia kuzungukia makutaniko.

Kutumikia katika nchi ya Japani, Nepal, na Bangladesh kumenifundisha mambo mengi kumhusu Yehova! Kila moja ya nchi hizo ina historia na utamaduni wa pekee. Isitoshe, kila mtu katika nchi hizo ni wa pekee. Nimejionea jinsi ambavyo Yehova anawatunza watu, anawakubali, anawasaidia na kuwabariki.

Kwa upande wangu, Yehova amenibariki kwa kuwa amenisaidia nimjue, amenipa kazi ya kufanya, na ameniwezesha kupata mume mwenye sifa nzuri za Kikristo. Mungu ameniongoza nifanye maamuzi mazuri, na sasa nina uhusiano mzuri pamoja naye na familia yangu. Ninamshukuru Yehova kwa sababu mimi na Mama yangu tumekuwa tena marafiki. Nafurahi sana kwamba sasa nina amani na Mungu pamoja na mama yangu.

Tunafurahia sana kuzungukia makutaniko