Hamia kwenye habari

Joseph Asindikizwa na Polisi

Joseph Asindikizwa na Polisi

Ikiwa wewe ni Shahidi wa Yehova, je, unaweza kuwazia kusindikizwa na polisi unapohubiri habari njema nyumba kwa nyumba? Hivyo ndivyo hali ilivyokuwa Joseph alipokuwa akihubiri katika eneo la Micronesia mnamo 2017. Yeye na Mashahidi wengine watatu walikuwa wakishiriki kampeni ya pekee ya kuwafikia watu katika visiwa vya mbali.

Saa sita hivi mchana, Mashahidi hao wanne walifika kwenye kisiwa kidogo ambacho kilikuwa na watu 600 hivi. Meya wa kisiwa hicho alifika kuwapokea ufuoni. Joseph anaeleza kilichotokea baada ya hapo: “Meya alisema kwamba gari la polisi linaweza kutupeleka kwenye kila nyumba. Tulishangazwa na jambo hilo, lakini tukakataa kwa heshima. Tulitaka kuwatembelea watu nyumba kwa nyumba kwa njia ya kawaida.”

Wahubiri hao wakaanza kutembea, wakiwa wameazimia kuzungumza na watu wengi kadiri iwezekanavyo. Mashahidi hao wanasema hivi: “Watu walitukaribisha na walipendezwa na ujumbe wetu. Kwa sababu hiyo, tulitumia muda mwingi kuliko tulivyotarajia katika kila nyumba.”

Baadaye siku hiyo, gari la polisi lilimpita Joseph mara mbili lakini mara ya tatu likasimama. Polisi mmoja akamuuliza Joseph ikiwa angembeba kwa gari kwenda nyumba ambazo bado hajazifikia. Joseph anasema: “Nilikataa. Lakini pindi hii walisisitiza wakisema, ‘Umebakisha muda mfupi sana kabla ya kuondoka kisiwa hiki, kwa hiyo tutakupeleka kwenye nyumba zilizosalia.’ Nisingaliweza kukataa tena kwa sababu nilikuwa nimebakisha nyumba nyingi. Tulipokaribia kila nyumba, maaskari hao wangeniambia jina la familia hiyo na kuniambia ikiwa hakuna mtu angefungua mlango, wangepiga honi ili kumjulisha mwenye-nyumba.

“Kwa msaada wao, tulifaulu kutembelea nyumba zote siku hiyo. Tuliacha machapisho mengi na kufanya mipango ya kuwarudia watu walioonyesha upendezi.”

Polisi hao walimwambia Joseph kwamba “walifurahia sana kueneza habari fulani njema.” Mashahidi walipokuwa wakiondoka jua lilipokuwa likitua, maaskari waliokuwa ufuoni waliwapungia mikono wakiwa wanatabasamu na wakiwa wameshika machapisho ya Biblia katika mkono mwingine.