Hamia kwenye habari

Anawafariji Wengine Licha ya Matatizo Yake ya Afya

Anawafariji Wengine Licha ya Matatizo Yake ya Afya

 Clodean, Shahidi wa Yehova anayeishi nchini Afrika Kusini, alipelekwa hospitalini ili afanyiwe upasuaji mkubwa. Alikuwa na matatizo mengi ya kiafya na alihitaji kuamua matibabu ambayo angekubali. Kabla na hata baada ya kufanyiwa upasuaji, alihisi uchovu, maumivu, na alikuwa na mkazo. Majuma kumi hivi baada ya kurudi nyumbani, bado hangeweza kuketi. Na kwa sababu ya janga la COVID-19, wageni hawangeweza kumtembelea.

 Clodean hakutaka kujisikitikia, basi alimwomba Mungu ampe nguvu ya kuwafariji wengine. Alipoweza tu kuketi, aliwasiliana na dada ya jirani yake, ambaye pindi moja alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi lakini akaacha. Clodean alishiriki naye wazo lenye kutia moyo kutoka kwenye Neno la Mungu, na hilo lilimchochea mwanamke huyo aanze tena kujifunza. Clodean alieleza umuhimu wa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na wakati uleule alihakikisha kwamba mwanafunzi wake anafaulu kujiunga na mikutano ya kutaniko kupitia mtandao. Mwanamke huyo alihudhuria mkutano na hata akatoa maelezo katika sehemu ya maswali na majibu.

 Clodean alizungumza pia na dada mdogo wa mwanafunzi wake, ambaye pia alitaka kujifunza Biblia. Hata alimwambia Clodean kuhusu wengine ambao pia wangependa kujifunza Biblia. Matokeo yakawaje? Clodean alianzisha mafunzo ya Biblia na wanawake wengine wanne. Lakini mambo yakawa mazuri hata zaidi!

Clodean

 Kwa sababu Clodean alipendezwa na wengine, alifaulu kuanzisha mafunzo ya Biblia na wanawake wengine kumi, wakati wa janga hili. Maana yake ni kwamba Clodean alikuwa akijifunza na wanawake 16. Baadhi yao wanahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida kupitia mtandao. Kuwa na mengi ya kufanya kunamsaidia Clodean asifikirie sana hali yake. Pia anahisi kwamba Yehova, “Mungu wa faraja yote,” alimfariji katika majaribu yake yote, na hivyo, yeye pia ameweza kuwafariji wengine.​—2 Wakorintho 1:3, 4.

 Wanafunzi wa Clodean wanahisije kuhusu mambo ambayo wamejifunza? Mmoja wao anasema: “Nimefaidika sana. Lakini faida kubwa zaidi ilikuwa kujifunza jina la Mungu. Hilo limenisaidia kumkaribia Yehova.” Mwanamke wa kwanza ambaye Clodean aliwasiliana naye, anatazamia kubatizwa hivi karibuni. Mambo hayo yamempatia Clodean shangwe nyingi. Na pia sasa amepata nafuu.