Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

INDONESIA

Painia Jasiri

André Elias

Painia Jasiri
  • ALIZALIWA 1915

  • ALIBATIZWA 1940

  • HISTORIA FUPI Painia jasiri aliyesimama imara alipohojiwa na kutishwa na wenye mamlaka.

WAKATI wa vita vya Pili vya Ulimwengu, Ndugu Elias na mke wake, Josephine, walifikishwa mbele ya maofisa wa Sukabumi, Java Magharibi, makao makuu ya jeshi la polisi la Japani lililoitwa Kempeitai. André alihojiwa kwanza. Aliulizwa maswali mengi sana. “Mashahidi wa Yehova ni nani? Je, mnapinga serikali ya Japani? Je, wewe ni mpelelezi?”

André alijibu hivi: “Sisi ni watumishi wa Mungu Mweza-Yote na hatujafanya kosa lolote.” Ofisa huyo mkuu alichomoa upanga ukutani na kuuinua juu.

Akafoka hivi kwa nguvu: “Nikuue?” André aliinamisha kichwa chake na kusali kimyakimya. Baada ya kimya kirefu, ofisa huyo aliangua kicheko. “Wewe ni jasiri!” akasema ofisa huyo. Kisha akamhoji Josephine. Alipotoa maelezo yanayofanana na ya André, ofisa huyo akasema: “Nyinyi si wapelelezi. Ondokeni hapa!”

Miezi kadhaa baadaye, André alisalitiwa na “ndugu wa uwongo” na akafungwa gerezani. (2 Kor. 11:26) Kwa miezi kadhaa, aliishi kwa kula makombo aliyookota kwenye sinki la kuoshea vyombo. Hata hivyo, walinzi wa gereza hawakuweza kumfanya avunje utimilifu wake. Josephine alipofaulu kumtembelea gerezani, André alimwambia hivi: “Usiwe na wasiwasi. Iwe wataniua au kuniacha huru, nitabaki mwaminifu kwa Yehova. Ninaweza kutoka hapa nikiwa maiti lakini sio nikiwa msaliti.”

Baada ya kifungo cha miezi sita, André alijitetea mbele ya Mahakama Kuu ya Jakarta na akaachiliwa huru.

Miaka 30 hivi baadaye, serikali ya Indonesia ilipowapiga tena marufuku Mashahidi wa Yehova, mwanasheria wa wilaya, huko Manado, Sulawesi Kaskazini, alimwita André ofisini kwake. “Je, unajua kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku?” akauliza.

“Ndiyo,” André akajibu.

“Je, uko tayari kubadili dini yako?” ofisa huyo akauliza.

André aliinama na kupigapiga kifua chake kwa ujasiri. Akasema hivi kwa sauti ya juu: “Unaweza kung’oa moyo wangu, lakini kamwe huwezi kunifanya nibadili dini yangu.”

Mwanasheria wa wilaya alimwachilia huru André na hakumsumbua tena.

André alikufa mwaka wa 2000 akiwa na umri wa miaka 85, baada ya kutumikia akiwa painia mwenye bidii kwa miaka 60