Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usalama wa Wanawake​—⁠Maoni ya Biblia

Usalama wa Wanawake​—⁠Maoni ya Biblia

 Mamilioni ya wanawake na wasichana ulimwenguni pote wametendewa vibaya kimwili, kingono, au hata kwa maneno. Je, wewe ni mmoja kati yao? Ona kwa nini usalama wako ni muhimu kwa Mungu na kile ambacho atafanya kuhusu dhuluma ambayo wanawake wamekabili.

 “Nilipokuwa mtoto, ndugu yangu mkubwa alinitendea vibaya kimwili na kunitukana kila siku. Baada ya kuolewa, mama mkwe aliendelea kunitendea vibaya. Yeye na baba mkwe walinitendea kama mtumwa wao. Nilianza kufikiria kujiua.”—Madhu, a India.

 Shiriki la Afya Ulimwenguni linasema kwamba “jeuri dhidi ya wanawake imeenea ulimwenguni pote.” Inakadiriwa kwamba mwanamke mmoja kati ya watatu amewahi kutendewa kwa jeuri kimwili au kingono wakati fulani maishani mwake.

 Ikiwa umewahi kupatwa na hali hiyo, huenda usijihisi salama. Huenda ukahisi kwamba popote utakapoenda utadhulumiwa kimwili, kingono, au hata kwa maneno. Kwa kuwa wanawake wanatendewa vibaya hivyo, huenda ukahisi kwamba watu wengi wanaamini ‘Wanawake si muhimu.’ Lakini je, kweli wanawake ni muhimu kwa maoni ya Mungu?

Biblia inaonyesha kwamba usalama wa wanawake ni muhimu kwa Mungu

Mungu ana maoni gani kuwahusu wanawake?

 Andiko: “Mwanamume na mwanamke [Mungu] aliwaumba.”—Mwanzo 1:27.

 Maana: Mungu aliwaumba wanaume na wanawake. Maoni yake ni kwamba wote wanastahili kuheshimiwa. Isitoshe, anatarajia mume ‘ampende mke wake kama anavyojipenda mwenyewe,’ badala ya kujaribu kumdhibiti, na pia asimtendee kwa jeuri wala kumrushia maneno makali. (Waefeso 5:33; Wakolosai 3:19) Ni wazi basi kwamba usalama wa wanawake ni muhimu kwa Mungu.

 “Nilipokuwa mtoto, nilitendewa vibaya kingono na watu wa ukoo. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, mwajiri wangu alitisha kunifuta kazi ikiwa nisingefanya ngono naye. Nilipokuwa mtu mzima, nilitendewa bila heshima na mume wangu, wazazi wangu, na majirani. Lakini hatimaye nilijifunza kumhusu Yehova, b Muumba wangu. Yeye anawaheshimu wanawake. Hilo lilinithibitishia kwamba ananipenda na kwamba mimi ni mwenye thamani machoni pake.”—Maria, Argentina.

Ni nini kinachoweza kukusaidia kuanza kupona kihisia?

 Andiko: “Kuna rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu kuliko ndugu.”—Methali 18:24.

 Maana: Rafiki wa kweli atakutegemeza. Ikiwa inafaa, mweleze hisia zako mtu unayemwamini.

 “Kwa miaka 20 sikumwambia mtu yeyote kwamba nilikuwa nimetendewa vibaya kingono. Kwa sababu hiyo, nikakosa furaha, nikawa na wasiwasi, na kuvunjika moyo. Lakini hatimaye nilipomweleza hisia zangu mtu aliyekuwa tayari kunisikiliza, nilifarijika sana.” —Elif, Uturuki.

 Andiko: ‘Tupa mahangaiko yako yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anakujali wewe.’—1 Petro 5:7.

 Maana: Unaposali, Mungu anasikiliza kwelikweli. (Zaburi 55:22; 65:2) Kwa kuwa anajali, anaweza kukusaidia kuelewa jinsi wewe ulivyo muhimu kwake.

 “Kujifunza kumhusu Yehova kulinisaidia kuanza kupona majeraha ya kihisia niliyokuwa nayo. Sasa ninaweza kusali kwa Mungu na kumweleza hisia zangu zote. Yeye ni kama rafiki anayeelewa kabisa hisia zangu.”—Ana, Belize.

Je, Mungu atakomesha tatizo la kuwatendea vibaya wanawake?

 Andiko: “Yehova . . . [atawatendea] haki mayatima na wale wanaopondwa, ili mwanadamu anayeweza kufa ambaye ni mavumbi asiwaogopeshe tena.” —Zaburi 10:​17, 18.

 Maana: Hivi karibuni Mungu atakomesha ukosefu wote wa haki, kutia ndani ukatili na jeuri dhidi ya wanawake.

 “Nimefarijika sana kujifunza kwamba hivi karibuni Yehova atahakikisha kwamba wanawake na wasichana hawatendewi vibaya tena. Kujua hilo kumenipa amani ya akili.”—Roberta, Mexico.

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu jinsi Biblia inavyotupatia tumaini, kwa nini unaweza kuamini ahadi zake, na jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyowasaidia watu kwa kutumia Biblia leo, omba utembelewe bila malipo.

 Pakua toleo linaloweza kuchapishwa la makala hii.

a Majina yamebadilishwa.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani? ”