Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Nchini Urusi

Walijitoa Wenyewe kwa Hiari—Nchini Urusi

MWAKA wa 1991, Mashahidi wa Yehova nchini Urusi walishangilia sana marufuku ya muda mrefu dhidi ya kazi yao ilipoondolewa na hatimaye kutambuliwa kisheria. Wakati huo, wengi hawakufikiria kuwa idadi ya Mashahidi ingeongezeka mara kumi zaidi na kufikia 170,000! Miongoni mwa wahubiri hao wa Ufalme kuna Mashahidi kutoka nchi nyingine ambao walihamia Urusi ili kusaidia katika uvunaji wa kiroho. (Mt. 9:37, 38) Acheni tusikie maelezo ya baadhi yao.

AKINA NDUGU WAJITOLEA KUYAIMARISHA MAKUTANIKO

Matthew kutoka Uingereza alikuwa na umri wa miaka 28, marufuku ilipoondolewa nchini Urusi. Kwenye kusanyiko la wilaya lililofanywa mwaka huo, kulikuwa na hotuba ambayo ilikazia uhitaji uliokuwepo katika makutaniko ya Ulaya Mashariki. Kwa mfano, msemaji alitaja kutaniko lililo St. Petersburg, Urusi, ambalo lilikuwa na mtumishi wa huduma mmoja na halikuwa na mzee. Hata hivyo, wahubiri walikuwa wakiongoza mamia ya mafunzo ya Biblia! “Baada ya hotuba hiyo,” Matthew anasema, “niliendelea kufikiria kuhusu Urusi, nilisali kwa Yehova hasa kuhusu tamaa yangu ya kuhamia huko.” Alihifadhi kiasi fulani cha pesa, akauza baadhi ya mali zake, na kuhamia Urusi mwaka wa 1992. Alipata matokeo gani?

Matthew

“Changamoto mojawapo ilikuwa lugha,” anaeleza Matthew. “Sikuweza kuzungumza na wengine kwa uhuru kuhusu mambo ya kiroho.” Changamoto nyingine ilikuwa kupata mahali pa kuishi. “Nililazimika kuhama mara nyingi sana, tena hata bila kupewa taarifa mapema.” Licha ya vikwazo hivyo, Matthew anasema hivi: “Kuhamia Urusi ulikuwa uamuzi bora sana niliowahi kufanya.” Anaeleza: “Kwa kutumikia hapa, nimejifunza kumtegemea zaidi Yehova na ameniongoza katika njia nyingi.” Baadaye, Matthew aliwekwa rasmi kuwa mzee na painia wa pekee na sasa anatumikia katika ofisi ya tawi iliyo karibu na jiji la St. Petersburg.

Mwaka wa 1999, Hiroo alihitimu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Japani akiwa na umri wa miaka 25. Mwalimu wake alimtia moyo aende kutumikia kwenye eneo la kigeni. Hiroo alisikia kwamba kuna uhitaji mkubwa nchini Urusi hivyo akaanza kujifunza Kirusi. Pia alichukua hatua nyingine. “Nilienda Urusi kwa miezi sita,” anaeleza. “Kwa kuwa baridi huwa kali sana wakati wa majira ya baridi, nilienda huko mwezi wa Novemba ili nione ikiwa ningeweza kustahimili baridi.” Baada ya kipindi hicho cha baridi kwisha, alirudi Japani na kuishi maisha rahisi sana ili aweze kuhifadhi pesa za kutosha kurudi Urusi na kuishi huko.

Hiroo na Svetlana

Hiroo ameishi Urusi kwa miaka 12 na ametumikia katika makutaniko kadhaa. Nyakati nyingine, alikuwa mzee peke yake kwenye kutaniko lenye wahubiri zaidi ya 100. Kwenye kutaniko fulani, kila juma aliongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi, Funzo la Mnara wa Mlinzi, na vikundi vitano vya Funzo la Kitabu la Kutaniko. Pia alifanya ziara nyingi za uchungaji. Hiroo anasema hivi anapofikiria miaka hiyo: “Nilifurahia sana kuwasaidia ndugu na dada wawe na nguvu zaidi kiroho.” Kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa kulimsaidiaje? Anasema hivi: “Nilikuwa mzee na painia kabla ya kuhamia Urusi, lakini ninahisi nimesitawisha uhusiano mpya kabisa na Yehova baada ya kuja hapa. Nimejifunza kumtegemea Yehova katika kila sehemu ya maisha yangu.” Mwaka 2005, Hiroo alimwoa Svetlana, na wanatumikia pamoja wakiwa mapainia.

Michael na Olga wakiwa na Marina na Matthew

Matthew, mwenye umri wa miaka 34, na mdogo wake Michael, mwenye umri wa miaka 28, wanatokea nchini Kanada. Walipotembelea Urusi walishangaa kuona watu wengi wanaopendezwa wakihudhuria mikutano, lakini kulikuwa na ndugu wachache sana wa kuongoza mikutano. Matthew anasema: “Watu 200 walihudhuria katika kutaniko nililotembelea, lakini mikutano yote iliongozwa na mzee mmoja mwenye umri mkubwa na mtumishi wa huduma mmoja kijana. Hali hiyo ilinifanya nitamani kuhamia eneo hilo ili kuwasaidia ndugu hao.” Alihamia Urusi mwaka 2002.

Miaka minne baadaye, Michael alihamia Urusi, na mara moja alitambua kwamba bado kulikuwa na uhitaji mkubwa sana wa akina ndugu. Akiwa mtumishi wa huduma, aliombwa asaidie kushughulikia hesabu, machapisho, na maeneo. Pia, aliombwa afanye kazi ambayo kwa kawaida hufanywa na mwandishi wa kutaniko, atoe hotuba za watu wote, na asaidie kupanga makusanyiko na kujenga Majumba ya Ufalme. Hadi sasa, bado makutaniko hayo yanahitaji msaada. Ingawa si rahisi kushughulikia migawo mingi, Michael, ambaye sasa ni mzee, anasema hivi: “Ninaridhika sana ninapowasaidia ndugu zangu. Hiyo ndiyo njia bora sana ya kutumia maisha yangu!”

Matthew alifunga ndoa na Marina, na Michael alimwoa Olga. Wote wanne, pamoja na wajitoleaji wengine, wanaendelea kuyasaidia makutaniko yanayozidi kukua.

DADA WENYE BIDII WASAIDIA KATIKA MAVUNO

Tatyana

Mwaka wa 1994, Tatyana alipokuwa na umri wa miaka 16, mapainia wa pekee sita kutoka Jamhuri ya Cheki, Poland, na Slovakia walianza kutumikia kwenye kutaniko lao nchini Ukrainia. Anasema hivi anapowakumbuka: “Walikuwa mapainia wenye bidii, fadhili, urafiki, na waliyajua vizuri Maandiko.” Aliona jinsi Yehova alivyobariki roho yao ya kujidhabihu, na akajiambia hivi, ‘Ningependa kuwa kama wao.’

Akichochewa na mfano mzuri wa mapainia hao, Tatyana alitumia likizo za shule kusafiri na wengine kwenda maeneo ya mbali ambayo hayakuwahi kuhubiriwa, huko Ukrainia na Belarus. Alifurahia sana safari hizo za kwenda kuhubiri hivi kwamba akapanga kupanua utumishi wake kwa kuhamia nchini Urusi. Kwanza, alienda huko kumtembelea dada mmoja aliyekuwa amehamia kutoka nchi nyingine, na pia kutafuta kazi itakayomwezesha kufanya upainia. Baadaye, mwaka 2000, alihamia Urusi. Mabadiliko hayo yalikuwa na changamoto gani?

Tatyana anasema hivi: “Kwa kuwa nisingeweza kugharimia nyumba nzima, nilikodi chumba kwenye nyumba ya mtu. Haikuwa rahisi kuishi katika mazingira hayo. Kuna nyakati ambazo nilitamani kurudi nyumbani. Lakini sikuzote Yehova alinisaidia kutambua kwamba ningefaidika kwa kuendelea na utumishi wangu.” Leo, Tatyana anatumikia akiwa mmishonari nchini Urusi. Anaeleza: “Nimejionea mambo mengi mazuri na kupata marafiki wengi katika miaka ambayo nimetumikia katika nchi ya kigeni. Zaidi ya yote, mambo niliyopitia katika miaka hiyo yameimarisha imani yangu.”

Masako

Masako kutoka Japani, ambaye sasa ana umri wa miaka 50 hivi, alitamani kwa muda mrefu kuwa mmishonari, lakini alishindwa kwa sababu ya matatizo ya afya. Hata hivyo, alipopata nafuu kidogo, alihamia Urusi ili kusaidia katika kazi ya mavuno. Ingawa haikuwa rahisi kupata mahali pazuri pa kuishi na kazi ya uhakika, aliweza kujiruzuku kwa kufundisha Kijapani na kufanya kazi ya kusafisha nyumba za watu ili aendelee na upainia. Ni nini kimemsaidia aendelee kutumikia?

Masako anasema hivi anapokumbuka miaka 14 aliyotumikia nchini Urusi: “Shangwe ninayopata katika utumishi inazidi matatizo yoyote ninayopata. Kuhubiri katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme huchangamsha na kufurahisha sana.” Anaongezea hivi: “Imekuwa ni muujiza kwangu kuona jinsi ambavyo Yehova ameniandalia chakula, mavazi, na mahali pa kuishi kwa miaka yote hiyo.” Mbali na kutumikia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa nchini Urusi, Masako ametumikia pia nchini Kyrgyzstan. Kwa kuongezea, amesaidia vikundi vya Kichina, Kiingereza, na Kiughuri. Sasa anaendelea kutumikia akiwa painia jijini St. Petersburg.

FAMILIA ZAUNGA MKONO NA KUPATA BARAKA

Inga na Mikhail

Kutokana na hali ngumu za kiuchumi, mara nyingi baadhi ya familia huhamia nchi nyingine ili kuboresha hali yao ya kiuchumi. Lakini kama Abrahamu na Sara, baadhi ya familia zimehamia katika nchi za kigeni ili kutimiza malengo ya kiroho. (Mwa. 12:1-9) Wafikirie Mikhail na Inga, wenzi wa ndoa kutoka Ukrainia, ambao walihamia Urusi mwaka 2003. Kwa muda mfupi walipata watu waliokuwa wakitafuta kweli ya Biblia.

Mikhail anaeleza hivi: “Wakati fulani tulihubiri eneo ambalo halikuwa limehubiriwa. Mwanaume fulani mzee alifungua mlango na kuuliza, ‘Ninyi ni wahubiri?’ Tulipomjibu ndiyo, akasema: ‘Nilijua tu siku moja mngekuja. Lazima maneno ya Yesu yatimie.’ Kisha mwanaume huyo akanukuu Mathayo 24:14.” Mikhail anaongezea hivi: “Katika eneo hilo, tulikutana pia na wanawake kumi hivi Wabaptisti, waliokuwa wanyofu na wenye kiu ya kujua kweli. Walikuwa na kitabu Kuishi Milele na walikitumia kujifunza Biblia kila mwisho juma. Tulitumia saa nyingi kujibu maswali yao na kuimba nao nyimbo za Ufalme, pia tukala chakula cha jioni pamoja. Siwezi kusahau mambo hayo.” Mikhail na Inga wanasema kwamba kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme kumewasaidia wamkaribie zaidi Yehova, wawapende sana watu, na kuwa na maisha yenye kuridhisha. Sasa, ndugu anatumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko.

Oksana, Aleksey, na Yury

Mwaka 2007, Yury na Oksana, wenzi wa ndoa kutoka Ukrainia, ambao sasa wana umri wa miaka 30 na kitu, wakiwa na mwana wao Aleksey, mwenye miaka 13, walitembelea ofisi ya tawi nchini Urusi. Wakiwa huko waliona ramani ya Urusi iliyoonyesha maeneo makubwa ambayo hayajahubiriwa. “Baada ya kuona ramani hiyo,” anasema Oksana, “tulitambua kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Jambo hilo lilitusaidia tuweke azimio la kuhamia nchini Urusi.” Ni jambo gani lingine lililowasaidia? Yury anasema: “Kusoma makala za machapisho yetu, kama vile ‘Je, Unaweza Kutumikia Katika Eneo la Kigeni?’ kulitusaidia sana. * Tulitembelea eneo ambalo ofisi ya tawi ilipendekeza tuhamie nchini Urusi na tukatafuta kazi na mahali pa kuishi.” Mwaka 2008, walihamia nchini Urusi.

Mwanzoni, haikuwa rahisi kupata kazi, na walihama mara nyingi kutoka nyumba moja hadi nyingine. Yury anasema hivi: “Tulisali mara kwa mara ili tusife moyo, kisha tukaendelea kuhubiri, tukitegemea kabisa msaada wa Yehova. Tuliona jinsi Yehova alivyotutunza tulipotanguliza kwanza masilahi ya Ufalme wake. Utumishi huo uliimarisha familia yetu kiroho.” (Mt. 6:22, 33) Kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa kumemsaidiaje Aleksey? “Kumemsaidia sana,” anasema Oksana. “Alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa akiwa na umri wa miaka tisa. Kuona kwamba kuna uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme kunamchochea afanye upainia msaidizi kila anapokuwa likizo. Tunafurahia sana kwa kuwa anaipenda huduma na anahubiri kwa bidii.” Sasa, Yury na Oksana ni mapainia wa pekee.

“JAMBO PEKEE NINALOJUTIA”

Kama maelezo ya wafanyakazi hao wa mavuno yanavyoonyesha, unahitaji kumtegemea kabisa Yehova ili kupanua utumishi wako kwa kuhamia katika maeneo mengine. Kwa kweli, wale wanaotumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wanapata changamoto nyingi katika eneo lao jipya, lakini pia wanapata shangwe kubwa kwa kuwahubiria ujumbe wa habari njema watu wenye mioyo minyofu. Je, unaweza kusaidia kazi ya mavuno kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme? Ukiamua kufanya hivyo, baada ya muda mfupi utahisi kama Yury, ambaye alisema hivi kuhusu uamuzi wake wa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa: “Jambo pekee ninalojutia ni kutofanya uamuzi huo mapema zaidi.”

^ fu. 20 Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1999, ukurasa wa 23-27.