Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ikiwa Kingsley Anaweza, Mimi Pia Ninaweza!”

“Ikiwa Kingsley Anaweza, Mimi Pia Ninaweza!”

BAADA ya kuguswa begani, Kingsley anaanza kusoma Biblia—mgawo wake wa kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Anatamka kila neno vizuri bila kuruka herufi hata moja. Lakini haangalii Biblia yake! Kwa nini?

Kingsley, anayeishi huko Sri Lanka, ni kipofu. Pia, ana matatizo ya kusikia na anatumia kiti cha magurudumu. Alijifunzaje kumhusu Yehova na kustahili kujiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Acheni niwasimulie.

Nilipokutana na Kingsley, nilivutiwa sana na jinsi alivyotamani kujua kweli ya Biblia. Tayari alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi kadhaa, na kitabu chake Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, cha maandishi ya vipofu, kilikuwa kimechakaa sana. * Alikubali kuanza kujifunza tena, lakini tulikabili changamoto mbili.

Kwanza, Kingsley aliishi na watu wengi katika makao ya kuwatunzia wazee na walemavu. Kulikuwa na kelele na Kingsley alikuwa na matatizo ya kusikia, hivyo nililazimika kuongea kwa sauti ya juu. Kila mmoja aliyekuwepo kwenye makao hayo, alisikia tulipokuwa tukijifunza Biblia kila juma!

Pili, Kingsley alikuwa na uwezo wa kusoma na kuelewa habari chache sana kwa wakati mmoja. Ili kufaidika na funzo, Kingsley alijitayarisha vizuri sana. Alisoma habari tena na tena kabla ya funzo, akasoma maandiko katika Biblia yake ya maandishi ya vipofu, kisha alipanga akilini jinsi atakavyojibu maswali. Njia hiyo ilimsaidia sana. Wakati wa funzo, alikaa kwenye zulia akiwa amekunja miguu yake, na alieleza kwa msisimko na kwa sauti ya juu mambo aliyojifunza. Baada ya muda mfupi, tulianza kujifunza mara mbili kwa juma, na tulitumia saa mbili katika funzo.

KUHUDHURIA NA KUSHIRIKI KATIKA MIKUTANO

Kingsley na Paul

Kingsley alitamani kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme, lakini haikuwa rahisi kufanya hivyo. Alihitaji kusaidiwa kupanda na kushuka kwenye kiti cha magurudumu na kwenye gari. Pia, alihitaji kusaidiwa kuingia na kutoka Jumba la Ufalme. Watu wengi kutanikoni walimsaidia kwa zamu, na walifurahia kufanya hivyo. Wakati wa mikutano, Kingsley alikaa karibu na msemaji, alisikiliza kwa makini, na hata alitoa maelezo!

Baada ya kujifunza kwa muda fulani, Kingsley aliamua kujiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Majuma mawili kabla ya hotuba yake ya kwanza ya usomaji wa Biblia, nilimuuliza ikiwa alifanya mazoezi. Alijibu hivi kwa uhakika, “Ndiyo, Ndugu, nimekuwa nikifanya mazoezi mara 30 hivi.” Nilimpongeza na nilimwomba asome mbele yangu. Alifungua Biblia yake, akaweka vidole kwenye maandishi ya vipofu, na kuanza kusoma. Hata hivyo, niligundua kwamba vidole vyake havikwenda sambamba na yale aliyokuwa akisoma. Alikuwa amekariri usomaji wote wa Biblia!

Nilistaajabu huku nikitiririkwa na machozi. Nilimuuliza Kingsley aliwezaje kukumbuka usomaji huo wote baada ya kufanya mazoezi mara 30 tu. Alijibu hivi: “Hapana, nimekuwa nikifanya mazoezi mara 30 kwa siku.” Kwa zaidi ya mwezi mmoja, Kingsley alisoma tena na tena usomaji huo wa Biblia mpaka akaukariri.

Kisha siku ya kutoa mgawo wake kwenye Jumba la Ufalme ikafika. Alipomaliza kutoa mgawo wake, kutaniko lilipiga makofi kwa shangwe, na wengi walitokwa na machozi. Mhubiri mmoja ambaye aliacha kushiriki katika shule kwa sababu ya wasiwasi, aliomba kujiandikisha tena. Kwa nini? Alisema, “Ikiwa Kingsley anaweza, mimi pia ninaweza!”

Septemba 6, 2008, baada ya kujifunza Biblia kwa miaka mitatu, Kingsley alionyesha wakfu wake kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Alikuwa Shahidi mwaminifu mpaka alipokufa Mei 13, 2014. Kingsley alikuwa na uhakika kwamba katika dunia Paradiso, ataendelea kutumikia kwa uaminifu akiwa na nguvu na afya kamili. (Isa. 35:5, 6)—Limesimuliwa na Paul McManus.

^ fu. 4 Kilichapishwa mwaka wa 1995; lakini sasa hakichapishwi tena.