Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uamuzi Niliofanya Utotoni

Uamuzi Niliofanya Utotoni

 

Nilipokuwa mvulana

Mwaka wa 1985, nilipokuwa na umri wa miaka kumi, watoto fulani kutoka Kambodia walijiunga na shule yetu huko Columbus, Ohio, Marekani. Mmoja kati ya wavulana hao alijua maneno machache ya Kiingereza. Kwa kutumia picha, alinisimulia mambo mengi yenye kutisha kuhusu mateso, mauaji, na jinsi walivyokimbia hali hiyo. Nililia usiku kila mara nilipokumbuka watoto hao. Nilitaka kuwaambia kuhusu tumaini la Paradiso na la ufufuo, hata hivyo hawakujua Kiingereza. Ingawa nilikuwa mvulana tu, niliamua kujifunza Kikambodia ili niwahubirie wanashule wenzangu kumhusu Yehova. Uamuzi huo ulikuwa na matokeo mazuri sana maishani mwangu.

Haikuwa rahisi kujifunza Kikambodia. Mara mbili, niliamua kuacha kujifunza lugha hiyo, lakini Yehova alinitia moyo kupitia wazazi wangu. Baada ya muda, walimu na wanafunzi wenzangu walianza kunihimiza nifuatilie elimu ya juu ili nipate kazi nzuri ya kimwili. Kwa kuwa nilitaka kufikia mradi wangu wa kuwa painia, nilichagua masomo ya sekondari ambayo yangenisaidia kupata kazi ya muda. Kwa kawaida nilihubiri na mapainia kila siku nilipotoka darasani. Nilijitolea pia kuwafundisha wanafunzi fulani Kiingereza, na kufanya hivyo kulinisaidia sana baadaye.

Nilipokuwa na umri wa miaka 16, niliambiwa kwamba kuna kikundi cha lugha ya Kikambodia huko Long Beach, California, Marekani. Nilienda huko na kujifunza kusoma Kikambodia. Baada tu ya kuhitimu shule nikawa painia na kuendelea kuwahubiria Wakambodia walioishi karibu nasi. Nilipofikisha umri wa miaka 18, nilianza kufikiria kuhamia Kambodia. Ingawa eneo hilo lilikuwa hatari, nilijua kwamba ni wachache tu kati ya watu milioni kumi nchini Kambodia waliokuwa wamesikia habari njema ya Ufalme. Wakati huo, kulikuwa na kutaniko moja tu lenye wahubiri 13 katika nchi nzima. Nilipokuwa na umri wa miaka 19, nilitembelea Kambodia kwa mara ya kwanza. Miaka miwili baadaye, niliamua kuhamia huko. Nilifanya kazi ya muda nikiwa mtafsiri na mwalimu wa Kiingereza huku nikiendelea na huduma. Baadaye, nilipata mke aliyekuwa na miradi kama yangu maishani. Tumefurahia kuwasaidia Wakambodia wengi kujiweka wakfu kwa Mungu.

Yehova amenipa ‘maombi ya moyo wangu.’ (Zab. 37:4) Hakuna kazi nyingine yoyote inayoridhisha sana kama kazi ya kufanya wanafunzi. Katika muda wa miaka 16 ambayo nimeishi Kambodia, kile kikundi kidogo cha watumishi 13 wa Yehova kimeongezeka na sasa kuna makutaniko 12 na vikundi 4 vilivyo mashambani!—Limesimuliwa na Jason Blackwell.