Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imepitwa Ama Ipo Mbele ya Wakati?

Imepitwa Ama Ipo Mbele ya Wakati?

SAYANSI

BIBLIA SI KITABU CHA SAYANSI, LAKINI INATAJA MAMBO AMBAYO YAMEKUJA KUTHIBITISHWA MIAKA MINGI BAADAYE NA WANASAYANSI. CHUNGUZA MIFANO KADHAA.

Je, ulimwengu una mwanzo?

Wakati fulani, wanasayansi mashuhuri waliamini kabisa kwamba ulimwengu hauna mwanzo. Lakini sasa wanakubali wazi kwamba ulimwengu una mwanzo. Biblia ilitaja jambo hilo miaka mingi mapema.—Mwanzo 1:1.

Dunia ina umbo gani?

Nyakati za kale, watu wengi walidhani dunia ni tambarare. Katika karne ya tano K.W.K., * wanasayansi Wagiriki walisema kwamba dunia ni duara. Lakini miaka mia tatu hivi mapema, mwandikaji wa Biblia, Isaya, tayari alikuwa ametaja kuhusu “duara ya dunia,” akitumia neno linaloweza kumaanisha pia “tufe.”—Isaya 40:22; maelezo ya chini.

Je, nyota na vitu vingine vya angani vinaweza kuchakaa?

Aristoto, mwanasayansi Mgiriki wa karne ya nne K.W.K., alifundisha kwamba vitu vilivyomo duniani ndivyo huchakaa, lakini nyota zilizo angani haziwezi kuchakaa wala kubadilika. Maoni hayo yalidumu kwa karne nyingi. Lakini katika karne ya 19, wanasayansi waligundua kwamba kitu chochote, kiwe duniani au angani, huchakaa kadiri muda unavyopita. Mmoja wa wanasayansi hao, Lord Kelvin, alitambua kile ambacho Biblia inasema kuhusu mbingu na dunia: “Zote zitachakaa kama vazi.” (Zaburi 102:25, 26) Kama ambavyo Biblia inafundisha, Kelvin aliamini kwamba Mungu anaweza kuamua kuzuia hali hiyo ya kuchakaa ili kulinda uumbaji Wake.—Mhubiri 1:4.

Sayari kama vile dunia yetu zimeshikiliwa na nini?

Aristoto alifundisha kwamba sayari, nyota, na vyote vilivyo angani viko katika maumbo ya mviringo yanayopitisha mwanga na yaliyoshikana, kila kimoja kikiwa ndani ya kingine na dunia ikiwa katikati kabisa. Kufikia karne ya 18 W.K., wanasayansi walikuwa wameanza kuamini kwamba nyota na sayari zinaning’inia bila kushikiliwa na chochote. Lakini kwenye kitabu cha Ayubu, kilichoandikwa katika karne ya 15 K.W.K., tunasoma kwamba Muumba ‘ameining’iniza dunia mahali pasipo na kitu.’—Ayubu 26:7.

TIBA

INGAWA BIBLIA SI KITABU CHA TIBA, KINA KANUNI KUHUSU AFYA ZILIZOFUNULIWA MAPEMA KABLA WATAALAMU HAWAJAZIGUNDUA.

Kuwatenga wagonjwa.

Sheria ya Musa iliagiza kwamba watu wenye ukoma walipaswa kutengwa na wengine. Madaktari walijifunza kutumia kanuni hiyo miaka 700 hivi iliyopita, kulipotokea mlipuko wa magonjwa ya kuambukiza, na bado inatumika hadi leo.—Mambo ya Walawi, sura ya 13 na 14.

Kunawa baada ya kugusa maiti.

Hadi kufikia mwishoni mwa karne ya 19, madaktari walikuwa na kawaida ya kushughulikia maiti na kisha kuwahudumia wagonjwa bila kunawa mikono. Zoea hilo lilisababisha vifo vingi. Hata hivyo, Sheria ya Musa ilisema kwamba mtu yeyote aliyegusa maiti alikuwa asiye safi. Kwa kuongezea, iliagiza kwamba maji yalipaswa kutumiwa ili kumfanya mtu huyo awe safi. Kwa kweli, mazoea hayo ya kidini yalisaidia kutunza afya.—Hesabu 19:11, 19.

Kuondoa takataka.

Kila mwaka, vifo vya watoto zaidi ya laki tano hutokea kutokana na ugonjwa wa kuharisha, hasa kwa sababu ya kuwa katika mazingira ambayo hakuna mifumo mizuri ya kuondoa kinyesi. Sheria ya Musa iliagiza kinyesi kichimbiwe na kufunikwa mbali na makazi ya wanadamu.—Kumbukumbu la Torati 23:13.

Umri unaofaa kutahiriwa.

Sheria ya Mungu ilisema kwamba mtoto wa kiume alipaswa kutahiriwa katika siku ya nane baada ya kuzaliwa. (Mambo ya Walawi 12:3) Inaeleweka kwamba, uwezo wa damu kuganda hufikia kiwango kinachofaa baada ya juma la kwanza la mtoto. Katika nyakati za Biblia, hata kabla ya maendeleo ya kitiba, kumtahiri mtoto juma moja baada ya kuzaliwa lilikuwa jambo la busara lililolinda uhai wake.

Uhusiano kati ya hali ya kihisia na afya ya mwili.

Watafiti wa mambo ya tiba na wanasayansi husema kwamba hisia nzuri kama vile kuwa na shangwe, tumaini, shukrani, na utayari wa kusamehe huboresha afya ya mwili. Biblia inasema: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka humfyonza mtu nguvu.”—Methali 17:22.

^ fu. 7 Ufupisho wa K.W.K. unamaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida,” na W.K. unamaanisha “Wakati wa Kawaida.”