Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwenzi wa Ndoa Anapofanya Uzinzi

Mwenzi wa Ndoa Anapofanya Uzinzi

“Nilitamani kufa mume wangu aliponiambia ananiacha ili amwoe mwanamke mwingine mwenye umri mdogo. Niliona amenitendea isivyo haki kabisa, hasa nilipokumbuka jinsi nilivyojidhabihu kwa ajili yake.”​—Maria, Hispania.

“Mke wangu aliponiacha ghafla, nilihisi kana kwamba sehemu fulani ya mwili wangu imekufa. Ndoto zetu, matarajio yetu, mipango yetu; vyote vilitokomea. Kuna nyakati nilihisi jambo hilo halinihangaishi, lakini hali ya kusononeka ilijirudia tena na tena.”​—Bill, Hispania.

INAUMIZA sana mwenzi wa ndoa anapofanya uzinzi. Baada ya kuombwa msamaha, wenzi fulani wameamua kuwasamehe wenzi wao waliowasaliti, na kujenga upya uhusiano wao. * Lakini iwe ndoa hiyo itasitawi tena au la, wenzi wanaogundua kwamba mwenzao ametoka nje ya ndoa, huhisi maumivu makali sana. Hivyo basi, mtu aliyesalitiwa anaweza kukabilianaje na maumivu hayo?

MAANDIKO YANAYOWEZA KUKUSAIDIA

Wenzi wengi ambao wamesalitiwa, wamehisi vizuri baada ya kuchunguza Maandiko, licha ya maumivu makali wanayohisi. Wamejifunza kwamba Mungu anaona kilio chao na anahisi uchungu walio nao.​—Malaki 2:13-16.

“Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.”​Zaburi 94:19.

Bill anasema: “Niliposoma andiko hilo, nilimwazia Yehova akinibembeleza kwa wororo, kama ambavyo baba mwenye huruma angefanya.”

“Kwa mtu mshikamanifu unatenda kwa ushikamanifu.”​Zaburi 18:25.

Carmen, ambaye mume wake alikuwa akitoka nje ya ndoa yao kwa miezi kadhaa, anasema: “Mume wangu alinisaliti. Lakini niliamini kwamba Yehova angebaki mshikamanifu kwangu. Hangenivunja moyo.”

“Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua . . . mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu.”​Wafilipi 4:6, 7.

Sasha anasema: “Nilisoma andiko hilo tena na tena. Kadiri nilivyosali, Mungu alinisaidia kupata amani.”

Kuna nyakati ambazo watu wote hao walionukuliwa, walihisi wanaelekea kukata tamaa. Lakini walimtegemea Yehova Mungu na walipata nguvu kupitia Neno lake. Bill alisema hivi: “Imani yangu iliniwezesha kuwa na kusudi la kuishi wakati ambapo nilihisi maisha yangu yamevurugika. Licha ya kwamba kwa kipindi fulani nilitembea ‘katika bonde lenye kivuli kizito,’ Mungu alikuwa pamoja nami.”—Zaburi 23:4.

^ Ili kujua mengi zaidi kuhusu uamuzi wa kusamehe au kutomsamehe mwenzi aliyekusaliti, soma mfululizo wenye kichwa “Mwenzi Anapokosa Uaminifu,” kwenye gazeti Amkeni! la Aprili 22, 1999.