Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu cha Kukunjwa cha Zamani “Chakunjuliwa””

Kitabu cha Kukunjwa cha Zamani “Chakunjuliwa””

Kipande kilichoungua kilichopatikana Ein Gedi hakingeweza kusomeka tangu kilipochimbuliwa mwaka wa 1970. Teknolojia ya 3-D scanning imefunua kwamba kitabu hicho cha kukunjwa kina sehemu fulani ya kitabu cha Mambo ya Walawi, kutia ndani jina la kibinafsi la Mungu

KATIKA mwaka wa 1970, wachimbuzi wa vitu vya kale walichimbua kitabu cha kukunjwa kilichokuwa kimeungua katika eneo la Ein Gedi, nchini Israel, karibu na ufuo wa magharibi wa Bahari ya Chumvi. Walipata kitabu hicho walipokuwa wakichimbua mabaki ya sinagogi fulani ambalo liliteketea kijiji fulani kilipoharibiwa na moto, yaelekea katika karne ya sita W.K. Kilikuwa kimeharibiwa hivi kwamba maandishi hayangeweza kusomeka vizuri; hata hakingeweza kukunjuliwa bila kukiharibu. Hata hivyo, kwa msaada wa teknolojia ijulikanayo kama 3-D scanning, kitabu hicho “kilikunjuliwa.” Na kwa msaada wa programu ya kidijitali ya kusoma picha, habari za kitabu hicho zinaweza kusomwa.

Teknolojia hiyo imefunua nini? Kitabu hicho cha kukunjwa ni maandishi ya Biblia. Mabaki ya kitabu hicho yana baadhi ya mistari ya kwanza-kwanza ya kitabu cha Mambo ya Walawi. Mistari hiyo ina jina la kibinafsi la Mungu katika Kiebrania, lililoandikwa katika herufi za Tetragramatoni. Inaonekana kitabu hicho kiliandikwa muda fulani kati ya mwaka wa 50 W.K. na mwaka wa 400 W.K., jambo linalofanya kitabu hicho kuwa kitabu cha Biblia cha kukunjwa cha zamani zaidi cha Kiebrania kilichowahi kuvumbuliwa tangu kupatikana kwa hati za Qumran. Gil Zohar aliandika hivi katika jarida la The Jerusalem Post, “Kufikia wakati ambapo kipande cha kitabu cha kukunjwa kilichopatikana Ein Gedi chenye maandishi ya kitabu cha Mambo ya Walawi kilipokunjuliwa kidijitali, tayari kulikuwa na pengo la miaka 1,000 kati ya Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vyenye umri wa miaka 2,000, vya wakati wa kipindi cha Hekalu la Pili na Kodeksi ya Aleppo iliyoandikwa katika karne ya 10 W.K.” Kulingana na wasomi, kitabu hicho kilichokunjuliwa kinaonyesha kwamba maandishi ya Wamasora ya kitabu cha Torati “yamehifadhiwa kwa uaminifu kwa maelfu ya miaka, na makosa ya wanakili hayakuingia.”