Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | KUDUMISHA AMANI NYUMBANI

Jinsi ya Kuchangia Amani Katika Familia

Jinsi ya Kuchangia Amani Katika Familia

JE, UNAFIKIRI Biblia inaweza kukusaidia kuchangia amani katika familia yako? Tafadhali linganisha kile ambacho Biblia inasema na mambo ambayo watu waliohojiwa walisema yamewasaidia. Chunguza mambo ambayo yanaweza kukusaidia kuepuka mizozo, kudumisha amani, na kuimarisha uhusiano wenu.

KANUNI ZA BIBLIA ZINAZOCHANGIA AMANI

UWE NA MTAZAMO UNAOFAA KUMWELEKEA MWENZAKO.

“Bila kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi, mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.”Wafilipi 2:3, 4.

“Tumejionea kwamba ni vizuri kumwona mwenzi wako kuwa muhimu kuliko unavyojiona au unavyowaona wengine.”—C. P., aliyefunga ndoa miaka 19 iliyopita.

SIKILIZA KWA MAKINI NA BILA KUKATA KAULI MAPEMA.

“Endelea kuwakumbusha . . . wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.”Tito 3:1, 2.

“Unapomjibu mwenzi wako kwa ukali unatokeza uhasama wa aina fulani kati yenu. Ni muhimu kuheshimu maoni yake na kumsikiliza bila kumhukumu hata ikiwa hukubaliani naye.”—P. P., aliyefunga ndoa miaka 20 iliyopita.

UWE MWENYE SUBIRA NA UPOLE.

“Kwa subira kiongozi hushawishiwa, na ulimi wa upole unaweza kuvunja mfupa.”Methali 25:15.

“Mizozo itatokea, lakini matokeo hutegemea roho unayoonyesha. Tunahitaji kuwa na subira. Tunapofanya hivyo, tumegundua kwamba mambo hutatuliwa.”—G. A., aliyefunga ndoa miaka 27 iliyopita.

USIMPIGE MWENZAKO WALA KUMRUSHIA MANENO.

“Yaondoleeni mbali mambo haya yote kutoka kwenu, ghadhabu, hasira, ubaya, matukano, na maneno machafu kutoka kinywani mwenu.”Wakolosai 3:8.

“Ninamheshimu sana mume wangu kwa uwezo wake wa kujizuia. Sikuzote yeye huwa mtulivu na hanigombezi wala kunitukana.”—B. D., aliyefunga ndoa miaka 20 iliyopita.

UWE TAYARI KUSAMEHE NA KUTATUA MIZOZO UPESI.

“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”Wakolosai 3:13.

“Unapokabili hali ngumu, si rahisi nyakati zote kuwa mtulivu na unaweza kusema au kufanya mambo ambayo yatamuumiza mwenzi wako. Nyakati kama hizo, inafaa sana kusamehe. Huwezi kuwa na ndoa nzuri bila kumsamehe mwenzako.”—A. B., aliyefunga ndoa miaka 34 iliyopita.

UWE NA MAZOEA YA KUTOA BILA KUTAZAMIA KUPEWA.

“Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. . . . Kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”Luka 6:38.

“Mume wangu anajua kinachonipendeza naye sikuzote hunifanyia mambo bila mimi kutazamia. Kwa sababu hiyo, nyakati zote mimi hujiuliza, ‘Ninaweza kufanya nini ili nimfurahishe?’ Hilo limefanya tuwe na pindi nyingi za kucheka pamoja, hadi leo.”—H. K., aliyefunga ndoa miaka 44 iliyopita.

USICHOKE KUENDELEZA AMANI NYUMBANI

Watu hao waliohojiwa na mwandishi wa Amkeni! wanatoka katika familia mbalimbali ambazo zimesaidiwa na Biblia kusitawisha sifa zinazochangia amani nyumbani. * Hata ikiwa baadhi ya watu katika familia zao hawaendelezi amani, wao wamejionea faida ya kuendelea kujitahidi kufanya amani, kwa kuwa Biblia inaahidi: “Wanaoshauri amani wanashangilia.”—Methali 12:20.

^ fu. 24 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi unavyoweza kuwa na familia yenye furaha, ona sura ya 14 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na kinapatikana kwenye www.pr418.com/sw. Pia tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA > MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA.