Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mama Wenye Afya, Watoto Wenye Afya

Mama Wenye Afya, Watoto Wenye Afya

Mama Wenye Afya, Watoto Wenye Afya

MTOTO mwenye afya analala akiwa ametulia mikononi mwa mama yake. Baba yake amefurahi sana. Kwa kuwa tukio hilo lenye kuleta shangwe hutukia mara nyingi sana kila mwaka, ni rahisi kuona kwamba kujifungua mtoto ni jambo la kawaida tu. Kwa kweli, hilo ni tukio la kiasili—kwa hiyo, kwa nini mtu awe na wasiwasi?

Ni kweli kwamba akina mama wengi hujifungua bila matatizo lakini haiwi hivyo nyakati zote. Kwa sababu hiyo, wazazi wenye busara hufanya chochote wanachoweza ili kuepuka matatizo. Kwa mfano, wao hujifunza mambo yanayosababisha matatizo wakati wa kujifungua, wanaenda kliniki ya akina mama waja-wazito, na wanachukua hatua rahisi za kupunguza matatizo wakati wa kujifungua. Acheni tuchunguze baadhi ya hatua hizo kwa undani.

Mambo Yanayosababisha Matatizo Wakati wa Kujifungua

Kisababishi kimoja cha matatizo kwa mama na mtoto wakati wa kujifungua ni kukosa kujitunza vizuri mama anapokuwa mja-mzito. Dakt. Cheung Kam-lau, ambaye ni tabibu wa watoto walio chini ya umri wa mwezi mmoja katika Hospitali ya Prince of Wales huko Hong Kong, anasema kwamba “kutoenda kliniki kabla ya kujifungua kunaweza kuhatarisha mimba.” Pia anasema kwamba “wengi wa akina mama hao hutazamia kujifungua watoto wenye afya na walionenepa, lakini mambo hayatendeki kama walivyotarajia.”

Likizungumza kuhusu matatizo yanayoweza kuwakumba akina mama, jarida Journal of the American Medical Women’s Association linasema kwamba “sababu kuu zinazowafanya akina mama wengi wafe wanapojifungua” ni kuvuja damu nyingi, mtoto kukaa vibaya tumboni, maambukizo, na kupanda sana kwa shinikizo la damu. Hata hivyo, matibabu yanayofanya kazi yanajulikana sana na katika visa vingi “matibabu ya kisasa . . . hayahitaji matumizi ya vifaa tata,” linasema jarida hilo.

Pia, watoto wengi wanaweza kufaidika ikiwa matibabu yanapatikana kwa urahisi. Jarida UN Chronicle linaripoti kwamba “asilimia 66 ya watoto wanaokufa wanapozaliwa vingeweza kuzuiwa ikiwa akina mama na watoto hao” wangepata matibabu “yanayojulikana sana, yanayofaa, na yasiyohitaji vifaa tata.” Kwa kusikitisha, akina mama wengi hawajui la kufanya na hawaendi kwenye kliniki za waja-wazito, linaripoti Shirika la Habari la Philippines.

Utunzaji Bora wa Mama Mja-Mzito na Kitoto Chake

“Akina mama wenye afya hujifungua watoto wenye afya,” linasema jarida UN Chronicle. Pia linasema kwamba mwanamke asipopata huduma nzuri za afya anapokuwa mja-mzito, anapojifungua, na baada ya kujifungua, mtoto wake pia hatapata huduma za afya.

Katika maeneo fulani, huenda ikawa vigumu kwa wanawake waja-wazito kupata huduma nzuri za afya. Huenda akahitaji kusafiri mbali, au asiwe na uwezo wa kugharamia huduma za afya. Hata hivyo, ikiwezekana, mama mja-mzito anapaswa kujaribu kupata huduma nzuri kutoka kwa mtu mwenye ujuzi wa kuwatunza akina mama waja-wazito. Hilo ni muhimu hasa kwa mwanamke anayeishi kupatana na mafundisho yanayopatikana katika Biblia Takatifu, inayosema kwamba uhai wa mwanadamu, kutia ndani uhai wa mtoto ambaye hajazaliwa, ni mtakatifu.—Kutoka 21:22, 23; * Kumbukumbu la Torati 22:8.

Je, kupata huduma nzuri za afya kunamaanisha kwenda kliniki kila juma? La, si lazima. Kuhusu matatizo ya kawaida yanayowapata wanawake wakati wa uja-uzito na wakati wa kujifungua, Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) “liligundua kwamba wanawake walioenda kliniki mara nne tu wakati wa uja-uzito” walipata matokeo yaleyale “kama wanawake walioenda kliniki mara 12 au zaidi.”

Madaktari Wanaweza Kufanya Nini?

Ili mama na mtoto ambaye bado hajazaliwa wawe na afya nzuri zaidi, madaktari, hasa wakunga, huchukua hatua zinazofuata:

▪ Wao huchunguza rekodi za matibabu za mama na kufanya uchunguzi ili kuona kama kunaweza kuwa na hatari na hivyo kuzuia matatizo yanayoweza kumpata mama au mtoto wake.

▪ Wanaweza kupima damu na mkojo ili kuchunguza mambo kama vile upungufu wa damu, maambukizo, ikiwa damu ya mama na mtoto hazipatani, na magonjwa. Magonjwa hayo yanaweza kutia ndani kisukari, surua ya rubella, magonjwa ya zinaa, na ugonjwa wa figo, ambayo yanaweza kufanya shinikizo la damu lipande.

▪ Inapofaa, madaktari wanaweza kupendekeza mgonjwa apewe chanjo dhidi ya magonjwa kama vile homa, pepopunda, na kutopatana kwa damu ya mama na mtoto.

▪ Pia wanaweza kupendekeza atumie vitamini mbalimbali, hasa aina fulani ya vitamini B inayoitwa folic acid.

Madaktari wanapotambua hatari zinazohusiana na mama mja-mzito na kuchukua hatua zinazofaa, au kumsaidia mama kuchukua hatua hizo, wanachangia afya nzuri kwa mama na mtoto wake ambaye bado hajazaliwa.

Kupunguza Hatari Wakati wa Kujifungua

“Wakati hatari zaidi kwa mama mja-mzito ni pindi anapopatwa na maumivu ya kuzaa hadi anapojifungua,” anasema Joy Phumaphi, aliyekuwa naibu msimamizi mkuu wa Shirika la Familia na Jamii la WHO. Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuzuia matatizo mabaya, kutia ndani yale yanayoweza kuhatarisha uhai, wakati huu muhimu? Kwa kweli, hatua hizo ni rahisi, lakini zinapaswa kuchukuliwa mapema. * Hili ni muhimu hasa kwa watu wanaokataa kutiwa damu mishipani kwa sababu zinazotegemea Biblia au kwa wale wanaotaka kuepuka damu kwa sababu ya hatari zake za kitiba.—Matendo 15:20, 28, 29.

Wagonjwa kama hao wanapaswa kufanya yote wanayoweza kuhakikisha kwamba daktari au mkunga wao ana uwezo na uzoefu wa kutumia matibabu mengine badala ya kuwatia damu mishipani. Pia, huenda ikafaa akina mama waja-wazito wahakikishe kwamba hospitali watakamojifungua iko tayari kushirikiana nao. * Unaweza kumwuliza daktari maswali haya mawili: 1. Utafanya nini ikiwa mama au mtoto anapoteza damu nyingi sana au ikiwa kuna matatizo mengine? 2. Utafanya mipango gani ya badala ikiwa hutakuwa karibu mama anapojifungua?

Bila shaka, mwanamke mwenye busara atamwomba daktari ahakikishe kwamba ana kiwango cha juu zaidi cha damu kabla ya wakati wa kujifungua. Ili kuongeza kiwango cha damu cha mgonjwa, daktari anaweza kupendekeza atumie aina mbalimbali za vitamini B na madini ya chuma.

Pia daktari atafikiria mambo mengine mengi. Kwa mfano, mama huyu alipokuwa akienda kliniki, je, aligundua matatizo yoyote ya afya yanayohitaji kuzingatiwa? Je, mwanamke huyo anahitaji kuacha kufanya kazi akiwa amesimama? Je, anapaswa kupumzika zaidi? Je, ni jambo la hekima kwa mwanamke huyo kuongeza au kupunguza uzito au kufanya mazoezi zaidi? Je, anapaswa kukazia uangalifu zaidi usafi wa mwili kutia ndani usafi wa kinywa?

Uchunguzi unaonyesha kwamba mwanamke anapokuwa mja-mzito, magonjwa ya fizi yanaweza kusababisha kifafa kinachotokana na mimba, tatizo baya sana ambalo dalili zake zinatia ndani kupanda ghafula kwa shinikizo la damu, maumivu makali ya kichwa, na kuvimba kwa mwili kwa sababu ya kuongezeka kwa maji. * kifafa kinachotokana na mimba kinaweza kumfanya mama ajifungue kabla ya wakati unaofaa na ndicho kisababishi kikuu cha vifo vya mama na mtoto wakati wa kujifungua, hasa katika nchi zinazoendelea.

Kwa kweli, daktari mwangalifu atakazia fikira dalili yoyote ya maambukizo katika mwanamke mja-mzito. Na anapopata maumivu ya kuzaa kabla ya wakati wake, atapendekeza alazwe hospitalini mara moja, jambo linaloweza kuokoa uhai.

“Wanawake huhatarisha maisha yao ili kutokeza uhai,” anasema Dakt. Quazi Monirul Islam, msimamizi wa Idara ya Kutunza Wanawake Waja-Wazito ya WHO. Lakini utunzaji mzuri wakati mwanamke anapokuwa mja-mzito, wakati wa kujifungua, na mara baada ya hapo unaweza kuzuia matatizo mengi sana, hata kifo. Jambo muhimu zaidi ni kudumisha afya nzuri. Kwa kweli, ikiwa unataka kupata mtoto mwenye afya nzuri, lazima ujitahidi uwezavyo kuwa mama mwenye afya nzuri.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Maandishi ya awali ya Kiebrania yanarejelea kifo cha mama au mtoto ambaye hajazaliwa.

^ fu. 21 Wenzi wa ndoa ambao ni Mashahidi wa Yehova wanaweza kuwasiliana na Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali (HLC) ya Mashahidi wa Yehova katika eneo lao kabla ya kujifungua. Washiriki wa halmashauri hiyo hutembelea hospitali na madaktari ili kuwapa habari kuhusu matibabu yasiyohusisha damu ambayo wagonjwa Mashahidi hukubali. Isitoshe, halmashauri hizo zinaweza kusaidia kumpata daktari anayeheshimu imani ya wagonjwa na aliye na uzoefu wa kutibu wagonjwa bila damu.

^ fu. 24 Ingawa uchunguzi mwingi zaidi unahitaji kufanywa ili kuona ikiwa ugonjwa wa fizi husababisha kifafa kinachotokana na mimba, sikuzote ni jambo la hekima kutunza fizi na meno yako.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Kulingana na tarakimu zilizochapishwa mnamo Oktoba 2007, mwanamke mmoja hufa karibu kila dakika, yaani, wanawake 536,000 kwa mwaka, kwa sababu ya matatizo yanayohusianishwa na uja-uzito.—Hazina ya Idadi ya Watu ya Umoja wa Mataifa

[Blabu katika ukurasa wa 28]

“Kila mwaka watoto milioni 3.3 huzaliwa wakiwa wamekufa na zaidi ya watoto milioni 4 wanaozaliwa hufa baada ya siku 28.”—UN Chronicle

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

 MATAYARISHO KWA AJILI YA KUJIFUNGUA

1. Fanya utafiti mapema ili uchague hospitali, daktari au mkunga kwa hekima.

2. Mtembelee daktari au mkunga wako kwa ukawaida ili usitawishe urafiki na kuaminiana.

3. Tunza sana afya yako. Ikiwezekana, tumia vitamini zinazopendekezwa, lakini epuka dawa zozote isipokuwa ziwe zimependekezwa na daktari. Ni jambo la hekima kuepuka kutumia kileo. “Ingawa watoto walio hatarini zaidi ni wale ambao mama zao hutumia kileo kupita kiasi, bado haijagunduliwa ikiwa kuna kiwango salama cha kileo ambacho mama mja-mzito anaweza kutumia,” inasema Taasisi ya Marekani Inayoshughulikia Matumizi Mabaya ya Kileo na Uraibu.

4. Ikiwa unapata maumivu ya kuzaa kabla ya wakati (kabla ya juma la 37), wasiliana na daktari wako au hospitali utakayojifungulia. Matibabu ya haraka yanaweza kusaidia mtoto asizaliwe kabla ya wakati wake na kuzuia matatizo mengine yanayoweza kutokea. *

5. Andika uamuzi wako kuhusu matibabu ambayo ungependa. Kwa mfano, wengi wameona inafaa kujaza mapema kadi ya mamlaka ya kudumu ya uwakilishi (DPA). Chunguza ni mambo gani yanayokubalika kisheria katika nchi unamoishi.

6. Baada ya kujifungua, tunza afya yako na ya mtoto wako, hasa ikiwa mtoto alizaliwa kabla ya wakati. Mwone daktari wa mtoto mara moja unapoona kuna tatizo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 41 Mara nyingi watoto wanaozaliwa kabla ya wakati wao ambao viungo vyao havitokezi chembe nyekundu za damu za kutosha, hutiwa damu mishipani.