Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 3

Jinsi ya Kuwa Mstahimilivu

Jinsi ya Kuwa Mstahimilivu

USTAHIMILIVU NI NINI?

Mtu mstahimilivu ana uwezo wa kurudia hali yake ya kawaida hata baada ya kukabili changamoto na matatizo. Kadiri mtu anavyokutana na changamoto za maisha, ndivyo anavyositawisha uwezo huo. Kama ambavyo mtoto huanguka mara kadhaa akiwa anajifunza kutembea, anapojifunza jinsi ya kupata mafanikio maishani atapitia changamoto mbalimbali.

KWA NINI USTAHIMILIVU NI MUHIMU?

Baadhi ya watoto huvunjika moyo wanaposhindwa kutimiza walichotaka, wanapopata matatizo, au wanaporekebishwa. Wengine hukata tamaa kabisa. Hata hivyo, wanapaswa kuelewa ukweli huu:

Ustahimilivu utamsaidia mtoto wako kupambana na changamoto za maisha kwa uthabiti.

JINSI YA KUMFUNDISHA MTOTO KUWA MSTAHIMILIVU

Anaposhindwa kutimiza alichotaka.

KANUNI YA BIBLIA: “Mwadilifu anaweza kuanguka mara saba, lakini atainuka tena.”​—Methali 24:16.

Msaidie mtoto wako kuwa na usawaziko. Kwa mfano, atafanya nini ikiwa atapata alama za chini kwenye mtihani shuleni? Huenda akakata tamaa na kusema: “Mimi siwezi kutimiza chochote!”

Ili kumfundisha ustahimilivu, msaidie kufikiria mbinu za kushughulikia tatizo kama hilo wakati mwingine. Kufanya hivyo kutamsaidia asitawishe uwezo wa kumudu tatizo badala ya kuhisi limemlemea.

Wakati huohuo, epuka kumtatulia tatizo lake. Badala yake, msaidie atafute mbinu za kulitatua yeye mwenyewe. Unaweza kumwuliza, “Utafanya nini ili uelewe vizuri zaidi mambo unayofundishwa?”

Matatizo yanapotokea.

KANUNI YA BIBLIA: “Hamjui jinsi maisha yenu yatakavyokuwa kesho.”​—Yakobo 4:14.

Maisha hayatabiriki. Mtu ambaye ni tajiri leo anaweza kuamka maskini kesho; mtu mwenye afya nzuri leo anaweza kuamka mgonjwa kesho. Biblia inasema: “Sikuzote si wenye mbio wanaoshinda mbio, wala wenye nguvu hawashindi vita . . . kwa sababu wakati na matukio yasiyotarajiwa huwapata wote.”​—Mhubiri 9:11.

Ukiwa mzazi, bila shaka wewe hufanya kila unachoweza ili kumlinda mtoto wako asipatwe na matatizo. Lakini ukweli ni kwamba, huwezi kumlinda mtoto wako kutokana na kila jambo baya linaloweza kumpata.

Huenda mtoto wako hajafikia umri wa kupoteza kazi au kupata matatizo ya kiuchumi. Lakini bado unaweza kumsaidia kupambana na matatizo mengine kama vile kuvunjika kwa urafiki au kufiwa na mshiriki wa familia. *

Anaporekebishwa.

KANUNI YA BIBLIA: “Sikiliza mashauri . . . ili uwe na hekima wakati wako ujao.”​—Methali 19:20.

Mtoto wako anaporekebishwa, usihisi anaonewa; ushauri anaopata unaweza kumsaidia kubadili mtazamo au mwenendo fulani usiofaa.

Wewe na mtoto wako mtanufaika ikiwa utamfundisha kukubali ushauri anaopewa. John, ambaye ni mzazi, anasema hivi: “Ikiwa sikuzote unawatatulia watoto matatizo yao, hawatawahi kujifunza. Watafanya kosa moja baada ya lingine, na sikuzote kazi yako itakuwa kutatua matatizo wanayosababisha. Hali hiyo itafanya maisha ya wazazi na ya mtoto kuwa magumu.”

Unaweza kumsaidiaje mtoto wako anufaike anaporekebishwa? Mtoto wako anaporekebishwa, iwe ni shuleni au mahali pengine, epuka kumwambia kwamba ushauri huo si wa haki. Badala yake, unaweza kumwuliza hivi:

  • “Unadhani ni kwa nini umerekebishwa?”

  • “Unaweza kutumiaje ushauri huo?”

  • “Utafanya nini wakati mwingine ukirekebishwa?”

Kumbuka kwamba, ushauri ambao mtoto wako anapewa utamnufaisha sasa na atakapokuwa mtu mzima.

^ fu. 21 Soma makala yenye kichwa “Msaidie Mtoto Wako Akabiliane na Huzuni,” kwenye toleo la Julai 1, 2008, la Mnara wa Mlinzi.