Hamia kwenye habari

Je, Sanda ya Turin Ndicho Kitambaa Ambacho Yesu Alifungwa Alipozikwa?

Je, Sanda ya Turin Ndicho Kitambaa Ambacho Yesu Alifungwa Alipozikwa?

Jibu la Biblia

 Sanda ya Turin haitajwi katika Biblia. Ni kitambaa cha kitani kinachofikiriwa na wengi kuwa kitambaa ambacho Yesu Kristo alifungwa alipozikwa. Kwa sababu ya imani hiyo, sanda hiyo inaonekana kuwa kati ya vitu vitakatifu zaidi katika dini ya Kikristo. Sanda hiyo imehifadhiwa chini ya ulinzi wa hali ya juu sana katika kanisa moja lililoko Turin, Italia.

 Je, masimulizi ya Biblia yanaunga mkono wazo la kwamba Sanda ya Turin ndicho kitambaa kilichotumiwa kumzika Yesu? Hapana.

 Chunguza mambo matatu kuhusu sanda hiyo yanayotofautiana na kile ambacho Biblia inasema.

  1.   Sanda hiyo ni kitambaa kimoja chenye ukubwa wa sentimita 442 kwa 113 iliyozungukwa na kitambaa kidogo cha sentimita 8 kilichoshonwa upande mrefu wa kitambaa.

     Biblia inasema nini: Mwili wa Yesu ulifungwa kwa vitambaa vingi vidogo-vidogo, bali si kitambaa kimoja cha kitani. Kichwa chake kilikuwa kimefungwa kwa kitambaa tofauti. Baada ya Yesu kufufuliwa, mtume mmoja alifika kwenye kaburi tupu na “akaona vile vitambaa vya kitani hapo chini.” Biblia inaendelea kusema: “Kitambaa ambacho Yesu alikuwa amefungwa kichwani hakikuwa pamoja na vitambaa vingine bali kilikuwa kimekunjwa na kuwekwa kando.”​—Yohana 20:​6, 7.

  2.   Sanda ya Turin ina alama zinazodhaniwa kuwa alama za damu kutoka kwenye maiti ambayo haikusafishwa.

     Biblia inasema nini: Yesu alipokufa, wanafunzi wake waliutayarisha mwili wake “kulingana na desturi ya mazishi ya Wayahudi.” (Yohana 19:39-​42) Desturi hiyo ilitia ndani kusafisha mwili na kuupaka mafuta na viungo kabla ya mazishi. (Mathayo 26:12; Matendo 9:​37) Hivyo, wanafunzi wa Yesu waliusafisha mwili kabla ya kuufunga kwa vitambaa.

  3.   Kulingana na Encyclopædia Britannica, sanda hiyo inaonyesha mwili wa mwanamume ulikuwa “umelazwa kwenye upande mrefu wa sanda hiyo kufikia nusu ya kitambaa hicho, kisha nusu ya pili ya kitambaa ikapitishwa kichwani na kuufunika upande wote wa mbele wa mwili.”

     Biblia inasema nini: Wanafunzi wa Yesu walizungumzia kifo chake, kaburi lililokuwa tupu, na ushahidi wa wanawake walioona “maono yasiyo ya kawaida ya malaika waliowaambia kwamba Yesu yuko hai.” (Luka 24:15-​24) Ikiwa sanda ingekuwepo, bila shaka wanafunzi wangeizungumzia pamoja na alama zozote ambazo zilikuwa juu yake. Hata hivyo, Biblia haisemi kwamba walizungumzia jambo lolote kama hilo.

Je, sanda ya Turin inapaswa kuabudiwa?

 Hapana. Hata ikiwa ingekuwa sanda ambayo ilitumiwa kumzika Yesu, bado lingekuwa kosa kuiabudu. Chunguza kanuni za Biblia zinazoeleza kwa nini ni kosa.

  1.   Kufanya hivyo si muhimu. Yesu alieleza hivi: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:​24) Ibada ya kweli haihusishi matumizi ya sanamu za kidini zilizohifadhiwa.

  2.   Sheria inakataza kufanya hivyo. Zile Amri Kumi zinatukataza kuabudu sanamu. (Kumbukumbu la Torati 5:​6-​10) Vivyo hivyo, Biblia inawaamuru hivi Wakristo: “Jiepusheni na sanamu.” (1 Yohana 5:​21) Huenda watu fulani wakasema kwamba sanda hiyo si sanamu bali ni ishara ya imani yao ya kidini. Hata hivyo, ishara kama hiyo inakuwa sanamu mtu anapoiona kuwa takatifu na kuiheshimu sana. a Hivyo, mtu anayetaka kumpendeza Mungu hatajitoa au kuheshimu sana kitu chochote, kutia ndani sanda hiyo.

a Sanamu ni picha, mchoro, au ishara ya kitu kinachoonwa kuwa kitakatifu na kuheshimiwa.