Hamia kwenye habari

“Funguo za Ufalme” Ni Nini?

“Funguo za Ufalme” Ni Nini?

Jibu la Biblia

 “Funguo za Ufalme,” zinawakilisha mamlaka ya kuwafungulia watu njia ya ‘kuingia katika ufalme wa Mungu.’ (Mathayo 16:19; Matendo 14:22) a Yesu alimpa Petro “funguo za ufalme wa mbinguni.” Hilo linamaanisha kwamba Petro alipokea mamlaka ya kufungua habari kuhusu jinsi watu waaminifu, wangeweza kufurahia pendeleo la kuingia katika Ufalme wa mbinguni, wanapopata roho takatifu ya Mungu.

Funguo hizo zilitumiwa kuwafungulia nani?

 Petro alitumia mamlaka kutoka kwa Mungu kufungua njia kwa ajili ya vikundi vitatu ili viingie katika Ufalme:

  1.   Wayahudi na Wayahudi waliogeuzwa imani. Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, Petro aliwatia moyo Wayahudi wamkubali Yesu kuwa yule aliyechaguliwa na Mungu kutawala katika Ufalme wake. Petro aliwaonyesha mambo wanayopaswa kufanya ili waokolewe. Kwa kufanya hivyo, aliwafungulia njia ya kuingia katika Ufalme, na maelfu ‘wakakubali neno lake.’​—Matendo 2:​38-​41.

  2.   Wasamaria. Baadaye, Petro alitumwa kwa Wasamaria. b Kwa mara nyingine alitumia ufunguo wa Ufalme wakati yeye, pamoja na mtume Yohana, ‘waliposali kwa ajili yao wapate roho takatifu.’ (Matendo 8:14-17) Hilo liliwafungulia njia Wasamaria waingie katika Ufalme.

  3.   Watu wa mataifa. Miaka mitatu na nusu baada ya kifo cha Yesu, Mungu alimfunulia Petro kwamba Watu wa Mataifa (wasio Wayahudi) wangekuwa pia na nafasi ya kuingia katika Ufalme. Hivyo, Petro akatumia ufunguo mmoja kuwahubiria Watu wa Mataifa, na hivyo kuwafungulia mlango wapate roho takatifu, wawe Wakristo, na wawe na tumaini la kuwa washiriki wa Ufalme.​—Matendo 10:30-​35, 44, 45.

‘Kuingia katika Ufalme’ kunamaanisha nini?

 Wale ambao ‘wanaingia katika Ufalme’ wanakuwa watawala pamoja na Yesu mbinguni. Biblia ilitabiri kwamba ‘wangeketi juu ya viti vya ufalme’ na ‘kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.’​—Luka 22:29, 30; Ufunuo 5:​9, 10.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu funguo za Ufalme

 Maoni yasiyo sahihi: Petro ndiye anayeamua ni nani atakayeingia mbinguni.

 Ukweli: Biblia inasema kwamba Kristo Yesu, si Petro, ndiye “ambaye amekusudiwa kuhukumu walio hai na wafu.” (2 Timotheo 4:1, 8; Yohana 5:​22) Kwa kweli, Petro mwenyewe alisema kwamba Yesu “ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.”​—Matendo 10:34, 42.

 Maoni yasiyo sahihi: Petro ndiye aliyeamua wakati wa kutumia funguo za Ufalme.

 Ukweli: Yesu alipozungumza kuhusu funguo za Ufalme, alimwambia Petro hivi: “Lolote utakalofunga duniani litakuwa jambo lililofungwa mbinguni, na lolote utakalofungua duniani litakuwa jambo lililofunguliwa mbinguni.” (Mathayo 16:19) Ingawa watu fulani wanaamini kwamba maneno hayo yanamaanisha Petro ndiye angeamua ni maamuzi gani yatakayofanywa mbinguni, vitenzi vya awali vya Kigiriki vinaonyesha kwamba maamuzi ya Petro yangefuata maamuzi yaliyofanywa mbinguni na si kwamba yangetangulia.

 Sehemu nyingine za Biblia zinaonyesha kwamba Petro alitegemea maamuzi yaliyofanywa mbinguni alipokuwa akitumia funguo za Ufalme. Kwa mfano, alifuata maagizo ya Mungu alipokuwa akitumia ufunguo wa tatu.​—Matendo 10:19, 20.

a Nyakati nyingine, Biblia inatumia neno “funguo” kama ishara ya mamlaka na wajibu.​—Isaya 22:20-​22; Ufunuo 3:​7, 8.

b Wasamaria walikuwa katika dini ambayo ilitofautiana na dini ya Kiyahudi lakini ilifuata baadhi ya mafundisho na mazoea ya Sheria ya Musa.