Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | MARIA MAGDALENE

“Nimemwona Bwana!”

“Nimemwona Bwana!”

Maria Magdalene alitazama mbinguni huku akifuta machozi. Bwana wake mpendwa alikuwa akining’inia kwenye mti. Ingawa ilikuwa karibu saa sita mchana wakati wa majira ya kuchipua, “kukawa na giza katika nchi yote mpaka saa tisa”! (Luka 23:44, 45) Akajifunika mabega yake kwa mtandio na kuwakaribia wanawake waliokuwa pamoja naye. Giza hilo lililoendelea kwa saa tatu halingeweza kuwa limesababishwa na kupatwa kwa jua ambako hutokea kwa dakika chache tu. Labda Maria na wengine waliokuwa wamesimama karibu na Yesu walianza kusikia sauti za wanyama wanaotembea usiku ambao kwa kawaida hawasikiki mchana. Baadhi ya watazamaji “wakaogopa sana na kusema: ‘Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.’” (Mathayo 27:54) Huenda wafuasi wa Yesu na watu wengine walifikiri kwamba Yehova alikuwa akionyesha huzuni yake kutokana na jinsi Mwana wake alivyotendewa kikatili.

Ilikuwa vigumu sana kwa Maria Magdalene kutazama kilichokuwa kikiendelea, lakini hangeweza kuondoka. (Yohana 19:25, 26) Lazima Yesu alikuwa na maumivu makali sana. Vilevile, mama ya Yesu alihitaji kufarijiwa na kutiwa moyo.

Kwa sababu ya mambo yote ambayo Yesu alikuwa amemtendea Maria, alichochewa kufanya yote aliyoweza kwa ajili ya Yesu. Wakati fulani alikuwa mwanamke wa kusikitikiwa na aliyekata tamaa, lakini Yesu alibadilisha hali hiyo. Alikuwa amefanya maisha yake yawe yenye kuheshimika na yenye kusudi. Sasa alikuwa mwanamke mwenye imani kubwa. Jinsi gani? Na leo tunajifunza nini kutokana na imani yake?

‘Walikuwa Wakiwahudumia kwa Mali Zao’

Katika Biblia, hadithi ya Maria Magdalene inaanza kwa kupokea zawadi. Yesu alimweka huru kutoka katika kifungo chenye kutisha. Siku hizo, lilikuwa jambo la kawaida kwa watu kupagawa, na roho waovu waliwashambulia watu wengi, hata waliingia ndani ya baadhi yao na kuwaongoza. Hatujui jinsi roho waovu walivyomwathiri Maria Magdalene; tunachojua ni kwamba alikuwa ameingiwa na roho saba waovu, waliomkandamiza. Kwa msaada wa Yesu Kristo, wote walifukuzwa!—Luka 8:2.

Akiwa amewekwa huru na kupata kitulizo cha ajabu, Maria alianza maisha mapya kabisa. Angeonyeshaje kwamba alikuwa na shukrani? Aliamua kuwa mfuasi mshikamanifu wa Yesu. Vilevile alichukua hatua ili kushughulikia uhitaji alioona. Yesu na mitume wake walihitaji chakula, mavazi, na mahali pa kulala usiku. Wanaume hao hawakuwa matajiri, na wakati huo hawakuwa wakifanya kazi ya kimwili. Ili wakazie fikira kazi ya kuhubiri na kufundisha, walihitaji msaada ili kushughulikia mahitaji yao ya kimwili.

Maria na wanawake wengine walisaidia kutimiza mahitaji hayo. Wanawake hao walikuwa “wakiwahudumia kwa mali zao.” (Luka 8:1, 3) Huenda baadhi yao walikuwa wanawake wenye uwezo. Biblia haisemi kama walitayarisha chakula, kufua nguo, au kupanga mahali pa kulala katika kijiji kimoja baada ya kingine. Lakini kwa hiari walitimiza kazi yao ya kuunga mkono kikundi hicho kilichokuwa kikisafiri, ambacho labda kilikuwa na watu 20 hivi. Kazi iliyofanywa na wanawake hao bila shaka ilimsaidia Yesu na mitume wake wakazie fikira kabisa kazi ya kuhubiri. Bila shaka, Maria alijua kwamba hangeweza kumlipa Yesu kwa mambo aliyokuwa amemfanyia—basi wazia shangwe aliyokuwa nayo alipofanya yote aliyoweza!

Leo, huenda watu wengi wakawadharau wale wanaofanya kazi za hali ya chini kwa niaba ya wengine. Lakini Mungu haoni mambo kwa njia hiyo. Wazia jinsi alivyofurahi kumwona Maria akijitoa kabisa kufanya yote aliyoweza ili kumuunga mkono Yesu na mitume wake! Leo pia, Wakristo wengi waaminifu hufurahi kufanya kazi za hali ya chini kwa niaba ya wengine. Nyakati nyingine, tunaweza kumsaidia mtu kwa kutoa msaada hususa au kusema neno lenye kujenga. Yehova anathamini mchango kama huo.—Methali 19:17; Waebrania 13:16.

“Kando ya Mti wa Mateso wa Yesu”

Maria Magdalene alikuwa kati ya wanawake wengi walioambatana na Yesu kwenda Yerusalemu kwa ajili ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. (Mathayo 27:55, 56) Aliposikia kwamba Yesu amekamatwa na kesi yake ikafanywa usiku, bila shaka alishikwa na hofu. Kisha akapata habari mbaya zaidi. Gavana Pontio Pilato, alishinikizwa na viongozi wa Kiyahudi na umati kumhukumu Yesu auawe kifo cha kikatili kwenye mti. Huenda Maria alimwona Bwana wake akiwa amechoka na damu ikimtoka, aking’ang’ana kutembea barabarani, huku akikokota mti mrefu ambao angeuawa juu yake.—Yohana 19:6, 12, 15-17.

Kwenye eneo ambapo Yesu aliuawa, baada ya giza kuingia saa sita mchana, Maria Magdalene na wanawake wengine walikuwa wamesimama “kando ya mti wa mateso wa Yesu.” (Yohana 19:25) Maria, ambaye alikuwa hapo hadi Yesu alipokufa, alimsikia akimwambia mtume Yohana ambaye alimpenda sana amtunze mama yake. Alimsikia Yesu akizungumza na Baba yake kwa uchungu. Na alisikia maneno yake ya ushindi ambayo alisema kabla tu ya kufa, “Imetimizwa.” Maria aliumia sana. Hata hivyo, baada ya Yesu kufa, inaonekana Maria bado alikuwa hapo. Baadaye aliendelea kusimama karibu na kaburi jipya ambamo tajiri aitwaye Yosefu wa Arimathea aliuweka mwili wa Yesu.—Yohana 19:30; Mathayo 27:45, 46, 57-61.

Mfano wa Maria unatukumbusha jambo tunalopaswa kufanya waabudu wenzetu wanapokabili hali ngumu. Huenda tukashindwa kuzuia msiba au kuondoa maumivu ya wale walioathiriwa. Hata hivyo, tunaweza kuonyesha huruma na ujasiri. Katika hali ngumu, kuwepo tu kwa rafiki anayejali kunaweza kufanya mambo yasiwe mabaya sana. Kuwa karibu na rafiki wakati wa taabu kunaonyesha imani kubwa na kunaweza kumfariji sana.—Methali 17:17.

Bila shaka mama ya Yesu alifarijiwa na kuwepo kwa Maria Magdalene

“Nitamwondoa”

Baada ya mwili wa Yesu kulazwa kaburini, Maria alikuwa kati ya wanawake waliotafuta manukato ya ziada ili baadaye waupake mwili wa Yesu. (Marko 16:1, 2; Luka 23:54-56) Kisha baada ya Sabato kwisha, aliamka asubuhi na mapema. Mwazie akitembea kwenye barabara zenye giza akiwa pamoja na wanawake wengine, wakielekea kwenye kaburi la Yesu. Wakiwa njiani, walianza kujiuliza wataliviringishaje jiwe kubwa lililokuwa kwenye mwingilio wa kaburi. (Mathayo 28:1; Marko 16:1-3) Lakini bado waliendelea na safari. Imani yao iliwachochea kufanya kile walichoweza na kumwachia Yehova mambo mengine.

Huenda Maria aliwatangulia wale wanawake wengine na akawa wa kwanza kufika kwenye kaburi. Ghafula alisimama akiwa ameshtuka. Jiwe lilikuwa limeondolewa—na kaburi lilikuwa tupu! Hakupoteza muda, alikimbia kwenda kuwajulisha Petro na Yohana jambo aliloona. Mwazie akisema hivi kwa mshangao huku akihema: “Wamemwondoa Bwana kaburini, nasi hatujui wamemlaza wapi”! Petro na Yohana wakakimbia kuelekea kaburini, wakahakikisha jambo hilo, kisha wakarudi nyumbani kwao. *Yohana 20:1-10.

Maria aliporudi kwenye kaburi, alikaa hapo peke yake kwa muda fulani. Kimya kilichokuwa kwenye kaburi hilo asubuhi hiyo kilimlemea naye akaanza kulia kwa uchungu. Alipochungulia tena ndani ya kaburi, bila kuamini kwamba Bwana hakuwepo, aliona jambo lililomshtua. Malaika wawili waliovaa mavazi meupe walikuwa wameketi hapo! “Kwa nini unalia?” wakamuuliza. Akiwa amechanganyikiwa, akarudia maneno aliyowaambia mitume: “Wamemwondoa Bwana wangu, nami sijui wamemlaza wapi.”—Yohana 20:11-13.

Alipogeuka, alimwona mwanamume fulani akiwa amesimama nyuma yake. Hakutambua ni nani, basi akafikiri kwamba ni mtunza-bustani anayefanya kazi kwenye eneo hilo. Kwa fadhili mtu huyo akamuuliza: “Mwanamke, kwa nini unalia? Unamtafuta nani?” Maria akajibu, “Bwana, ikiwa umemchukua, niambie umemlaza wapi, nami nitamwondoa.” (Yohana 20:14, 15) Fikiria maneno hayo. Je, mwanamke huyo akiwa peke yake angeweza kuubeba mwili wa Yesu Kristo, ambaye alikuwa mwanamume mzito na mwenye nguvu? Maria hakufikiria jambo hilo. Alichojua ni kwamba alipaswa kufanya jambo lolote analoweza kufanya.

“Nitamwondoa”

Tunapopatwa na majonzi na vizuizi ambavyo huenda ikaonekana vinapita uwezo wetu, je, tunaweza kumwiga Maria Magdalene? Ikiwa tutakazia fikira udhaifu na mapungufu yetu, huenda tukalemewa na woga na shaka. Lakini tukiazimia kufanya yote tuwezayo na kumwachia Mungu mambo mengine, tutatimiza mengi kuliko tunavyoweza kuwazia. (2 Wakorintho 12:10; Wafilipi 4:13) Jambo muhimu zaidi ni kwamba tutamfurahisha Yehova. Maria alifanya hivyo na Yehova alimthawabisha kwa njia yenye kustaajabisha.

“Nimemwona Bwana!”

Mwanamume aliyesimama mbele ya Maria hakuwa mtunza-bustani. Wakati fulani alikuwa seremala, kisha akawa mwalimu, na kisha Bwana mpendwa wa Maria. Lakini Maria hakumtambua kwa hiyo, akaanza kugeuka na kuondoka. Maria hangeweza kuwazia jambo lililokuwa limetokea: Yesu alikuwa amefufuliwa akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo. Alikuwa amejivika mwili wa kibinadamu, lakini si mwili ule ambao alikuwa ameudhabihu. Baada ya kufufuliwa kwake, mara nyingi hata wale waliomfahamu vizuri hawangeweza kumtambua.—Luka 24:13-16; Yohana 21:4.

Yesu alimsaidiaje Maria kutambua yeye ni nani? Ni kupitia jinsi alivyomwita jina lake: “Maria!” Maria akageuka haraka na kupaza sauti akisema neno la Kiebrania ambalo bila shaka alikuwa amelitumia kumwita Yesu mara nyingi—“Raboni!” Mwanamume huyo alikuwa Mwalimu wake mpendwa! Alijawa na shangwe. Akamshika na hakutaka kumwachilia.—Yohana 20:16.

Yesu alijua alichokuwa akiwazia. Kwa hiyo, akamwambia: “Acha kuning’ang’ania.” Tunaweza kumwazia akisema maneno hayo kwa fadhili, labda akitabasamu kwa uchangamfu, huku akijaribu kujinasua kwa utaratibu kutoka kwenye mikono ya Maria na kumhakikishia hivi: “Bado sijapanda kwenda kwa Baba.” Muda wake wa kurudi mbinguni haukuwa umefika. Bado kulikuwa na kazi ambayo alipaswa kufanya duniani, na alitaka Maria amsaidie. Kama kawaida, Maria alikuwa akisikiliza kwa makini. Alimwambia hivi: “Nenda kwa ndugu zangu, nawe uwaambie, ‘Ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.’”—Yohana 20:17.

Alikuwa amepewa mgawo mkubwa na Bwana wake! Maria alikuwa kati ya wanafunzi wa kwanza kupata pendeleo la kumwona Yesu aliyefufuliwa, na sasa alipewa pendeleo la kuwajulisha wengine habari hizo njema. Wazia jinsi alivyowatafuta wanafunzi kwa shangwe na bidii. Mwazie akihema na kusema maneno haya ambayo bila shaka yeye na wanafunzi wengine waliyakumbuka kwa muda mrefu baadaye: “Nimemwona Bwana!” Kisha akawaambia mambo yote ambayo Yesu alikuwa amemwambia, akibubujikwa kwa maneno yenye msisimko. (Yohana 20:18) Simulizi lake liliunga mkono maneno ambayo wanafunzi walikuwa wamesikia kutoka kwa wale wanawake wengine walioenda na kuona kaburi tupu la Yesu.—Luka 24:1-3, 10.

“Nimemwona Bwana!”

“Hawakuwaamini Wanawake Hao”

Wanaume hao waliitikiaje ujumbe huo? Mwanzoni hawakuitikia vizuri. Tunasoma hivi: “Waliyaona maneno hayo kama upuuzi, nao hawakuwaamini wanawake hao.” (Luka 24:11) Wanaume hao wenye nia nzuri walikuwa wamelelewa katika jamii ambayo haikuwaamini wanawake; kulingana na desturi za kirabi, mwanamke hakuruhusiwa kutoa ushahidi mahakamani. Huenda mitume walikuwa wameathiriwa na utamaduni wao kuliko walivyofikiri. Lakini Yesu na Baba yake hawana ubaguzi. Walimpa mwanamke huyo pendeleo kubwa sana.

Bila shaka, Maria hakuruhusu itikio la wanaume hao limhuzunishe. Alijua kwamba Bwana wake alimwamini, na hilo lilitosha. Vivyo hivyo, wale wanaomfuata Yesu wamekabidhiwa ujumbe wanaopaswa kuutangaza. Biblia inauita ujumbe huo “habari njema ya Ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Yesu hakuwaahidi wafuasi wake kwamba kila mtu angewaamini au kuthamini kazi yao. Mambo yangekuwa kinyume kabisa. (Yohana 15:20, 21) Kwa hiyo, Wakristo wanapaswa kukumbuka kielelezo cha Maria Magdalene. Ingawa ndugu zake wa kiroho walitilia shaka ujumbe wake, hilo halikupunguza shangwe yake ya kuwaambia habari njema kumhusu Yesu aliyefufuliwa!

Baadaye, Yesu aliwatokea mitume wake, kisha akawatokea wafuasi wake wengi zaidi. Pindi fulani, aliwatokea wanafunzi 500 kwa wakati mmoja! (1 Wakorintho 15:3-8) Bila shaka, imani ya Maria ilizidi kukua kila mara Yesu alipoonekana, iwe Maria alimwona au alisikia kuhusu jambo hilo. Labda Maria Magdalene alikuwa kati ya wanawake waliohudhuria mkutano huko Yerusalemu siku ya Pentekoste wakati ambapo roho takatifu ilimiminwa juu ya wafuasi wa Yesu waliokusanyika.—Matendo 1:14, 15; 2:1-4.

Vyovyote vile, tuna sababu nyingi za kuwa na uhakika wa jambo hili: Maria Magdalene alidumisha imani yake hadi mwisho. Kila mmoja wetu na aazimie kufanya vivyo hivyo! Tutaiga imani ya Maria Magdalene ikiwa tutaonyesha shukrani kwa ajili ya mambo yote ambayo Yesu ametufanyia na kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu huku tukitegemea msaada wa Mungu.

^ fu. 12 Inaelekea kwamba tayari Maria alikuwa ameondoka wakati ambapo wale wanawake wengine walikutana na malaika aliyewaambia kuhusu kufufuliwa kwa Kristo. Kwa sababu ikiwa angekuwepo, bila shaka Maria angewajulisha Petro na Yohana kwamba alikuwa amemwona malaika aliyeeleza kwa nini mwili wa Yesu haukuwepo.—Mathayo 28:2-4; Marko 16:1-8.