Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | ELIYA

Alivumilia Hadi Mwisho

Alivumilia Hadi Mwisho

Eliya alipata habari kwamba Mfalme Ahabu alikuwa amekufa. Tunaweza kumwazia nabii huyo aliyezeeka akigusa ndevu zake huku akitafakari, akikodoa macho yake, na kufikiria makumi ya miaka ambayo alilazimika kukabiliana na mfalme huyo mwovu. Eliya alikuwa amevumilia mengi! Alikuwa ametishwa, akawindwa, na hata alikuwa karibu kuuawa. Matatizo yote hayo yalisababishwa na Ahabu na malkia wake, Yezebeli. Mfalme hakuwa amefanya jambo lolote kumzuia Yezebeli asiwaue manabii wengi wa Yehova. Kwa sababu ya pupa, wenzi hao wa ndoa walikuwa wamepanga njama ya kumuua Nabothi, mwanamume mwadilifu na asiye na hatia pamoja na wana wake. Kwa sababu ya matendo hayo, Eliya alitumwa akatangaze ujumbe wa hukumu dhidi ya Ahabu na familia yake yote ya kifalme. Sasa, maneno ambayo Mungu alikuwa amesema yalikuwa yakitimia. Ahabu alikufa katika njia ileile ambayo Yehova alikuwa ametabiri.​—1 Wafalme 18:4; 21:​1-​26; 22:37, 38; 2 Wafalme 9:​26.

Hata hivyo, Eliya alijua kwamba alihitaji kuendelea kuvumilia. Yezebeli bado alikuwa hai, na aliendelea kuwa na uvutano mbaya juu ya familia yake na taifa lote. Eliya angekabili changamoto nyingine nyingi, naye alikuwa na mengi ya kumfundisha mwandamani wake ambaye angerithi kazi yake, Elisha. Kwa hiyo, acheni tufikirie kuhusu mitatu kati ya migawo ya mwisho ya Eliya. Tunapoona jinsi imani yake ilivyomsaidia kuvumilia, tutaona jinsi tunavyoweza kuimarisha imani yetu wakati wa hizi nyakati ngumu tunamoishi.

Kumhukumu Ahazia

Ahazia, mwana wa Ahabu na Yezebeli, ndiye aliyekuwa akitawala sasa. Badala ya kujifunza kutokana na matendo ya kipumbavu ya wazazi wake, alifuata hatua zao mbovu. (1 Wafalme 22:52) Kama wao, Ahazia aliabudu Baali. Ibada ya Baali iliwafanya watu watende mambo mabaya kama vile kuendeleza ukahaba hekaluni na hata kuwadhabihu watoto. Je, kuna lolote ambalo lingemsadikisha Ahazia kubadili njia zake na kuwafanya watu waache kumtendea Yehova kwa njia hiyo iliyoonyesha ukosefu mkubwa sana wa ushikamanifu?

Msiba ulimpata mfalme huyo kijana aliyekuwa mkaidi. Alianguka chini kupitia kiunzi kilichokuwa katika chumba chake cha darini naye akajeruhiwa vibaya sana. Ingawa uhai wake ulikuwa hatarini, hakutafuta msaada kutoka kwa Yehova. Badala yake, aliwatuma wajumbe katika jiji la Ekroni lililokuwa la maadui wao Wafilisti ili kumuuliza mungu Baal-zebubu ikiwa angepona. Yehova alikasirika sana. Alimtuma malaika akamwambie Eliya aende kukutana na wajumbe hao. Nabii aliwatuma warudi kwa mfalme wakampe ujumbe mkali sana. Ahazia alikuwa ametenda dhambi nzito sana kwa kutenda kana kwamba hakukuwa na Mungu katika Israeli. Kwa hiyo, Yehova aliamua kwamba Ahazia hatatoka katika kitanda chake kamwe.​—2 Wafalme 1:​2-4.

Badala ya kutubu, Ahazia akauliza: “Mtu aliyekuja kukutana nanyi na kusema maneno hayo alikuwaje?” Wajumbe wakafafanua mavazi ya hali ya chini ambayo nabii alikuwa amevaa, naye Ahazia mara moja akasema: “Ni Eliya.” (2 Wafalme 1:​7, 8) Inapendeza kuona kwamba Eliya aliishi maisha rahisi na alitanguliza kumtumikia Mungu hivi kwamba angeweza kutambuliwa kwa mavazi yake ya hali ya chini. Kwa kweli, jambo kama hilo haliwezi kusemwa kumhusu Ahazia au wazazi wake ambao walipenda vitu vya kimwili kwa pupa. Mfano wa Eliya unatukumbusha leo kwamba tunapaswa kuishi kupatana na shauri ambalo Yesu alitoa la kuishi maisha rahisi, jicho letu likizingatia mambo ya maana zaidi.​—Mathayo 6:​22-​24.

Akiwa ameazimia kulipiza kisasi, Ahazia akatuma kikosi cha askari 50 na mkuu wao waende kumkamata Eliya. Walipomkuta Eliya akiwa “ameketi kwenye kilele cha mlima,” * mkuu huyo wa jeshi akamwamrisha Eliya ‘ashuke chini’ katika jina la mfalme​—jambo ambalo huenda lilimaanisha anaenda kuuawa. Wazia hilo! Hata ingawa askari hao walijua kwamba Eliya alikuwa “mtu wa Mungu wa kweli,” walifikiri eti wanaweza tu kumtisha. Walikuwa wamekosea kama nini! Eliya alimwambia hivi huyo mkuu: “Ikiwa kwa kweli mimi ni mtu wa Mungu, moto na ushuke kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na wanaume wako 50.” Kisha Mungu akatenda! “Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukamteketeza pamoja na wanaume wake 50.” (2 Wafalme 1:​9, 10) Msiba uliowapata askari hao ni kikumbusho cha wazi kwamba Yehova haoni kuwa ni jambo dogo kuwatendea watumishi wake kwa dharau au bila heshima.​—1 Mambo ya Nyakati 16:21, 22.

Ahazia akamtuma mkuu mwingine akiwa na wanaume 50. Mkuu huyu wa pili alitenda kwa ukaidi zaidi kuliko yule wa kwanza. Kwanza kabisa hakuwa amejifunza lolote kutokana na kifo cha wale wanaume 51 waliomtangulia, ingawa huenda bado majivu yao yalikuwa kwenye mlima huo. Halafu mbali na kumwamrisha Eliya, kama mwenzake aliyemtangulia alivyomwamrisha kwa kusema “shuka chini,” mkuu huyo aliongezea neno “haraka”! Ulikuwa upumbavu mkubwa kama nini! Yeye na wanaume wake walikufa kama wale wa kikundi cha kwanza. Hata hivyo, mfalme ndiye aliyekuwa na ujasiri wa kipumbavu zaidi. Bila kujali, alituma kikosi cha tatu. Inapendeza kwamba mkuu huyu wa tatu alikuwa mwenye hekima. Alimfikia Eliya kwa unyenyekevu na kumsihi kwamba asimuue yeye na wanaume wake. Eliya, akiwa mtu wa Mungu, bila shaka alitafakari kuhusu rehema ya Yehova alipomjibu mkuu huyo mnyenyekevu. Malaika wa Yehova alimwagiza Eliya aende pamoja na askari hao. Eliya alitii na akarudia kutangaza hukumu ambayo Yehova alikuwa amempa mfalme huyo mwovu. Ahazia alikufa kama Mungu alivyokuwa amesema. Alikuwa ametawala kwa miaka miwili tu.​—2 Wafalme 1:​11-​17.

Eliya alimwonyesha rehema ya Yehova yule mkuu mnyenyekevu

Eliya aliwezaje kuvumilia licha ya kuzungukwa na watu wakaidi? Hilo ni swali muhimu kwetu leo, sivyo? Je, umewahi kukasirika kwa sababu mtu fulani unayempenda alikataa kusikiliza maneno yenye hekima na kusisitiza afuate mwenendo wenye kudhuru? Tunawezaje kuvumilia hali kama hizo zenye kuvunja moyo? Tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na mahali ambapo askari walimkuta Eliya, yaani, “kwenye kilele cha mlima.” Hatuwezi kusema kihususa kwa nini Eliya alikuwa huko juu, lakini tunaweza kusema kwa uhakika kwamba kwa kuwa alikuwa na kawaida ya kusali, Eliya aliona kwamba eneo hilo lisilo na watu lilimpa nafasi nzuri ya kumkaribia zaidi Mungu wake aliyempenda. (Yakobo 5:​16-​18) Sisi pia tunaweza kutenga wakati wa kuwa peke yetu pamoja na Mungu, kusali kwake tukiliitia jina lake na kumweleza matatizo na wasiwasi tunaokabili. Tukifanya hivyo, itakuwa rahisi zaidi kuvumilia wakati watu wanaotuzunguka wanapotenda kwa njia zisizofaa na zinazowadhuru.

Kukabidhi Vazi Lake Rasmi

Wakati ulikuwa umefika wa Eliya kuacha mgawo wake rasmi. Ona jambo alilofanya. Yeye na Elisha walipokuwa wakitoka katika mji wa Gilgali, Eliya alimsihi Elisha abaki huko, naye angesafiri akiwa peke yake kwenda Betheli, lililokuwa kilomita 11 hivi kutoka Gilgali. Elisha alimjibu hivi kwa uthabiti: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama unavyoishi, sitakuacha.” Walipofika Betheli, Eliya alimwambia Elisha kwamba ataenda Yeriko akiwa peke yake, lililokuwa umbali wa kilomita 22 kutoka Betheli. Kwa mara nyingine tena Elisha akajibu kwa uthabiti kwamba hatamwacha. Huko Yeriko, kwa mara ya tatu jambo lilelile likatokea tena kabla ya Eliya kwenda kwenye Mto Yordani uliokuwa kilomita 8 hivi kutoka Yeriko. Kwa mara nyingine tena, Elisha aliyekuwa kijana akajibu kwa uthabiti. Hatamwacha Eliya!​—2 Wafalme 2:​1-6.

Elisha alikuwa akionyesha sifa muhimu, upendo mshikamanifu. Hiyo ni aina ya upendo ambao Ruthu alimwonyesha Naomi, aina ya upendo unaoshikamana na kitu bila kuacha. (Ruthu 1:​15, 16) Watumishi wote wa Mungu wanahitaji sifa hiyo​—hasa leo kuliko wakati mwingine wowote. Je, tunaona umuhimu wake kama Elisha alivyofanya?

Eliya aliguswa moyo sana kuona upendo mshikamanifu wa mwandamani wake aliyekuwa kijana. Kwa sababu hiyo, Elisha alipata pendeleo la kuona muujiza wa mwisho wa Eliya. Wakiwa kando ya kingo za Mto Yordani, ambao husonga kwa kasi na una sehemu fulani zenye kina kirefu, Eliya alipiga maji hayo kwa vazi lake rasmi. Maji yakagawanyika! “Wana 50 wa manabii” walikuwa pia wakitazama muujiza huo. Inaonekana walifanyiza kikundi kilichokuwa kikiongezeka cha wanaume waliokuwa wakizoezwa kuongoza katika ibada safi nchini. (2 Wafalme 2:​7, 8) Huenda Eliya alisimamia mpango huo wa mazoezi. Miaka kadhaa mapema kuna wakati ambapo Eliya alihisi ni yeye tu aliyebaki akiwa mwaminifu nchini kote. Tangu wakati huo, Yehova alikuwa amemthawabisha Eliya kwa sababu ya uvumilivu wake, kwa kumruhusu aone maendeleo makubwa miongoni mwa waabudu wa Yehova.​—1 Wafalme 19:10.

Baada ya kuvuka Mto Yordani, Eliya akamwambia Elisha: “Omba jambo unalotaka nikutendee kabla sijachukuliwa na kukuacha.” Eliya alijua kwamba wakati wake wa kuondoka ulikuwa umefika. Hakumkabidhi shingo upande rafiki yake mwenye umri mdogo mapendeleo na kazi yake muhimu. Badala yake, Eliya alikuwa na hamu ya kumsaidia kwa njia yoyote ambayo angeweza. Elisha aliomba jambo hili moja tu: “Tafadhali, naweza kupata mafungu mawili ya roho yako?” (2 Wafalme 2:9) Hakumaanisha kwamba alitaka kiasi maradufu cha roho takatifu ambayo Eliya alikuwa amepokea. Badala yake, alikuwa akiomba urithi kama ule wa mwana mzaliwa wa kwanza, ambaye kulingana na sheria alipokea urithi mkubwa zaidi, au maradufu, uliolingana na madaraka yake mapya akiwa kichwa cha familia. (Kumbukumbu la Torati 21:17) Akiwa mrithi wa kiroho wa Eliya, aliona uhitaji wa kuwa na roho ya ujasiri kama ya Eliya ili atimize kazi.

Kwa unyenyekevu, Eliya alimwachia Yehova ajibu ombi hilo. Ikiwa Yehova angemruhusu Elisha amwone Eliya anapochukuliwa na Mungu, basi Mungu angekuwa amekubali ombi la Elisha. Na punde si punde, marafiki hao wa muda mrefu walipokuwa wakitembea “huku wakizungumza,” jambo lenye kustaajabisha likatokea!​—2 Wafalme 2:​10,11.

Urafiki wa Eliya na Elisha uliwasaidia wote wawili kuvumilia hali ngumu

Mwangaza wa ajabu ulionekana angani na ukakaribia zaidi na zaidi. Tunaweza kuwazia mngurumo na sauti ya dhoruba ya upepo iliyotokea ghafla, ikifuatiwa na kitu kinachong’aa kilichowakaribia wanaume hao wawili na kuwalazimisha kutengana, labda kwa sababu walichoona kiliwafanya warudi nyuma kwa mshangao. Waliona gari la kukokotwa, liking’aa kana kwamba limefanyizwa kwa moto. Eliya alijua kwamba wakati wake ulikuwa umefika. Je, alipanda gari hilo? Simulizi hilo halisemi. Vyovyote vile, alijihisi akipandishwa juu, juu zaidi angani, na kubebwa na dhoruba hiyo!

Elisha alipigwa na bumbuazi. Kwa sababu alijionea tukio hilo la ajabu, Elisha alijua kwamba Yehova angempa “mafungu mawili” ya roho ya ujasiri ya Eliya. Lakini jambo hilo pia lilimhuzunisha Elisha. Hakujua rafiki yake mwenye umri mkubwa alikuwa ameenda wapi, lakini huenda hakutarajia kumwona tena Eliya. Alisema hivi kwa sauti: “Baba yangu, baba yangu! Gari la Israeli na wapanda farasi wake!” Alitazama huku mwalimu wake mpendwa akitoweka; kisha Elisha akararua mavazi yake kwa huzuni.​—2 Wafalme 2:​12.

Eliya alipoinuliwa angani, je, alisikia kilio cha rafiki yake kijana na labda akatokwa na machozi kidogo? Vyovyote vile, alijua kwamba kuwa na rafiki kama huyo kulimsaidia kuvumilia hali fulani ngumu. Sisi sote tunapaswa kujifunza kutokana na mfano wa Eliya na kuanzisha urafiki na watu wanaompenda Mungu na wanaotaka kufanya mapenzi yake!

Yehova alimhamisha Eliya hadi kwenye mgawo mpya

Mgawo wa Mwisho

Eliya alienda wapi baada ya hapo? Dini fulani zinafundisha kwamba alichukuliwa mbinguni akaishi na Mungu. Lakini hilo haliwezekani. Karne kadhaa baadaye, Yesu Kristo alisema kwamba hakuna mtu yeyote aliyekuwa amepanda kwenda mbinguni kufikia wakati huo. (Yohana 3:13) Kwa hiyo, tunaposoma kwamba “Eliya akapanda kuelekea mbinguni katika dhoruba ya upepo,” lazima tujiulize, Ni mbingu zipi hizo? (2 Wafalme 2:11) Mbali tu na kuwakilisha makao ya Yehova, Biblia inatumia neno “mbingu” kuwakilisha maeneo ya angani yanayozunguka dunia yetu, ambako mawingu hufanyizwa na ndege huruka. (Zaburi 147:8) Eliya alipanda kuelekea mbingu hizo, yaani, alipanda angani. Kisha akaenda wapi?

Yehova alimhamisha nabii huyo mpendwa hadi kwenye mgawo mpya, kwenye ufalme jirani wa Yuda. Biblia inaonyesha kwamba Eliya alikuwa bado akifanya kazi huko, miaka saba hivi baadaye. Mfalme Yehoramu mwovu ndiye aliyekuwa akitawala Yuda wakati huo. Alikuwa amemwoa binti ya Ahabu na Yezebeli, kwa hiyo uvutano wao mwovu bado ulikuwepo. Yehova alimwagiza Eliya aandike barua ya kutangaza hukumu juu ya Yehoramu. Kama ilivyotabiriwa, Yehoramu alikufa kifo kibaya sana. Na jambo baya hata zaidi ni kwamba simulizi hilo linamalizia kwa kusema: “Hakuna mtu yeyote aliyesikitishwa na kifo chake.”​—2 Mambo ya Nyakati 21:12-​20.

Kuna tofauti kubwa sana kati ya mtu huyo mwovu na Eliya! Hatujui Eliya alikufa jinsi gani na wapi. Lakini tunajua hakufa kama Yehoramu alivyokufa, bila mtu kuhuzunikia kifo chake. Elisha alimkosa sana rafiki yake. Manabii wale wengine waaminifu pia walimkosa. Yehova mwenyewe bado alimthamini Eliya miaka 1,000 baadaye, kwa sababu alitokeza maono ya nabii huyo wakati Yesu alipogeuka sura. (Mathayo 17:1-9) Je, ungependa kujifunza kutoka kwa Eliya na kusitawisha imani inayodumu licha ya hali ngumu? Basi, usisahau kuanzisha urafiki na watu wanaompenda Mungu, kutanguliza mambo ya kiroho maishani mwako, na kusali mara nyingi kutoka moyoni. Wewe pia na upate sehemu ya kudumu katika moyo wa Yehova wenye upendo!

^ fu. 6 Wasomi fulani wamesema kwamba mlima unaotajwa hapa ni Mlima Karmeli, ambapo Mungu alimwezesha Eliya kuwashinda manabii wa Baali miaka michache mapema. Hata hivyo, Biblia haisemi waziwazi ulikuwa mlima gani.