Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi Talaka Inavyowaathiri Watoto

Jinsi Talaka Inavyowaathiri Watoto

 Wenzi fulani wa ndoa ambao wana matatizo kati yao hujiambia kwamba talaka itakuwa na manufaa kwa watoto wao. Wanaona ni afadhali kutalikiana kuliko kuwalazimisha watoto kuishi pamoja na wazazi wawili wanaogombana. Ukweli wa mambo unaonyesha nini?

 Talaka huwaathirije watoto?

 Utafiti unaonyesha kwamba watoto huathiriwa vibaya sana wazazi wanapotalikiana. Kuna uwezekano mkubwa zaidi wa watoto ambao wazazi wao wametalikiana kupata madhara yafuatayo:

  •   Kuwa na hasira, mfadhaiko, na kushuka moyo

  •   Kujiendesha kwa njia ambayo inawadhuru wao na watu wengine

  •   Kupata matatizo ya kujifunza wanapokuwa shuleni au hata kuacha shule kabisa

  •   Wana uwezekano mkubwa zaidi wa kuwa wagonjwa

 Mbali na hilo, watoto wengi hujilaumu wakifikiri huenda wao ndiyo waliofanya wazazi wao watalikiane au huenda wangeweza kuzuia hilo lisitokee.

 Matatizo ambayo watoto hupata baada ya wazazi wao kutalikiana huendelea hata wanapokuwa watu wazima. Huenda wakahisi kwamba hawana thamani au huenda ikawa vigumu kwao kuwaamini wengine. Vilevile kuna uwezekano mkubwa sana kwamba wao pia watatalikiana wanakapokabili matatizo katika ndoa zao.

 Jambo kuu: Ingawa watu fulani wanaofikiria kutalikiana hujiambia kwamba hilo litawanufaisha watoto wao, utafiti hauungi mkono maoni hayo. Mtaalamu wa kutunza watoto, Penelope Leach, anaandika hivi: a

 Kanuni ya Biblia: ‘Mwangalie, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.’—Wafilipi 2:4.

 Je, mtoto wetu atakuwa na atakuwa na furaha ikiwa tutatalikiana?

 Huenda watu fulani wangesema ndiyo. Lakini ni vizuri kukumbuka kwamba mahitaji ya mzazi na mahitaji ya mtoto yanatofautiana. Anayefikiria kuhusu talaka, anataka kuanza maisha mapya. Lakini kwa kawaida mtoto hataki maisha yake yabadilike, na anataka kuendelea kuishi pamoja na baba na mama yake.

 Baada ya kuchunguza ndoa nyingi sana za watu waliotalikiana, waandikaji wa kitabu The Unexpected Legacy of Divorce waliandika hivi: “Jambo moja ni wazi: hakuna mtoto aliyesema kwamba ana furaha zaidi. Badala yake wanasema waziwazi, ‘Siku ambayo wazazi wangu walitalikiana, ndiyo siku niliyoacha kuwa na furaha maishani.’” Kitabu hiki kinaongezea kusema kwamba wanaona hawawezi kumtegemea mtu yeyote ulimwenguni, na kwamba ulimwengu unaonekana hatari kwa sababu uhusiano wa watu wawili walio karibu zaidi nao haukudumu.

 Jambo kuu: Kuna uwezekano mdogo sana wa watoto kuwa na furaha baada ya wazazi wao kutalikiana.

 Kanuni ya Biblia: “Roho iliyopondeka humfyonza mtu nguvu.”—Methali 17:22.

 Ninapaswa kujua nini kuhusu kulea watoto pamoja tukiwa tumetalikiana?

 Wenzi fulani wa ndoa waliotalikiana hujaribu kushirikiana majukumu ya kuwalea watoto wao kana kwamba bado wameoana. Hata hivyo, kufanya hivyo si rahisi. Utafiti unaonyesha kwamba wenzi wa ndoa waliotalikiana, mara nyingi:

  •   Hawatumii muda wa kutosha na watoto wao

  •   Wanawafundisha watoto wao viwango vinavyopingana

  •   Huwaruhusu watoto wafanye chochote wanachotaka kwa sababu wanajihisi wakiwa na hatia au kwa sababu wamechoka sana

 Pia, huenda mtoto wa wazazi waliotalikiana akahisi kwamba hahitaji kuwatii wazazi wake. Kwa sababu anahisi kwamba wazazi wake walishindwa kushikamana na viwango bora kama vile, kudumisha ahadi yao ya kuishi pamoja. Huenda basi akajiuliza, ‘Kwa nini niwatii?’

 Jambo kuu: Si rahisi kwa wenzi waliotalikiana kuwalea watoto pamoja. Lakini hali inakuwa ngumu hata zaidi kwa watoto wao.

 Kanuni ya Biblia: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21.

 Je, kuna njia nzuri zaidi ya kushughulikia matatizo ya ndoa?

 Mara nyingi, jitihada nyingi ambazo wenzi wa ndoa hutia baada ya kutalikiana, zingaliweza kutumiwa ili kusuluhisha matatizo katika ndoa yao. Kitabu The Case for Marriage kinasema hivi: “Kwa kuwa ndoa tu ina matatizo, haimaanishi ya kwamba hali itaendelea kuwa hivyo. Baada ya muda kupita, hali katika ndoa nyingi huanza kuwa nzuri na wenzi wa ndoa huanza kuwa na furaha.” Kwa ujumla, watoto huwa na furaha zaidi wazazi wao wanapoendelea kuishi pamoja.

 Hilo halimaanishi kwamba wenzi wa ndoa hawapaswi kutalikiana kamwe. Kwa kweli, Biblia huruhusu wenzi wa ndoa kutalikiana kwa sababu ya uasherati. (Mathayo 19:9) Hata hivyo, Biblia inasema “mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Mume na mke wanapokuwa na matatizo katika ndoa yao wanapaswa kuzingatia hali zote—kutia ndani madhara ambayo watoto wao watakabili kwa sababu ya talaka.

 Bila shaka, huenda mengi zaidi yakahitajika kuliko kuvumilia tu katika ndoa ambayo haina furaha. Biblia inatoa ushauri bora zaidi wa kuwasaidia waume na wake kusitawisha sifa zinazohitajika ili kuwa na ndoa zinazodumu na zenye furaha. Hilo halishangazi, kwa kuwa mtungaji wa Biblia, Yehova, ndiye mwanzilishi wa mpango wa ndoa.—Mathayo 19:4-6.

 Kanuni ya Biblia: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Ninayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”—Isaya 48:17.

a Imetolewa kwenye kitabu Your Growing Child—From Babyhood Through Adolescence