Hamia kwenye habari

APRILI 24, 2024
AFRIKA KUSINI

Maelfu ya Mashahidi Wanashiriki Ujumbe wa Tumaini Kutoka Katika Biblia na Watu Wanaozungumza Lugha ya Kihosa

Maelfu ya Mashahidi Wanashiriki Ujumbe wa Tumaini Kutoka Katika Biblia na Watu Wanaozungumza Lugha ya Kihosa

Kuanzia Januari 29 hadi Machi 11, 2024, zaidi ya ndugu na dada 11,000 wa Afrika Kusini, walishiriki katika kampeni ya kuhubiri katika lugha ya Kihosa kwenye eneo la Eastern Cape. Zaidi ya watu milioni saba wanaoishi katika jimbo hilo wanazungumza Kihosa. Kupitia kampeni hiyo, zaidi ya watu 2,700 waliomba kujifunza Biblia.

Wakati wa kampeni hiyo, akina dada wawili walikutana na mwanamke ambaye majuma mawili kabla ya siku hiyo alikuwa amempoteza ndugu yake katika aksidenti mbaya. Mwanamke huyo alipokuwa akiwaeleza akina dada hao kuhusu kifo cha kaka yake huku machozi yakimtoka, walimfariji kwa kusoma naye andiko la Ufunuo 21:3, 4. Kwa kuwa alitaka kujifunza mengi zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya kuondoa kifo na maumivu, mwanamke huyo aliuliza kuhusu siku na mahali ambapo mikutano yetu inafanyika. Pia, mwanamke huyo akaanza kujifunza Biblia.

Dada anayeitwa Zukiswa alianzisha mazungumzo na mwanamke anayesumbuliwa na ugonjwa mbaya wa yabisi-kavu. Hali yake ilifanya iwe vigumu kwake kutayarisha chakula kwa ajili ya watoto wake. Mwanamke huyo alihofu kwamba watoto wake hawangeweza kula siku hiyo kwa kuwa hakuwa na nguvu za kukanda unga ili kutengeneza mkate. Kwa upendo Zukiswa alikanda donge la mkate huku dada aliyeandamana naye akishiriki ujumbe wa Biblia pamoja na mwanamke huyo. Kwa kuwa alivutiwa na jinsi walivyomjali na kumsaidia kwa upendo, mwanamke huyo aliwaeleza marafiki zake wengi kuhusu mambo ambayo dada hao wawili walikuwa wamemfanyia. Muda mfupi baada ya hapo, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Walipokuwa wakishiriki huduma ya nyumba kwa nyumba katika jiji la Gqeberha, akina ndugu wawili walikutana na mwanamume mmoja ambaye alikuwa na mguu mmoja. Mwanamume huyo alisema kwamba alikuwa akijiuliza kwa nini Mungu alikuwa amemruhusu Shetani kuutawala ulimwengu, hata ingawa wanadamu wametokana na Mungu. (1 Yohana 5:19) Ndugu zetu walijibu maswali yake kwa kutumia Biblia. Baadaye siku hiyohiyo, baada ya kutazama video yenye kichwa Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka?, kwa furaha mwanamume huyo na mke wake walikubali kujifunza Biblia.

Dada yetu mwingine, ambaye alikuwa akihubiri pia katika eneo la Gqeberha, alimuuliza mwanamke mmoja ikiwa angependa kusoma andiko la Zaburi 37:29. Baada ya kusoma mstari huo kutoka katika nakala yake mwenyewe ya Biblia, mwanamke huyo alisema kwamba hajaelewa mstari huo. Kisha dada huyo alimsomea mstari huo kutoka katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kihosa. Mwanamke huyo akasema: “Kihosa kilichotumiwa katika Biblia hii kinaeleweka kwa urahisi. Ninaelewa kwa urahisi zaidi kuliko Biblia yangu!” Sasa mwanamke huyo anafurahia kujifunza Biblia kwa ukawaida.

Tunashangilia kwamba watu wengi wanaozungumza Kihosa nchini Afrika Kusini wanakubali ujumbe wa tumaini ambao “Mungu wa faraja yote” anatufundisha kupitia Neno lake, Biblia.​—2 Wakorintho 1:3.