Ona video zinazopatikana

BIBLIA INABADILISHA MAISHA YA WATU

Nilikuwa Nimeshindwa Kuongoza Maisha Yangu

Nilikuwa Nimeshindwa Kuongoza Maisha Yangu
  • Alizaliwa Mwaka wa: 1971

  • Inchi: Tonga

  • Alikuwa: Anatumia dawa za kulewesha, alifungwa mu gereza

MAISHA YANGU YA ZAMANI

Nilizaliwa mu inchi ya Tonga, inchi yenye iko na visiwa 170 hivi, yenye kupatikana kusini mangaribi mwa Bahari ya Pasifiki. Tulikuwa tunaishi maisha ya mwepesi, hatukukuwa na umeme ao gari. Lakini tulikuwa na maji mu nyumba yetu, na tulikuwa na kuku kidogo. Wakati wa mapumuziko ya masomo, mimi na ndugu zangu wawili tulikuwa tunasaidia baba yetu kufanya kazi mu shamba la familia, mwenye tulilima ndizi, aina fulani ya viazi (ignames), mahole, na mihogo. Baba yangu alitutimizia mahitaji yetu kwa kuuzisha chakula chenye alikuwa anakomalisha na kwa kufanya kazi za kidogo-kidogo. Sawa vile wakaaji wengine wa visiwa, familia yetu ilikuwa inaheshimia sana Biblia, na tulikuwa tunaenda ku kanisa kwa ukawaida. Lakini, tulikuwa hakika kama kusudi maisha yetu ikuwe muzuri, tulipaswa tu kuhamia mu inchi tajiri zaidi.

Wakati nilikuwa na miaka 16, mujomba wangu alifanya mipango juu familia yetu ihamie Kalifornia, Amerika. Haikukuwa mwepesi kabisa kuzoea desturi mupya! Hata kama tulianza kupata feza, tuliishi mu eneo fulani maskini kwenye watu walikuwa wenye jeuri sana na walikuwa wanatumia sana dawa za kulewesha. Mara mingi tulisikia mulio wa bunduki usiku, na majirani wetu wengi waliogopa kushambuliwa na watu wenye jeuri. Watu mingi walikuwa wanabeba bunduki ili kujilinda ao ili kumaliza ugomvi. Ningali na risasi mu kifua changu juu ya ugomvi fulani.

Wakati nilikuwa ku masomo ya segondere, nilipenda kuwa kama vijana wengine. Pole kwa pole, nilianza kujiingiza sana mu karamu za kupita kiasi, kunywa sana, jeuri, na kutumia dawa za kulewesha. Kisha, nilifikia kuwa mutumwa wa kokaine. Nilianza kuiba juu nipate feza za kuuza dawa za kulewesha. Hata kama watu wa familia yangu walikuwa wanaenda sana ku kanisa, sikupata muongozo wenye ungenisaidia nishinde vishawishi vya marafiki wenye walinichochea kufanya mambo ya mubaya. Mara mingi, nilikamatwa juu ya matendo yangu ya jeuri. Nilikuwa nimeshindwa kuongoza maisha yangu! Nilifikia kufungwa mu gereza.

NAMNA BIBLIA ILIBADILISHA MAISHA YANGU

Siku moja, mu mwaka wa 1997, wakati nilikuwa mu gereza, mufungwa mwingine aliniona na Biblia. Ilikuwa siku ya Noeli, siku yenye watu wengi wa Tonga wanaona kuwa takatifu sana. Aliniuliza kama ninajua mambo yenye Biblia inafundisha kabisa juu ya kuzaliwa kwa Kristo, lakini sikujua mambo yenye Biblia inasema. Alinionyesha habari ya mwepesi ya kuzaliwa kwa Yesu yenye inapatikana mu Biblia, na nilivumbua kama desturi mingi zenye kufanywa siku ya Noeli hazitajwe hata mu Biblia. (Matayo 2:1-12; Luka 2:5-14) Nilishangaa sana na nilipenda nijue mambo ingine yenye Biblia inasema. Ule mwanaume alikuwa anahuzuria mikutano ya kila juma yenye Mashahidi wa Yehova walikuwa wanafanya mu gereza, na niliamua kujiunga naye. Walikuwa wanazungumuzia kitabu cha Biblia cha Ufunuo. Hata kama sikuelewa mambo mingi yenye ilikuwa inasemwa, nilitambua kama kila kitu chenye walikuwa wanafundisha kilitoka mu Biblia.

Wakati Mashahidi waliniomba nianze kujifunza nao Biblia, nilikubali kwa furaha. Kwa mara ya kwanza, nilijifunza ahadi ya Biblia yenye kuonyesha kama dunia itakuwa paradiso wakati wenye kuja. (Isaya 35:5-8) Nilitambua waziwazi kama juu nimufurahishe Mungu, nilipaswa kufanya mabadiliko makubwa mu maisha yangu. Nilitambua kama Yehova Mungu hangeniruhusu niingie mu Paradiso yenye ametuahidi kama ningeendelea na tabia zangu za mubaya. (1 Wakorinto 6:9, 10) Kwa hiyo, niliamua kabisa kuacha kukasirika-kasirika, kuacha kuvuta tumbako, na kuacha kunywa pombe sana na kutumia dawa za kulewesha.

Mu mwaka wa 1999, mbele muda wenye nilipaswa kupitisha mu gereza umalizike, wakubwa wa serikali walinihamishia mu kambi ya watu wenye wanapenda kuhamia mu inchi zingine. Kwa zaidi ya mwaka mumoja, sikuonana na Mashahidi. Lakini, niliazimia kuendelea kufanya mabadiliko. Mu mwaka wa 2000, serikali haikuniruhusu tena kuendelea kuishi mu inchi ya Amerika, na nilipelekwa Tonga.

Wakati nilirudia Tonga, nilitafuta sana Mashahidi wa Yehova na nilianza kujifunza tena Biblia. Nilipenda mambo yenye nilikuwa ninajifunza, na nilishangaa wakati nilitambua kama Mashahidi mu kile kisiwa walikuwa wanafundisha mambo yenye inatoka mu Biblia, sawasawa tu na Mashahidi wa inchi ya Amerika.

Baba yangu alikuwa anajulikana sana mu eneo kwenye tuliishi kwa sababu alikuwa na cheo cha juu mu kanisa lake. Njo maana, ku mwanzo, watu wa familia yangu walishangaa sana na kukasirika wakati nilianza kujiunga na Mashahidi wa Yehova. Lakini kisha, wazazi wangu walifurahi kuona namna kanuni za Biblia zilinisaidia niachane na tabia za mubaya.

Sawa vile wanaume wengi wa Tonga, nilipitisha wakati mingi kila juma ili kunywa pombe yenye kuitwa kava

Badiliko moja la nguvu sana lenye nilipaswa kufanya mu maisha yangu ilikuwa kuacha kunywa pombe yenye watu mingi walikuwa wanakunywa sana mu eneo letu. Wanaume mingi wa Tonga walipitisha wakati mingi kila juma ili kunywa kava, pombe yenye kuregeza mwili na kufanya mutu alale usingizi yenye ilitengenezwa na mizizi ya mumea wa pilipili. Sasa, kwa sababu nilikuwa nimerudia mu inchi yangu, nilianza kuenda fasi wanauzisha kava karibu kila mangaribi na nilikuwa ninakunywa kava mupaka wakati nilipoteza ufahamu. Tatizo moja ni kwamba nilichochewa na marafiki wenye hawakuheshimia kanuni za Biblia. Kisha, Mashahidi walinisaidia kujua kama tabia zangu zilimuchukiza Mungu. Nilifanya mabadiliko kusudi nipate baraka za Mungu na kusudi anikubali.

Nilianza kuhuzuria mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova. Kujiunga na wengine wenye walikuwa wanajikaza kumufurahisha Mungu kulinisaidia nishinde vishawishi vya kufanya mambo ya mubaya. Mu mwaka wa 2002, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

FAIDA YENYE NIMEPATA

Uvumilivu wa Mungu wenye Biblia inazungumuzia umeniletea faida. Biblia inasema hivi: “Yehova . . . ni muvumilivu kuwaelekea ninyi kwa sababu hataki mutu yeyote aharibiwe lakini anataka wote wafikie kutubu.” (2 Petro 3:9) Kwa kweli, tayari Mungu angekuwa ameharibu mupangilio huu muovu, lakini ameuacha uendelee juu ya kupatia watu kama mimi nafasi ya kuwa rafiki yake. Ninafurahi wakati ninafikiria namna anaweza kunitumia juu ya kusaidia wengine pia wakuwe marafiki wake.

Yehova amenisaidia niweze kuongoza tena maisha yangu. Siibake tena juu ya kuuza vitu vyenye vinaweza kuniua. Lakini, ninajikaza kusaidia majirani wangu wakuwe pia marafiki wa Yehova. Kujiunga na Mashahidi wa Yehova kulinisaidia nikutane na Tea, bibi yangu mupendwa. Mimi na bibi yangu na mutoto wetu mwanaume, tuko na maisha ya familia yenye furaha sana. Sisi wote pamoja tunafundisha wengine mambo yenye Biblia inasema juu ya tumaini la wakati wenye kuja la kuishi milele mu paradiso yenye amani.