Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

Namna ya Kufariji Watu Wenye Walifiwa

Namna ya Kufariji Watu Wenye Walifiwa

Umekwisha kujisikia kuwa haujue namna ya kusaidia mutu fulani mwenye kuhuzunika kwa sababu ya kifo cha mutu mwenye anapenda? Wakati fulani tunaweza kuona kuwa hatujue tuseme nini ao tufanye nini, kwa hiyo tunabakia bila kusema ao kufanya jambo lolote. Lakini kuko mambo yenye kufaa, na yenye kusaidia ambayo tunaweza kufanya.

Mara nyingi, jambo la lazima ni kuwa hapo na kusema tu maneno mepesi kama vile, “pole sana.” Katika desturi nyingi, kukumbatia mutu mwenye alifiwa ao kumusalimia na mukono kwa upole ni njia ya muzuri ya kuonyesha kama unamuhangaikia. Kama mutu mwenye alifiwa anataka kuzungumuza, umusikilize kwa huruma. Na jambo la muzuri zaidi, ufanye kazi fulani kwa ajili ya watu wa familia wenye walifiwa, pengine kazi yenye hawakuweza kufanya, kama vile kupika chakula, kuhangaikia watoto, ao kusaidia katika mipango ya maziko kama ni lazima kufanya vile. Matendo hayo yanaweza kuwa na matokeo ya muzuri kuliko maneno yenye kupangwa muzuri sana.

Kisha wakati fulani, unaweza kuzungumuza juu ya mutu mwenye alikufa, pengine kwa kukazia sifa zake fulani za muzuri ao mambo fulani ya kufurahisha yenye mulifanya pamoja. Mazungumuzo kama hayo yanaweza hata kufanya mutu mwenye alifiwa acheke kidogo. Kwa mufano, Pam alifiwa na bwana yake, Ian, kumepita miaka sita. Anasema hivi: “Wakati fulani watu wananiambia mambo ya muzuri yenye Ian alifanya yenye nilikuwa sijue, na hilo linafanya moyo wangu ufurahi.”

Kulingana na ripoti moja ya wachunguzi, watu wenye walifiwa wanapata musaada wa kwanza tu, lakini mambo yenye wako nayo lazima yanasahauliwa haraka wakati marafiki wanarudilia mambo yenye kuhusu maisha yao wenyewe. Kwa hiyo, kisha rafiki yako kufiwa, ujikaze kuzungumuza naye mara kwa mara. * Watu wengi wenye walifiwa wanafurahia sana nafasi hiyo ili kumaliza huzuni yao ya muda murefu.

Fikiria mufano wa Kaori, kijana mumoja mwanamuke wa Japani. Alivunjika moyo sana kwa sababu ya kifo cha mama yake na kifo cha dada yake mukubwa mwaka moja na miezi tatu kisha kifo cha mama yake. Jambo la kufurahisha ni hili: marafiki waaminifu waliendelea kumutolea musaada. Mumoja kati yao mwenye kuitwa Ritsuko ni mukubwa sana kumupita. Alifanya naye urafiki wa sana. Kaori anasema hivi: “Kusema kweli, sikufurahia jambo hilo. Sikupenda mutu yeyote akamate nafasi ya mama yangu, na sikuwazia kama mutu fulani angeweza kufanya vile. Lakini, nilifikia kumukaribia sana Mama Ritsuko kwa sababu ya namna alinitendea. Kila juma, tulienda katika kazi ya kuhubiri pamoja na tulienda kwenye mikutano ya Kikristo pamoja. Mara nyingi, aliniita ili tukunywe chai pamoja, aliniletea chakula, na kuniandikia barua. Mawazo ya muzuri ya Mama Ritsuko yalinisaidia sana.”

Kumepita miaka 12 tangu mama yake na Kaori alikufa, na leo yeye na bwana yake ni wahubiri wa wakati wote. Kaori anasema hivi: “Mama Ritsuko anaendelea kunihangaikia. Wakati ninarudia nyumbani, ninamutembelea kila mara na kufurahia urafiki wenye kujenga.”

Poli, Shahidi wa Yehova katika inchi ya Saiprasi, na yeye pia alipata faida kwa sababu wengine waliendelea kumusaidia. Poli alikuwa na bwana muzuri mwenye kuitwa Sozos. Sozos aliweka mufano muzuri wa muchungaji Mukristo; alizoea kualika mayatima na wajane kwenye nyumba yake ili kula na kupitisha wakati pamoja. (Yakobo 1:27) Jambo la huzuni ni hili: wakati Sozos alikuwa na miaka 53 alikufa kwa sababu sehemu moja kwenye ubongo wake ilikuwa yenye kuvimba. Poli anasema hivi: “Nilipoteza bwana yangu muaminifu mwenye nilifanya naye miaka 33 katika ndoa.”

Tafuta namna za kusaidia watu wenye walifiwa

Kisha maziko, Poli alihamia Kanada pamoja na Daniel, mutoto wake mudogo mwanaume wa miaka 15. Huko, walianza kujiunga na kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Poli anakumbuka hivi: “Marafiki katika kutaniko letu mupya hawakujua kitu juu ya maisha yetu ya zamani na juu ya hali zetu ngumu. Hata hivyo, walitukaribia na kutuambia maneno yenye kufariji na kutusaidia. Musaada huo ulikuwa wa maana, zaidi sana wakati huo wenye mutoto wangu mwanaume alikuwa na lazima ya baba yake! Wale wenye kuongoza katika kutaniko walimuhangaikia Daniel sana. Zaidi sana mumoja wao hakumusahau Daniel wakati alipenda kupitisha wakati pamoja na marafiki ao wakati alienda kucheza nao kabumbu.” Leo, mama na mutoto, wote wawili wanaendelea muzuri.

Kwa kweli, kuko namna nyingi za kusaidia na kufariji watu wenye walifiwa. Biblia inatufariji pia kupitia tumaini la muzuri sana la wakati unaokuja.

^ fu. 6 Watu fulani wametia hata alama kwenye tarehe ya kifo cha mutu fulani kwenye kalenda yao ili wakumbuke tarehe hiyo na kufariji mutu mwenye alifiwa wakati anakuwa na lazima zaidi ya kufarijiwa, tarehe hiyo ao wakati inakaribia.