Hamia kwenye habari

Maelfu ya Watu Watembelea Ofisi ya Tawi ya Amerika ya Kati

Maelfu ya Watu Watembelea Ofisi ya Tawi ya Amerika ya Kati

Mnamo 2015, wageni 175,000 hivi walitembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Amerika ya Kati iliyoko Mexico​—huo ni wastani wa watu 670 kwa kila siku ya kazi! Wageni wengi walikuja katika vikundi vikubwa, wakisafiri kwa siku nyingi kwa kutumia basi zilizokodiwa. Wengine walipanga safari zao miezi mingi kabla ya hapo.

“Mradi wa Kutembelea Betheli”

Baadhi ya wale waliotembelea ofisi ya tawi, inayoitwa Betheli, walihitaji kujidhabihu sana. Kwa mfano, washiriki wengi wa kutaniko lililo katika jimbo la Veracruz, Mexico hawakuwa na pesa za kulipia nauli ya basi ya safari hiyo yenye urefu wa kilomita 550. Kwa hiyo walianzisha mradi waliouita “Mradi wa Kutembelea Betheli.” Walipanga vikundi vya kutayarisha na kuuza vyakula. Pia walikusanya chupa za plastiki zilizotumiwa na kuziuza. Baada ya miezi mitatu, walikuwa wamekusanya pesa za kutosha kwa ajili ya safari hiyo.

Je, jitihada zao zilikuwa na faida? Walihisi kwamba walifaidika sana. Kwa mfano, Lucio, kijana katika kutaniko hilo, aliandika hivi: “Kutembelea Betheli kulinifanya nijiwekee miradi mingine ya kiroho, na sasa ninatumika zaidi kutanikoni.” Na Elizabeth, mwenye umri wa miaka 18, alisema: “Tulipokuwa Betheli, nilijionea na kuhisi upendo wa kweli unaowatambulisha wale wanaomtumikia Yehova. Nilichochewa kujitoa zaidi kwa Mungu, kwa hiyo nikawa mhudumu wa wakati wote.”

Maelfu Walikuja

Nyakati nyingine, maelfu ya wageni hufika siku ileile kwa ajili ya matembezi. Wafanyakazi katika Dawati la Matembezi hufanya kazi kubwa ya kuwapokea wote kwa ukarimu. Lizzy anasema: “Inatia moyo kuona ni wangapi wanaokuja. Imani yangu huimarishwa ninapoona uthamini wa wageni na kusikia jinsi walivyojidhabihu ili kutembelea ofisi ya tawi.”

Ili kuwapokea maelfu ya watu wanaokuja, wale walio katika idara nyingine za Betheli hushiriki pia kuwatembeza wageni. Hata ingawa hilo huhusisha kazi ya ziada, wanafurahia kuwapokea wageni. Juan anasema, “Ninapomaliza kuwatembeza na kuona nyuso zenye furaha za wageni ninajua kwamba jitihada zangu zilikuwa na faida.”

“Watoto Wanaipenda Sana”

Watoto pia hufurahia kutembelea Betheli. Noriko, anayefanya kazi kwenye Idara ya Kompyuta, anasema: “Mimi huwauliza watoto katika kikundi ninachotembeza ikiwa wangependa kuja kutumika Betheli. Wote husema, ‘Ndiyo!’” Sehemu ambayo watoto hupenda zaidi ni “Kona ya Caleb.” Hapo, wanaweza kupiga picha na vinyago vya Caleb na Sofia, vibonzo vilivyo katika video za mfululizo wa Uwe Rafiki ya Yehova. “Watoto wanaipenda sana,” anasema Noriko.

Watoto wengi hushukuru sana kwa kazi inayofanywa Betheli. Kwa mfano, Henry, mvulana mdogo nchini Mexico, alihifadhi pesa ili atoe mchango anapokuja Betheli. Aliandika hivi katika barua aliyoambatanisha na mchango huo: “Tafadhali tumieni pesa hizi kutokeza machapisho zaidi. Asanteni kwa kumfanyia Yehova kazi.”

Unakaribishwa Kutembea

Mashahidi wa Yehova wanawakaribisha watu kutembelea ofisi zao za tawi na viwanda vya uchapishaji vilivyoko ulimwenguni pote bila malipo. Ikiwa ungependa kutembelea ofisi fulani ya tawi, unakaribishwa kwa uchangamfu. Tuna uhakika kwamba utafurahia matembezi yako. Unaweza kupata habari zaidi kuhusu matembezi hayo chini ya KUTUHUSU > OFISI NA MATEMBEZI.